KONA YA MALOTO: Huyu ndiye Brian Mundubile, Tundu Lissu wa Zambia

Rais Hakainde Hichilema ataendelea kuiongoza Zambia kwa muhula wa pili. Halikuwa daraja rahisi kuvuka. Mpinzani wake mkuu, Brian Mundubile, amempa ushindani wenye nguvu. Hata hivyo, wastani wa matokeo ambayo wamepata, yanaweza yasionekane yakiakisi ushindani uliokuwapo.

Rais Hichilema amepata kura 2,965,326, ambazo ni asilimia 61 ya waliojitokeza kupiga kura, ambao namba yao ni 5,028,616. Mundibile kura zake ni 1,856,217, asilimia 38. Wagombea wengine 11, hakuna hata mmoja aliyeweza kupata japo asilimia moja ya kura. Dhahiri, ulikuwa uchaguzi wa wawili.

Katika muhula wake wa kwanza, Hichilema aliweza kufanya mageuzi chanya ya kiuchumi. Pamoja na hivyo, Mundubile aliweza kujenga ushawishi kwa umma kwamba ukuaji wa uchumi Zambia hauendani na hali ngumu ya maisha ya wananchi. Ni hoja hii ya ugumu wa maisha na malalamiko kuhusu haki za binadamu, zilizomfanya Mundubile ampe changamoto pevu Hichilema.

Uchaguzi Mkuu wa Zambia 2026, ulikuwa wa saba kwa Hichilema kugombea. Ameshinda mara mbili. Ya kwanza ilikuwa Uchaguzi Mkuu 2021, alipomshinda Rais aliyekuwa madarakani, Edgar Lungu. Kabla ya hapo, Hichilema aligombea urais Uchaguzi Mkuu 2016, alipotoka wa pili nyuma ya Lungu, kwa tofauti ndogo, asilimia 50.4 dhidi ya 47.6. Mwaka 2015, Hichilema alikabiliana na Lungu, kuwania urais ili kumalizia muhula, kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa nchi hiyo, Michael Sata.

Mwaka 2011, Hichilema alikuwa kwenye makaratasi ya kupigia kura za urais Zambia, alipotoka wa tatu nyuma ya Sata, na Rais wa zamani wa nchi hiyo, Rupiah Banda. Mwaka 2008, Hichilema alikuwa wa tatu, nyuma ya Banda, aliyeshinda, na Sata aliyetoka wa pili. Mwaka 2006, ndiyo ilikuwa mara ya kwanza Hichilema kutokeza kuwania urais, na aliangukia namba tatu, aliyeshinda alikuwa Levy Mwanawasa, Sata alikuwa wa pili.

Maana yake ni kuwa Hichilema alikuwa kwenye mnyukano ambao anaujua vema. Akiwa na umri wa miaka 64 sasa, mara yake ya kwanza kuwania urais alikuwa na miaka 44. Alichomoza katikati ya vigogo wa siasa wa nchi hiyo, Rais Mwanawasa na Rais Sata. Akakabiliana mara tatu na Rais Lungu, ya tatu akamwondoa madarakani. Upande wa Mundubile, umekuwa uchaguzi wake wa kwanza.

Zambia, nchi tajiri wa madini ya shaba, imekuwa katikati ya ushindani wa China na Marekani, zinazoshindania uwekezaji wa madini hayo. Uchaguzi wake uliofanyika Agosti 13, 2026, ulikumbwa na misukosuko na machafuko. Usiku wa uchaguzi, watu 11 walikamatwa, wakiwamo viongozi wa upinzani. Ukamatamaji huo ulihusisha kurushiana risasi, Mundubile akiwa eneo la tukio.

Baada ya ghasia hizo, siku iliyofuata, Tume ya Uchaguzi Zambia (ECZ), iliahirisha kuhesabu kura, kufuatia ripoti kwamba maofisa wa uchaguzi walifanyiwa vurugu, vilevile karatasi za kupigia kura ziliibwa. Mundubile alisema, alikuwa na taarifa ya uwezekano wa matokeo kubadilishwa ili kumpa ushindi Hichilema. Upande wa Hichilema, walijibu kuwa Mundubile alikuwa akiongopa.

Mundubile pia alisema kuwa mamlaka za Zambia zilikuwa zinatumia mbinu za Tanzania, na akasema “Zambia siyo Tanzania.” Kauli hiyo, iliweza kumpambanua Mundubile kama mwanasiasa anayeweza kutamka maneno makali bila kuzingatia athari za kidiplomasia. Mathalan, angetangazwa mshindi, bila shaka angehitaji muda wa kutibu kauli yake, kabla ya kupata uhuru wa kufanya kazi na Tanzania.

Mapema kabisa, Mundubile aliahidi kuyagomea matokeo, na alisema angefungua kesi dhidi ya ECZ. Hata hivyo, mchambuzi wa siasa Zambia, Greg Musiker, wa kampuni ya ushauri wa mambo ya siasa na usalama, inayoitwa Signal Risk, akizungumza na Shirika la Habari la Reuters, alisema ni vigumu kwa kesi ya Mundubile kufanikiwa.

Kuanzia aina yake ya siasa, matamshi na matokeo, Mundubile anapita kwenye njia za Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu. Uchaguzi Mkuu Tanzania 2020, Lissu alikimbilia ubalozi wa Ujerumani nchini Tanzania kuomba hifadhi, kisha akakimbia nchi chini ya ulinzi wa ubalozi. Mundubile, alikimbilia kwenye shirika moja la Umoja wa Taifa, akiwa na aliyekuwa mgombea mwenza wake, Makebi Zulu. Taarifa zinasema tayari Mundubile na Zulu wameshatoroka Zambia

Lissu yupo mahabusu akikabiliwa na kesi ya uhaini. Mundubile anatafutwa na mamlaka za Zambia ili aunganishwe kwenye kesi ya uhaini, yeye akiwa mshitakiwa namba moja. Mundubile anatuhumiwa kuongoza genge la kijeshi, lenye silaha, lililokuwa na malengo ya kuipindua serikali. Bila shaka, asili ya kesi hiyo ni mapigano ya bunduki, baina polisi Zambia na timu ya Mundubile, usiku wa uchaguzi.

Brian Muntayalwa Mundubile ni mwanasheria, kama Lissu. Mundubile ana elimu pia ya uhasibu. Alizaliwa Januari 5, 1971, kwenye mji wa Mporokoso, Kaskazini ya Zambia. Mundubile alichomoza kisiasa kupitia chama cha Patriotic Front (PF), akagombea na kushinda ubunge jimbo la Mporokoso, mwaka 2016. Chini ya uongozi wa Rais Lungu, Mundubile alitumikia nafasi mbalimbali kwenye baraza la mawaziri, ikiwamo kuwa Mnadhimu wa Serikali.

Kuanguka kwa PF kwenye uchaguzi wa mwaka 2021, hivyo United Party for National Development (UPND) cha Hichilema kuongoza serikali, Mundubile alichaguliwa kuwa Kiongozi wa Upinzani kwenye Bunge la Zambia. Nafasi hiyo aliitumikia kuanzia mwaka 2021, ulipofika mwaka 2023, Mundibile alikoma kuwa Kiongozi wa Upinzani Bungeni kutokana na mabadiliko ndani ya PF.

Mundubile alichomoza na kukua kisiasa akiwa mfuasi wa Lungu. Juni 2025, Lungu alifariki dunia. Baada ya hapo Mundubile aliweza kuibuka kama nyota wa mchezo wa upinzani, hivyo kushawishi muungano wa vyama vya upinzani Zambia, Tonse Alliance, kumteua kuwa mgombea urais Januari 2026. Chama chake, PF, hakikubaliana na ushirikiano na Tonse, hivyo kumtenga kuelekea Uchaguzi Mkuu Zambia 2026.

Ukiacha gharama za maisha, demokrasia na haki za binadamu, Mundubile aliendesha kampeni zake akijipambanua kama mwarobaini wa umaskini wa Wazambia, kilimo, na ukosefu wa ajira. Huyo ndiye Mundubile, ambaye kwa msamiati wa wanasoka, alimlaza Hichilema na viatu, yaani alimpa mechi ngumu kwelikweli. Huyo ndiye Mundubile, Tundu Lissu wa Zambia.

Pilikapilika Stendi ya Magufuli, Latra yatoa kibali kwa shuttle

Dar es Salaam. Baada ya wamiliki wa mabasi kutii amri ya Serikali, Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (Latra) imewataka kutumia magari madogo ya shuttle kusafirisha abiria kutoka Stendi ya Magufuli iliyopo Mbezi Luis kwenda maeneo mengine, huku mabasi makubwa yakitakiwa kuanzia na kumalizia safari zake katika kituo hicho.

Hatua hiyo imekuja wakati wa utekelezaji wa agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alilolitoa Agosti 11, 2026, likiwataka wamiliki wa mabasi kurejesha shughuli za kupakia na kushusha abiria katika Stendi ya Magufuli ndani ya siku saba.

Ofisa Mfawidhi wa Latra katika Stendi ya Magufuli, Rukia Kibwana, amesema kampuni zinazohitaji kuwafikisha abiria wao katikati ya jiji au maeneo mengine zinapaswa kutumia shuttle, badala ya mabasi makubwa kuondoka na abiria kutoka stendi kwenda kwenye ofisi zao.

“Tunataka mabasi yote yapakie na kushusha abiria katika Stendi ya Magufuli. Kampuni inayohitaji kuwafikisha abiria katikati ya jiji itumie shuttle,” amesema Rukia.

Basi la kampuni ya Abood likiwa limesimama katika kituo chake kilichopo eneo la Shekilango, karibu na Ubungo Plaza, eneo hilo aghalabu hujaa mabasi mengi yakiwa yamejipanga ya kampuni hiyo, hasa nyakati za asubuhi na jioni kupakia abiria kwenda mikoa tofauti.

Amesema hakuna kampuni itakayoruhusiwa kuchukua abiria katika ofisi zake na kuwapeleka Stendi ya Magufuli kwa kutumia basi kubwa, akieleza kuwa watakaokiuka utaratibu huo watachukuliwa hatua.

Kwa mabasi yanayotumia Barabara ya Bagamoyo, amesema yanatakiwa kuanzia safari Stendi ya Magufuli na kutumia Barabara ya Goba kuelekea Tegeta.

Hatua hiyo imeanza kubadili sura ya maeneo ya Shekilango hadi Magomeni, ambayo kwa muda mrefu yalikuwa na msongamano wa mabasi yaliyokuwa yakipakia na kushusha abiria kwenda mikoa mbalimbali.

Mabasi 200 yarejea Magufuli

Rukia amesema utekelezaji wa agizo hilo umeanza kuonesha mafanikio baada ya zaidi ya mabasi 200 kurekodiwa katika mfumo wa Stendi ya Magufuli ndani ya saa 24, kutoka wastani wa mabasi 150 yaliyokuwa yakiingia na kutoka kwa siku.

Amesema mafanikio hayo yametokana na elimu iliyotolewa kwa kampuni za mabasi kwa ushirikiano na ofisi ya mkuu wa wilaya, ambapo maofisa walikwenda katika maeneo yenye ofisi nyingi za mabasi, ikiwamo Shekilango.

“Kuanzia saa tisa mchana wengi walianza kuleta magari yao na hadi sasa ni zaidi ya magari 200 tumeshayarekodi kwenye mfumo wetu,” amesema.

Mabasi yakataliwa kuondoka na abiria

Katika utekelezaji wa agizo hilo, Mwananchi ilishuhudia baadhi ya mabasi yaliyotaka kuondoka na abiria Stendi ya Magufuli kwenda kwenye ofisi zao mjini na maeneo mengine yakizuiwa na kuamriwa kuwashusha.

Basi moja lililotoka nje ya nchi lilionekana likisimamishwa katika geti la kutokea Stendi ya Magufuli, huku askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wakikagua mabasi yaliyokuwa yakitoka mikoani kuhakikisha hayaondoki na abiria nje ya utaratibu.

Mkurugenzi wa Habari kwa Umma wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa), Mustapha Mwalongo, amesema kampuni wanachama zimetekeleza uamuzi huo, huku wakiendelea kutafuta nafasi ya kukutana na mkuu wa mkoa kwa ajili ya kuzungumzia changamoto zilizojitokeza.

“Tangu Agosti 13 hadi sasa tunafanya jitihada za kumtafuta mkuu wa mkoa ili tuzungumze naye. Barua tulishatuma. Naamini tukishafanya mazungumzo naye tutatoa msimamo wetu,” amesema Mwalongo.

Meneja Stendi ya Magufuli

Kaimu Meneja wa Stendi ya Mabasi cha Magufuli, Naamini Leonard, amesema stendi hiyo imepangwa kuhudumia mabasi takribani 500 kwa siku.

Hata hivyo, amesema baada ya baadhi ya kampuni kuanzisha vituo vyao nje ya stendi hiyo, idadi ya mabasi yaliyokuwa yakiingia na kutoka kituoni ilishuka hadi kufikia takribani mabasi 150 kwa siku.

Leonard amesema stendi hiyo ina uwezo wa kuegesha na kuhudumia mabasi 200 kwa wakati mmoja katika eneo lake la ndani.

Hata hivyo, uwezo huo hauzuii kuhudumia mabasi 500 kwa siku kwa kuwa huduma zinaendeshwa kwa saa 24, na kila basi hupewa muda wa takribani saa mbili kupakia abiria na kuondoka, hivyo kuwezesha mabasi mengine kuingia na kutumia nafasi hiyo.

Leonard amesema uongozi wa stendi umejipanga kuboresha huduma za kijamii, ikiwamo vyoo, maeneo ya kukaa abiria na udhibiti wa wapiga debe, huku huduma za usafiri zikitarajiwa kuendelea kwa saa 24.

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando, amesema kila anayejihusisha na biashara ya usafirishaji katika wilaya hiyo atalazimika kuanza safari katika Stendi ya Magufuli.

Amesema basi litakalokiuka utaratibu huo halitaruhusiwa kutumia Barabara ya Shekilango kuelekea Mwenge wala Barabara ya Mlimani City kuelekea Mwenge.

“Njia pekee utakayoweza kutumia ni Barabara ya Goba kama unaelekea Bagamoyo, au njia ya Chalinze kama unaelekea Kibaha,” amesema.

Msando amesema utekelezaji huo si kuwaonea wafanyabiashara, bali ni kuhakikisha shughuli za usafirishaji zinafanyika kwa utaratibu, usalama na uwajibikaji.

Amesema Serikali imejipanga kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa licha ya baadhi ya watu kujaribu kulizuia.

Mizigo yawekewa utaratibu

Kuhusu usafirishaji wa mizigo, Msando amesema Serikali haijazuia huduma hiyo, bali imeweka utaratibu ambao wasafirishaji wanapaswa kuufuata.

Amesema kumekuwa na mizigo inayosafirishwa bila kufuata utaratibu, hali ambayo baadhi ya kampuni zimekuwa zikitumia kama mwanya wa kupakia abiria baadaye.

“Hatuzuii usafirishaji wa mizigo, tunachosisitiza ni kufuata utaratibu mzuri,” amesema.

Amesema Serikali haiwezi kuruhusu kampuni kutumia kisingizio cha kusafirisha mizigo, wakati huo huo zikikusanya abiria katika maeneo yasiyoruhusiwa.

Abiria walalamikia gharama

Pamoja na Serikali kusisitiza kuwa utaratibu huo unalenga kuboresha huduma, baadhi ya abiria wameeleza kuwa unawaongezea gharama za usafiri kutoka Stendi ya Magufuli hadi kufika maeneo wanakokwenda.

Yudas Joachim, mkazi wa Manzese, amesema awali mabasi aliyokuwa akitumia kutoka Morogoro yalikuwa yakimfikisha karibu na nyumbani, lakini sasa atalazimika kutumia takribani Sh5,000 zaidi kwa usafiri na mizigo kutoka stendi hadi nyumbani.

Ameiomba Serikali kuangalia namna ya kupunguza gharama hizo ili utaratibu huo usiwe mzigo kwa wananchi.

Mariam Ngoma, mkazi wa Mbagala, amesema hana tatizo na mabasi kuanzia na kumalizia safari Stendi ya Magufuli, lakini ameshauri Serikali kuangalia gharama za usafiri wa umma.

Pia, ameiomba Serikali kuboresha barabara zinazotumiwa na wasafiri kuelekea Mbagala kutokana na foleni zinazoweza kuongeza muda wa safari.

Kicheko kwa wafanyabiashara

Kwa upande wa wafanyabiashara katika Stendi ya Magufuli, kurejea kwa mabasi kumewapa matumaini baada ya biashara zao kudorora kutokana na magari mengi kupakia abiria nje ya kituo hicho.

Said Rajabu, amesema awali mabasi yalipokuwa yakipakia abiria katika ofisi zao mjini, yalipofika stendi yalikuwa yakichukua abiria wachache, wakati mwingine wasiozidi watano.

Amesema hali hiyo iliathiri biashara, lakini kurejea kwa mabasi kumeanza kuleta ahueni.

Aisha Bakari, mjasiriamali katika stendi hiyo, amesema awali alikuwa akipata takribani Sh30,000 kwa siku licha ya kuamka saa 10 usiku.

Amesema baada ya mabasi kuanza kurejea, mapato yake yameongezeka na kufikia Sh60,000 kwa siku na anaamini yataongezeka kadiri siku zinavyoendelea.

Shekilango yapata sura mpya

Katika ziara ya Mwananchi eneo la Shekilango leo, Agosti 18, 2026, ilishuhudiwa mabadiliko ya mandhari baada ya mabasi kuanza kuondoka katika maeneo yaliyokuwa yakitumika kama vituo vya kupakia na kushusha abiria.

Msongamano wa mabasi umepungua, lakini shughuli za ukataji tiketi na upokeaji wa mizigo bado zinaendelea katika ofisi za kampuni hizo.

Ofisi za mabasi yakiwamo Katarama, BM, Happy Nation na Abood zinaendelea na ukatishaji tiketi, huku mawakala wakiendelea kutafuta abiria.

Mizigo ya wasafiri pia imeonekana ikiwa imepangwa nje ya baadhi ya ofisi hizo na kuandikwa majina ya wahusika.

Serikali yatoa siku nane kwa wazalishaji saruji kushusha bei

Dar es Salaam. Serikali imewapa wazalishaji wa saruji siku nane kuhakikisha wanapunguza bei na kuongeza upatikanaji wa bidhaa hiyo, baada ya uhaba wa wiki kadhaa kusababisha mfuko wa kilo 50 kufikia Sh26,000 katika baadhi ya maduka ya rejareja.

Agizo hilo limetolewa leo Jumanne, Agosti 18, 2026  baada ya Wizara ya Viwanda na Biashara kuwaita wazalishaji wa saruji kwenye kikao cha dharura kujadili kupanda kwa bei na changamoto ya upatikanaji wa bidhaa hiyo.

Katibu mkuu wa wizara hiyo, Rajabu Salum amesema wazalishaji wamepewa hadi Agosti 28, 2026 kutekeleza hatua za kuongeza upatikanaji wa saruji na kushusha bei.

“Tumekutana na wazalishaji wa saruji Agosti 18 na kuwapa siku nane kuhakikisha bei zinashuka na upatikanaji wa bidhaa unaimarika. Baada ya Agosti 28 tutawaita tena kwa ajili ya kikao kingine na kutathmini hali,” amesema.

Salum amesema Serikali itaendelea kufuatilia bei na upatikanaji wa saruji katika kipindi hicho kabla ya kuamua iwapo hatua zaidi zitahitajika.

Kwa mujibu wa wazalishaji, uhaba huo umechangiwa kwa kiasi na kuharibika kwa mitambo katika viwanda vikubwa vinavyozalisha klinka, malighafi muhimu katika utengenezaji wa saruji.

Gharama za mafuta na usafirishaji pia zimeongeza gharama za uzalishaji na usambazaji.

Salum ametaja Kiwanda cha Maweni, Tanga na Dangote kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa klinka nchini, akisema hitilafu za mitambo katika viwanda hivyo zimeathiri uzalishaji.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum (kulia ) akizungumza na wamiliki wa viwanda vya saruji nchini akiwa pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango wa wizara hiyo, Needpeace Wambuya kikao hicho kimefanyika jijini Dodoma.

Amesema licha ya kuwepo kwa viwanda vingine vinavyozalisha klinka, matatizo katika wazalishaji hao wawili yanaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa saruji katika soko.

Hatua hiyo ya Serikali imekuja wakati bei ya saruji ikizidi kuwa na athari kwa sekta ya ujenzi, ambayo inategemea bidhaa hiyo katika ujenzi wa nyumba, majengo ya biashara na miundombinu.

Utafiti wa hivi karibuni wa bei katika viwanda unaonesha tani moja ya saruji inauzwa kwa wastani wa Sh321,251 kabla ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), kutoka takriban Sh300,000 Juni.

Kwa kuwa tani moja ni sawa na mifuko 20 ya kilo 50, bei hiyo ya kiwandani ni takriban Sh16,063 kwa mfuko kabla ya VAT au Sh18,954 baada ya kujumuisha VAT.

Hata hivyo, uchunguzi umebaini baadhi ya wauzaji wa rejareja wanauza mfuko huo hadi Sh26,000, hali iliyozua wasiwasi kuhusu tofauti kubwa kati ya bei ya kiwandani na ile ya rejareja.

Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC), Dk Matiko Mturi, amesema gharama za usafirishaji, mahitaji makubwa na uhaba katika baadhi ya maeneo ni miongoni mwa sababu zinazochangia kupanda kwa bei.

Amesema bei ya wastani ya tani moja ya saruji Dar es Salaam imeongezeka kwa takriban Sh21,000 tangu Juni.

Dk Mturi amesema bei ya kiwandani pekee haiwezi kueleza kiasi anacholipa mtumiaji kwa sababu gharama za usafirishaji na usambazaji huongezwa katika mnyororo wa biashara.

Ametoa mfano kuwa mfuko unaweza kutoka kiwandani kwa takriban Sh18,900 ukiwa na VAT, kabla mawakala na wauzaji kuongeza gharama za usafirishaji na usambazaji.

“Wakala akiusafirisha mfuko wa saruji kutoka kiwandani hadi dukani kwake, anaweza kuongeza Sh1,000 au Sh1,500. Bei inaweza kufikia Sh20,000 hadi Sh21,000,” amesema.

Amesema wanunuzi wanaonunua kwa kiasi kidogo na kusafirisha saruji kwenda maeneo yaliyo mbali na vituo vikuu vya usambazaji, wanaweza kuongeza gharama nyingine za Sh2,000 hadi Sh3,000 kwa mfuko.

Dk Mturi amesema shughuli nyingi za ujenzi nchini pia zimeongeza mahitaji ya saruji.

“Karibu kila unakokwenda kuna ujenzi unaendelea. Pia, kuna barabara nyingi zinazojengwa, baadhi zikitumia zege. Kwa hiyo mahitaji ni makubwa sana,” amesema.

Ameongeza kuwa gharama za usafirishaji zimepanda kwa kiasi kikubwa, huku baadhi ya wasafirishaji wakiongeza viwango vyao kwa kiwango kikubwa kuliko ongezeko la bei ya mafuta.

Julai 8,  mwaka huu, gazeti la Mwananchi liliandika kuhusu kupanda kwa bei ya saruji, baada ya wazalishaji wakubwa kutangaza marekebisho ya bei yaliyofanya mfuko mmoja wa saruji kufikia kati ya Sh17,000 na Sh18,150, kutegemea aina ya saruji, eneo la mauzo na gharama za usambazaji.

Ongezeko hilo lilitokana na wazalishaji kuongeza bei kwa kati ya Sh500 na Sh650 kwa mfuko kabla ya VAT, wakitaja kupanda kwa gharama za uzalishaji, malighafi, usafirishaji, kodi na uendeshaji. Hatua hiyo ilitarajiwa kuongeza gharama za ujenzi kwa wananchi, makandarasi na waendelezaji wa miradi mbalimbali.

Kampuni ya Saruji ya Dangote ilitangaza kuongeza bei kwa Sh650 kwa mfuko wa kilo 50 bila VAT kwa aina zote za saruji zinazozalishwa na kampuni hiyo, ikiwamo 32.5R, 32.5N, 42.5N, 42.5R na 52.5N.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, marekebisho hayo yalitokana na ongezeko la majukumu ya kifedha, gharama za kisheria, ununuzi wa malighafi na gharama za jumla za uendeshaji.

Nayo Moshi Cement, inayomilikiwa na Jun Yu Investment International Company Limited, ilitangaza kuongeza bei kwa Sh500 kwa mfuko mmoja, ikitaja kupanda kwa gharama za malighafi na usafirishaji.

Baadhi ya wazalishaji walitangaza mabadiliko ya bei kwa kuzingatia tani badala ya mifuko.

Maweni Limestone Limited (Huaxin) iliongeza bei kwa Sh13,000 kwa tani bila VAT kwa saruji inayozalishwa katika viwanda vyake vya Tanga na Mkuranga, ikieleza kuwa hatua hiyo imesababishwa na ongezeko la gharama za uzalishaji na matengenezo ya mitambo.

Tanga Cement PLC (Simba Cement) nayo ilitangaza ongezeko la Sh13, 000 kwa tani, ikitaja kupanda kwa gharama za kodi, pembejeo na uendeshaji wa biashara.

Lake Cement Limited, wazalishaji wa Saruji ya Nyati, pia ilitangaza ongezeko la Sh13, 000 kwa tani kutokana na kupanda kwa gharama za uendeshaji na usafirishaji.

Wamiliki wa viwanda vya saruji nchini wakiwa katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum hayupo pichani.

Mbeya Cement Company Limited ilifanya marekebisho kulingana na aina ya bidhaa, ambapo Fastaplus 32.5 imeongezeka kwa Sh9, 085 kwa tani, huku Tembo Supaset 42.5 na Tembo Powerplus 42.5N ikiongezeka kwa Sh14,136 kwa tani.

Mabadiliko hayo ya bei yamekuja wakati Serikali ikianza kutekeleza marekebisho ya viwango maalumu vya ushuru wa bidhaa katika mwaka wa fedha 2026/27.

Serikali ilivyoingilia kati

Awali, wataalamu wa uchumi na ujenzi walionya kuwa, iwapo hali ya kupanda kwa bei za vifaa vya ujenzi itaendelea, athari zake hazitaishia kwa wanaojenga pekee, bali zitawaathiri pia wapangaji, wafanyabiashara na ajira zinazotegemea sekta ya ujenzi.

Agosti 11, mwaka huu, Balozi Salum, akizungumza na Gazeti Dada la The Citizen kuhusu kadhia hiyo alisema Serikali itakutana na wazalishaji wa saruji Jumanne ya Agosti 18 (jana), ili kubaini sababu za kupanda kwa bei hiyo na kutafuta hatua za kuidhibiti.

“Jumanne, Agosti 18, tutakutana na wazalishaji kujadili changamoto zilizopo na kubaini kinachoendelea. Wanasema kuna uhaba wa klinka (malighafi ya kutengeneza saruji), hivyo tunahitaji kuwasikiliza moja kwa moja,” alisema.

Balozi Salum Serikali ina wasiwasi kuhusu ongezeko kubwa la bei katika maduka ya rejareja na inataka wazalishaji waeleze sababu zinazoendesha mabadiliko hayo.

Alisema Serikali pia itashirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) endapo itahitajika, ili kubaini iwapo kuna masuala yanayohitaji hatua za udhibiti.

“Endapo tatizo ni uhaba wa klinka, tunahitaji kulielewa ili nasi tuweze kuwaandaa wananchi. Haiwezekani maduka yote ya rejareja kwa ghafla yakaongeza bei hadi kiwango hiki. Hii ina maana kuna tatizo kubwa zaidi linalohitaji kuchunguzwa,” alisema.

Balozi Salum, alisema timu ya Serikali tayari iko katika maeneo mbalimbali kuchunguza sababu za kupanda kwa bei hiyo.

Mchengerwa ataja vipaumbele sita kupunguza vifo vya mama, mtoto

Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa ametaja mambo sita yanayopaswa kupewa kipaumbele na nchi za Afrika Mashariki na Kusini, ili kupunguza vifo vya mama na mtoto, kukabiliana na milipuko ya magonjwa na kuimarisha mifumo ya afya.

Mchengerwa amesema hayo leo Jumanne, Agosti 18, 2026, katika Mkutano wa Nne wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Afya wa Mashariki na Kusini mwa Afrika, unaojadili usalama wa afya, kujitegemea katika sekta hiyo na kuongeza uwekezaji katika afya ya msingi, mama na mtoto.

Mkutano huo umewakutanisha mawaziri na wawakilishi kutoka nchi 14 za eneo hilo.

Amesema kipaumbele cha kwanza ni kuipa afya ya msingi, usalama wa afya na afya ya mama na mtoto katika mipango ya maendeleo na bajeti za kitaifa.

Amesema Tanzania inalenga kuendelea kupunguza vifo vya mama kuelekea lengo la kimataifa la vifo 70 kwa kila vizazi hai 100,000, akisisitiza kuwa, mafanikio hayo hayawezi kupatikana bila uwekezaji wa kutosha.

Waziri wa Afya Zanzibar, Saada Mkuya akizungumza wakati wa mkutano wa nne wa Kamati ya Mawaziri wanaohusika na Afya wa Mashariki na Kusini mwa Afrika, unaojadili namna ya kuimarisha usalama wa afya na kuongeza uwekezaji katika afya ya msingi, mama na mtoto.

“Ni muhimu kuimarisha bajeti zetu na si kuziimarisha katika tarakimu pekee, bali kuhakikisha wakati wote tunapotoka hapa kwenye mabaraza yetu ya mawaziri katika kila nchi tunazungumzia umuhimu wa kuwekeza kwenye sekta ya afya,” amesema.

Kipaumbele cha pili, amesema ni kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji, maandalizi na mwitikio wa magonjwa katika mipaka ya nchi, badala ya kusubiri mlipuko utokee.

“Ugonjwa hautambui masuala ya boda, hautambui mipaka, hautambui kama hapa ni Tanzania, Kenya au Uganda,” amesema Mchengerwa.

Ametolea mfano mlipuko wa Ebola Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), akisema hali hiyo inaonesha umuhimu wa ushirikiano wa nchi jirani.

AmesemaTanzania hushirikiana na Uganda na DRC kwa kutoa wataalamu, dawa na rasilimali nyingine wakati wa milipuko, huku ufuatiliaji ukiendelea katika vituo vya mipakani.

Kipaumbele cha tatu amesema ni kutekeleza mpango wa afya ya mama, mtoto mchanga na mtoto kwa kuweka malengo yanayopimika, muda wa utekelezaji na mifumo ya uwajibikaji.

Mchengerwa amesema kipaumbele cha nne ni kutafuta fedha za ndani zinazotabirika na bunifu, pamoja na kuimarisha ununuzi wa pamoja na uzalishaji wa dawa, vifaa tiba na bidhaa nyingine za afya barani Afrika.

Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akiteta jambo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk Grace Magembe

Mchengerwa ametaja pia uwajibikaji kuwa kipaumbele cha tano, akitaka ahadi zifuatiliwe, matokeo yapimwe na nchi zibadilishane uzoefu.

Kipaumbele cha sita amesema ni kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika kukabiliana na milipuko na changamoto nyingine za afya.

Waziri wa Afya Zanzibar, Saada Mkuya amesema afya ya mama na mtoto ni miongoni mwa ajenda kuu, huku nchi zikihimizwa kubadilishana uzoefu kuhusu mifumo ya afya, rasilimali watu na miundombinu.

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Africa CDC, Dk Raji Tajdin amesema Afrika inazalisha takriban asilimia moja pekee ya mahitaji yake ya chanjo, akisisitiza umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa ndani.

Dk Tajdin amesema Afrika inakabiliwa na zaidi ya magonjwa 200 yanayoibuka na kuibuka tena, huku mabadiliko ya tabianchi yakiongeza hatari mpya za kiafya.

“Hatupaswi kusubiri mlipuko ndipo tuanze kukimbizana. Tunahitaji maandalizi,” amesema Dk Tajdin.

Babu adai kupigwa ngwara na mwalimu Bahi

Bahi. Mvutano kati ya mzee mwenye umri wa miaka 86, anayemtuhumu Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mpamantwa kwa madai ya kumpiga ngwara, umeingia sura mpya baada ya Serikali ya Kijiji kueleza ilivyopokea na kushughulikia malalamiko hayo.

Tukio hilo linamhusisha mzee Joseph Ndega, maarufu Shamba, anayedai mwalimu mkuu wa shule hiyo, Ramadhan Kipenya, kumpiga ngwara Agosti 4, 2026, baada ya kufika shuleni hapo kuulizia adhabu walizopewa wajukuu zake pamoja na wanafunzi wengine.

Kwa mujibu wa Shamba, aliamua kwenda shuleni baada ya wajukuu zake kurudi nyumbani wakilalamika kupigwa viboko vingi.

Amesema alipofika na kumsogelea mwalimu mkuu, alikasirika na kumshambulia.

“Watoto walirudi wanalia, wakasema wamepigwa sana, nikaamua kwenda kuwasikiliza na kujua chanzo. Lakini, aliponiona akapatwa na hasira. Baada ya kumsogelea akanipiga ngwara, tukaanguka wote, ndipo akanipiga makofi mawili,” amesema.

Shamba anasema hakufikisha malalamiko yake kwa viongozi wa ngazi za juu kwa sababu alielekezwa kuwa suala hilo lilipaswa kumalizwa katika ngazi ya kijiji.

Ameongeza kuwa anaamini tabia ya kupiga wanafunzi imekuwa ikijitokeza shuleni hapo, na ndiyo iliyomsukuma kufuatilia suala hilo baada ya wajukuu wake kupewa adhabu.

Akijibu tuhuma hizo, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mpamantwa, Ally Kipenya, amekana kumpiga Mzee Shamba.

“Kwa sasa niko benki, kwa hiyo siwezi kulisema sana jambo hili, ila kifupi halipo na sijawahi kufanya hivyo. Labda watu wangesikia huko, nikitoka nitakutafuta,” amesema.

Hata hivyo, baada ya mazungumzo hayo, Kipenya hakupatikana tena kwa simu.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mpamantwa, John Makolokolo, amekiri kuwepo kwa mvutano huo, lakini amekanusha madai kuwa mwalimu mkuu alimpiga mzee Shamba.

Amesema baada ya mzee Shamba kufika kijijini kulalamikia adhabu za wajukuu wake, Serikali ya Kijiji ilimuita mwalimu mkuu kwa mahojiano.

“Mwalimu mkuu alituambia siku hiyo alimkuta mzee Shamba anavutana na mwalimu wa zamu, ndipo akamshika mkono na kumtoa eneo hilo ili kuzuia mvutano. Hapo ndipo hali ilipotulia,” amesema Makolokolo.

Kuhusu madai ya wanafunzi kuchapwa viboko vingi, Makolokolo amesema si kweli kuwa walimu wana utaratibu huo, akisema adhabu zinazotolewa ni za kawaida.

Amesema siku hiyo wajukuu wa Shamba waliitwa na Serikali ya Kijiji ilimtuma mtendaji pamoja na ofisa maendeleo wa kijiji, ambao waliwakagua na kutoa taarifa kuwa hawakuona alama zilizoashiria walipigwa viboko kupita kiasi.

Makolokolo amesema Shamba amekuwa akihusika katika migogoro kadhaa katika maeneo tofauti, hasa anaposikia wajukuu wake wamepewa adhabu.

Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi

Arusha. “Mali ya baba inanitoa roho, bora nikae pembeni, niinusuru roho yangu mimi…” Hicho ndicho kibwagizo cha wimbo ‘Kilio cha Mtu Mzima’ wa OTTTU Jazz Band kilichotumiwa na Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Mbulu, Mosses Ntumengwa, kuanza uamuzi wa mgogoro wa ardhi uliowakutanisha ndugu wawili waliokuwa wakigombea shamba waliloachiwa na baba yao.

Kwa kutumia ujumbe wa wimbo huo unaogusia migogoro na maumivu yanayoweza kujitokeza katika kugawana au kugombea mali ya wazazi, Ntumengwa alionyesha namna mali ya familia inavyoweza kugeuka chanzo cha uhasama na kuvunja undugu.

Katika shauri hilo, Baraza limemtangaza Tlaka’ari Bura kuwa mmiliki halali wa ekari 11 za ardhi zilizopo Kitongoji cha Labom, Kijiji cha Mighaw, Kata ya Endahagichan, huku ndugu yake, Matle Bura, akitangazwa kuwa mvamizi wa eneo hilo.

Mwenyekiti Ntumengwa amefananisha mgogoro huo na maudhui ya wimbo huo na kueleza kuwa  ujumbe wake unafundisha kuwa mali au ardhi zilizoachwa na wazazi baada ya kufariki dunia kamwe zisifikishe mahali ndugu kupoteza utu, undugu, upendo na hata kugharimu maisha kwa sababu ya ugomvi, chuki na mifarakano kutokana na mali hizo.

Mwenyekiti huyo ameeleza kuwa wadaawa katika shauri hilo ambao ni ndugu wa damu, Baraza liliwapa nafasi ya kumaliza mgogoro huo kwa njia ya suluhu ili amani na upendo vidumu kati yao, lakini juhudi hizo hazikufanikiwa.

Mwenyekiti huyo amesema kutokana na sababu hiyo Baraza halina namna nyingine bali kuwaamua wadaawa kwa mujibu wa sheria, ili baada ya hukumu wachukue kapu na kuvuna wenyewe kila walichokipanda katika ushahidi wao.

“Kwani Baraza halina mikono, jembe na shamba la kulima pale ndugu wanapogombana ili mwishoni lichukue kapu na kuvuna. Na hii ni kulingana na methali ya Waswahili isemayo “ndugu wakigombana shika jembe ukalime, wakipatana chukua kapu ukavune,”ameeleza Mwenyekiti huyo.

Katika maombi hayo ya ardhi namba 7/2026,Tlaka’ari alidai mbele ya Baraza kuwa baba yao, Bura Gitiye alimpa eneo hilo Septemba 20,1991 na alilitumia kwa kilimo cha mahindi, maharage na alizeti toka mwaka  1991 hadi 2026, (miaka 35).

Amedai mgogoro ulianza mwaka 2024 baada ya ndugu yake kuvamia eneo hilo kwa kulima na trekta na kuwa mgogoro huo ulipelekwa kwenye ofisi za Kijiji cha Mighaw kwa ajili ya suluhu, lakini ilishindikana na ukaibuka tena mwaka 2025 .

Amedai mwaka jana mdaiwa alifyeka vichaka na kutengeneza boma huku akidai kuwa eneo hilo alipewa na wazee jambo ambalo sio la kweli, na kuwa mgogoro huo uliwahi kupelekwa kwenye Baraza la Kata ya Endahagichan kwa ajili ya suluhu lakini ilishindikana.

Mdai aliliomba Baraza kuwa atamkwe yeye ndiye mmiliki halali wa eneo hilo, Baraza litoe zuio la kudumu na amri stahiki kwa mdaiwa, wafanyakazi wake wote na wale wote wanaofanya kazi chini yake kutoingilia tena eneo la mgogoro.

Kwa upande wake mdaiwa, aliwasilisha utetezi wake mbele ya Baraza hilo huku akiomba maombi haya yatupiliwe mbali, na eneo la mgogoro litamkwe kuwa ni   la kurithi na wadaawa katika shauri na kuwa mdaiwa afidiwe gharama zake alizozitumia.

Mashahidi wa Tlaka’ari walieleza Baraza kuwa walishuhudia baba yao akimpatika Tlaka’ari eneo hilo na amekuwa akilitumia kwa muda mrefu bila mgogoro.

Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote, Mwenyekiti  amesema  Tlaka’ari amethibitisha  madai yake ya umiliki wa eneo  hilo kuwa alilipata baada ya kupewa na baba yake mzazi.

Baraza lilisema ushahidi huo uliungwa mkono na ndugu zake, Askwari Bura na Charles Bura, waliodai kushuhudia baba yao akimpa Tlaka’ari eneo hilo, pamoja na Kwaslema Matle aliyethibitisha kuwa Tlaka’ari alikuwa akilitumia eneo hilo kwa muda mrefu.

Kuhusu Matle, Baraza lilisema ushahidi wake haukuwa na nguvu, huku mashahidi wake wakitoa maelezo yaliyokinzana kuhusu chanzo cha umiliki.

“Baada ya kuona na maoni ya wazee wa baraza ambao wameona maombi hayo ya mdai yakubaliwe na mdai atamkwe kuwa mmiliki halali na mdaiwa atamkwe kuwa mvamizi na abakie eneo alilokuwa akilitumia.”

 “Baraza hili linatoa amri zifuatazo, maombi ya mdai yana mashiko na yanakubaliwa, mdai anatamkwa kuwa ndiye mmiliki halali wa eneo la mgogoro. Mdaiwa anatamkwa kuwa ni mvamizi kwenye eneo la mgogoro mali ya mdai na kwa kuwa wadaawa nia ndugu moja, kila upande utabeba gharama zake,”amesema Mwenyekiti.

Mwili wa mtoto wa miaka saba wakutwa shimoni Tabora

Tabora. Mtoto Yusra Juma (7), mkazi wa Mtakuja, Kata ya Malolo, Manispaa ya Tabora, amekutwa amefariki dunia ndani ya shimo la kuchimbwa mchanga, huku Jeshi la Polisi likisema uchunguzi wa awali umebaini alinyongwa na watu ambao hawajafahamika.

Akizungumza kuhusu tukio hilo leo, Jumanne Agosti 18, 2026, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Twaha Lulengelule amesema: “Tukio hili limetokea jana majira ya saa nane mchana baada ya kutoka shuleni, tunaendelea na uchunguzi ili kuwabaini waliofanya kitendo hiki.”

Amesema mtoto huyo alikuwa mwanafunzi wa darasa la pili katika Shule ya Msingi Mawiti iliyopo Malolo Manispaa ya Tabora.

Kamanda Lulengelule amesema kifo cha mtoto huyo kilibainika baada ya bibi yake kuona muda umeenda bila kurejea nyumbani ndipo akatoka kufuatilia na hatimaye kuukuta mwili wake kwenye shimo.

Wananchi katika kata ya Malolo wakiwa eneo la tukio alipouawa mtoto Yusra.

“Ufuatiliaji wa bibi yake ndio uliosababisha kuupata mwili wa mtoto huyo mapema, uchunguzi wa madaktari unaeleza kuwa, mtoto huyo amefariki kwa kukosa hewa baada ya kushikwa shingo,” amesema.

Diwani wa Malolo, Manispaa ya Tabora, Naomi Kasanga amelaani tukio hilo akisema ni la kinyama na halikubaliki katika jamii.

Ameliomba Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini waliohusika na tukio hilo na kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria.

“Mtoto huyu ametuumiza sana, kwanza mdogo halafu sasa hana hatia kabisa, kwa nini mtu amuue kinyama hivi,” amesema Kasanga.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mtakuja, Hamisi Ibrahim amelaani tukio hilo akisema ni la kinyama na halivumiliki katika jamii.

Amesema mauaji hayo ni miongoni mwa matukio mabaya yanayohitaji hatua za haraka za kisheria.

“Hatupaswi kuwa na mazingira ya kuogofya kiasi hiki, lazima amani iwepo, watoto hawa ni hazina yetu lazima waishi kwa amani, kifupi tumeumizwa sana,” amesema.

Beatrice Katatula, mkazi wa Malolo amesema tukio la Yusra sio la kwanza kwa Kata ya Malolo kwa sababu miezi kadhaa nyuma alipoteza maisha mtoto mwingine katika mazingira ya kinyama.

“Mpaka tunaogopa sasa jamani maana hatuwezi kwenda na watoto kazini, na ni lazima pia waende shule, sasa kama shule njiani tena usalama hakuna, hii inatuumiza na kutuvuruga kwa kweli,” amesema.

WRRB, MIKOA NA HALMASHAURI KUIMARISHA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA

 

Na Matukio Daima Media DODOMA

BODI ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imesema itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri nchini ili kuimarisha utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRS), kuongeza tija kwa wakulima na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, ameyasema hayo leo Agosti 18, 2026, wakati akizungumza na Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Bw. Bangu amesema utekelezaji wenye tija wa mfumo huo katika mikoa na halmashauri unahitaji ushiriki wa karibu wa Maafisa Biashara, hususan katika usimamizi wa shughuli zinazohusiana na maghala pamoja na minada ya mazao inayofanyika katika maeneo yao.

Amesema Maafisa Biashara wana nafasi muhimu katika kuhakikisha taarifa sahihi kuhusu mahitaji ya maghala katika maeneo yao zinapatikana, sambamba na kufuatilia hali, matumizi na uhitaji wa maghala katika halmashauri na mikoa ili kuwezesha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutekelezwa kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano wa WRRB, Bw. Dionis Musseru, amesema utoaji wa elimu kwa umma umeendelea kuongeza uelewa na ushiriki wa wadau katika mfumo huo, ambapo hadi sasa mazao 11 yanauzwa kupitia WRS.

Tatoa yatishia kupaki malori | Mwananchi

Dar es Salaam. Wakati Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam akianzisha operesheni ya kukamata malori yanayoegeshwa kwenye  hifadhi za barabara, Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa) kimetishia kusitisha shughuli za usafirishaji endapo Serikali  haitashughulikia changamoto zinazowakabili.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Tatoa, Elias Lukumay, alipokuwa akizungumzia agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, la kuanzisha operesheni dhidi ya malori yanayoegeshwa kwenye hifadhi za barabara.

Agosti 11, 2026, Chalamila aliliagiza Jeshi la Polisi kupitia Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa, kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), kuajiri vijana watakaosaidia katika operesheni ya kuwakamata madereva wa malori wanaokiuka utaratibu kwa kuegesha katika maeneo yaliyotengwa kwa matumizi mengine.
Chalamila alisema hatua hiyo inalenga kukabiliana na uholela katika Jiji la Dar es Salaam na kuhakikisha maeneo ya barabara yanatumika kwa mujibu wa utaratibu. Alisema agizo hilo pia linawahusu wamiliki wa mabasi.
Hata hivyo, Tatoa imeeleza operesheni za kukamata malori si suluhisho la kudumu, ikitaka Serikali ikae pamoja na wadau wa sekta hiyo ili kujadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili.

Akizungumza  jijini Dar es Salaam leo Agosti 18, 2026, Lukumay amesema wamiliki wa malori wanakabiliwa na kero mbalimbali, zikiwemo kukamatwa kwa magari, madereva kuvamiwa na kupokonywa namba za magari na malalamiko kuhusu mizani ya Iringa na Mikumi.

Amesema wamiliki wa malori hawapingi usimamizi wa Serikali, bali wanataka utekelezaji wa sheria uende sambamba na mazungumzo yatakayosaidia kutatua changamoto zinazojitokeza katika shughuli zao.

“Mnatupitisha kwenye njia ngumu kila kukicha, kero ni zilezile. Naamini katika njia ya maelewano kama itashindikana, hapo tuko tayari kuyapaki haya malori mpaka hapo tutakapokubaliana,” amesema Lukumay.

Amesema kusitisha shughuli za malori kunaweza kuathiri sekta nyingine zinazotegemea usafirishaji wa bidhaa, hususan Bandari ya Dar es Salaam, biashara ya mafuta na shughuli za wafanyabiashara wanaosafirisha bidhaa ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Lukumay, sekta ya usafirishaji pia ni chanzo cha ajira kwa madereva, wapakuaji na makundi mengine yanayohusika katika mnyororo wa usafirishaji.

Amesema Serikali na wamiliki wa malori wanapaswa kujenga utaratibu wa mazungumzo ya kudumu ili kuepusha migogoro na kuhakikisha shughuli za usafirishaji zinaendelea bila kuathiri uwekezaji na maeneo mengine ya  kiuchumi.

Lukumay amezitaka mamlaka husika kupunguza utegemezi wa operesheni za kukamata malori na badala yake kuweka mfumo wa ushirikiano unaozingatia sheria, usalama wa barabara na masilahi ya sekta ya usafirishaji.

Akisimulia changamoto wanazokutana nazo hadi kulazimika kuegesha malori katika hifadhi za barabara, mmoja wa madereva, Elias Mwaningo, amesema tatizo kubwa ni ukosefu wa maeneo maalumu ya kuegesha.

Mwaningo alitoa kauli hiyo mbele ya Chalamila wakati mkuu huyo wa mkoa alipofanya ziara katika maeneo ya Kurasini na kushuhudia malori yakiwa yameegeshwa kwenye hifadhi ya barabara.

“Changamoto ni nyingi. Tunaleta mizigo mingi, lakini kasi ya kuipokea kwenye ICD ni ndogo, kiasi kwamba msongamano wa malori unakuwa mkubwa na tunakosa hata sehemu ya kwenda kujisaidia haja ndogo,” amesema.

Kwa mujibu wa Mwaningo, madereva pia wanakabiliwa na changamoto katika maeneo wanapopeleka mizigo, ikiwemo vitendo vya rushwa na ucheleweshaji wa upakuaji.

Amesema wakati mwingine gari linaweza kukaa hadi wiki bila kuruhusiwa kushusha mzigo, huku magari yaliyowasili baadaye yakipewa kipaumbele cha kushusha mizigo.

 “Kuna wakati gari inamaliza hadi wiki hairuhusiwi kwenda kushusha mzigo, badala yake anachukuliwa aliyefika leo kwenda kushusha bila kujali kuna wengine waliojipanga kwenye mstari,” amesema.