Blog

  • NBC kuchochea nguvu ya uchumi Zanzibar

    NBC kuchochea nguvu ya uchumi Zanzibar

    Zanzibar. Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imesema itaendelea kuwa mshirika wa kimkakati katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar kwa kuwawezesha wafanyabiashara, wawekezaji na wajasiriamali kutumia fursa zinazotokana na uwekezaji, maendeleo ya miundombinu na ukuaji wa sekta ya utalii.

    Benki hiyo imesema itaendelea kutoa huduma na suluhisho za kifedha zitakazowawezesha wafanyabiashara kupata mitaji, kupanua shughuli zao, kuongeza uzalishaji na kuwekeza katika fursa mpya za biashara, hususan maeneo yenye kasi ya ukuaji wa uchumi kama Kizimkazi.

    Kauli hiyo ilitolewa jana Jumapili, Agosti 16, 2026, na Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, wakati wa hitimisho la Tamasha la Kizimkazi mwishoni mwa wiki. Mgeni rasmi katika hitimisho hilo alikuwa Rais Samia Suluhu Hassan.

    Sabi alisema benki hiyo inaona fursa kubwa katika mabadiliko yanayoendelea Zanzibar na imejipanga kushirikiana na sekta binafsi kuzigeuza fursa hizo kuwa shughuli endelevu za kiuchumi.

    “NBC itaendelea kuwa mshirika wa wafanyabiashara na wawekezaji katika kutumia fursa zinazopatikana Zanzibar, ikiwemo Kizimkazi. Tumejipanga kutoa suluhisho mbalimbali za kifedha zitakazowasaidia kupata mitaji, kukuza biashara zao na hatimaye kuchangia katika ukuaji wa uchumi,” alisema.

    Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi (kulia), akizungumza na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba wakati wa hafla ya kuhitimisha Tamasha la Kizimkazi lililoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

    Sabi alisema uwezeshaji wa kifedha ni muhimu katika kujenga mazingira yanayowezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya uchumi, kwa kuwa ukuaji wa biashara unaweza kuongeza uzalishaji, ajira na fursa za kipato kwa wananchi.

    Kauli hiyo imekuja wakati Zanzibar, hususan maeneo ya Kusini, ikiendelea kushuhudia ongezeko la shughuli za kiuchumi linalochochewa na uwekezaji katika sekta ya utalii na maendeleo ya miundombinu.

    Akihitimisha tamasha hilo Agosti 14, 2026, Rais Samia Suluhu aliwahimiza wafanyabiashara na wawekezaji kutumia fursa zinazozidi kujitokeza Zanzibar.

    Rais Samia alisema Wilaya ya Kusini imepiga hatua kubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita kutokana na ongezeko la uwekezaji, hasa katika sekta ya utalii.

    “Wilaya ya Kusini imepata mabadiliko makubwa sana ikilinganishwa na mwaka 2016 kutokana na kuongezeka kwa fursa za biashara zilizotokana na uwekezaji, hususani kwenye maeneo ya utalii. Tamasha la Kizimkazi limekuwa chachu muhimu kuelekea mafanikio hayo. Hivyo, tunawakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji kutumia fursa hizi,” alisema.

    Akizungumzia wito huo, Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa NBC, Elvis Ndunguru, alisisitiza nafasi ya sekta binafsi katika kunufaika na mnyororo wa thamani unaotokana na ukuaji wa utalii.

    Alisema fursa hizo zinahusisha biashara za huduma, usafirishaji, malazi, chakula na vinywaji, bidhaa za ndani, burudani, sanaa na huduma nyingine zinazohusiana na utalii.

    “Dhamira ya NBC ya kushirikiana na wafanyabiashara na wawekezaji ipo wazi na inaakisi umuhimu wa upatikanaji wa huduma na mitaji inayowawezesha wadau wa sekta binafsi kuchangamkia fursa hizo na kuzifanya kuwa shughuli za kibiashara zenye tija na endelevu,” alisema.

    Ndunguru alisema ushiriki huo unaonesha dhamira ya NBC kwenda zaidi ya utoaji wa huduma za kifedha kwa kushirikiana na wadau katika masuala yenye umuhimu kwa maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kimazingira.

    Katika hafla hiyo, Rais Samia aliwashukuru wadau mbalimbali walioshiriki na kuchangia kufanikisha Tamasha la Kizimkazi, akiwemo NBC kwa mchango wake.

  • Samia: Fursa zinazoibuliwa Kizimkazi ziwaguse wananchi

    Samia: Fursa zinazoibuliwa Kizimkazi ziwaguse wananchi

    Unguja. Rais Samia Suluhu Hassan amefunga Tamasha la Kizimkazi akiwataka viongozi kuhakikisha fursa zinazozalishwa au kuibuliwa ndani ya tamasha hilo zinawagusa wananchi.

    Amesema kutokana na tamasha hilo, Wilaya ya Kusini imechangamka, imefurahi, imekuwa na biashara na imepata fursa ilizokusudia katika kuboresha maisha na ustawi wa wananchi.

    Rais Samia ametoa kauli hiyo leo, Agosti 14, 2026, wakati akihitimisha tamasha hilo katika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

    “Tunaziunga mkono na kuzichochea kwa wananchi wetu, kama Rais wa Zanzibar (Dk Hussein Mwinyi) alivyoahidi. Kwa hiyo, shangwe iwe lango la fursa, na fursa hizo ziwe chanzo cha ustawi wa wananchi wetu na taifa kwa ujumla,” amesema Dk Samia.

    Amesema miradi yote iliyozinduliwa au kujengwa kupitia tamasha hilo, ndiyo malengo hasa ya kuanzishwa kwa tamasha hilo.

    “Mnakubaliana nami nyote mlioshiriki tamasha hili, mmeona ukweli huu kwamba Kizimkazi na Wilaya ya Kusini kwa ujumla ilinoga,” amesema.

    Amesema baada ya shangwe hilo kumalizika, wananchi wabaki na huduma, miundombinu, biashara na fursa zinazoendelea kufanya kazi, huku akipongeza kaulimbiu ya mwaka huu akisema imetendewa haki.

    Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza na wananchi katika Kilele cha Tamasha la Kizimkazi (Kizimkazi Festival) lililofanyika, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 14, 2026.

    “Kaulimbiu ya mwaka huu inasema ‘Kizimkazi kumenoga, shangwe na fursa’. Asanteni sana mlioshiriki kuileta shangwe hiyo Kizimkazi na maeneo ya jirani, na hatimaye fursa kuibuka,” amesema.

    Rais Samia amesema Wilaya ya Kusini ya leo imebadilika, siyo kama ilivyokuwa miaka 10 au 15 iliyopita, tofauti na mwaka 2016 walipoanza tamasha hilo, ambapo Kizimkazi imekuwa na fursa nyingi za biashara na uwekezaji.

    Kwa mujibu wa kiongozi huyo, miundombinu na miradi wanayoijenga imeendelea kuvutia wananchi na wawekezaji kuja kufanya shughuli zao katika eneo hilo.

    “Nawaomba wale wote walioziona fursa ndani ya wilaya hii, waje kwa uwekezaji, tunawakaribisha. Rais wa Zanzibar ameweka mazingira mazuri sana ya uwekezaji. Karibuni sana kuja kuwekeza,” amesema Samia.

    Katika kutengeneza fursa, Rais Samia amesema wanajenga uwanja wa michezo ambao ukikamilika utaweza kutumika katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) itakayofanyika Juni 2027.

    Amesema: “Uwanja huo ni fursa kwenu wawekezaji kuja kuwekeza kwa ajili ya huduma zitakazotolewa kwa wachezaji na watu wote watakaoshiriki katika michuano hiyo.”

    Rais Samia ametumia fursa hiyo kusisitiza suala la amani, usalama na utulivu ndani ya nchi. Amesema kila anapopata fursa ya kuzungumza na wananchi, imekuwa ni utaratibu wake kusisitiza na kuwakumbusha umuhimu wa kuendelea kuzilinda na kuzitunza tunu hizo kwa nguvu zote.

    “Uwekezaji, maendeleo tunayoyaona hapa, uwekezaji, utalii, biashara, ajira na huduma za jamii, haya hayawezi kustawi katika mazingira ya vurugu na uvunjifu wa amani.

    “Niwaombe Watanzania wenzangu, hususan vijana, msikubali kuharibu amani ya nchi yenu. Amani ndiyo kila kitu katika maisha yetu. Tukatae kwa nguvu zote wasiolitakia mema taifa letu, na tulinde Tanzania yetu na Muungano wetu kwa mustakabali wa kizazi chetu na kizazi kijacho,” amesema Rais Samia.

    Kwa upande wake Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi, amesema tamasha hilo lina mchango mkubwa katika kutangaza, kuhifadhi na kuenzi mila na utamaduni, na hivyo kuchochea na kuhamasisha shughuli za maendeleo ya wananchi wa Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja na Zanzibar kwa ujumla.

    Amempongeza Rais Samia kwa maono yake ya kuanzisha tamasha hilo.

    “Hakika, mwaka huu tamasha hili limefana sana, hongereni sana. Mheshimiwa Rais Samia, tamasha hili limekuwa ni jukwaa muhimu la kuhamasisha shughuli za maendeleo, kwani pamoja na shughuli za burudani na michezo,” amesema Dk Mwinyi.

    Pia, amesema wameshuhudia uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo barabara, maji, elimu, afya, nyumba za makazi na viwanja vya michezo.

    Ametumia fursa hiyo kuahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha miradi yote iliyozinduliwa na ile itakayojengwa baadaye inatunzwa na kuendelezwa ipasavyo kwa maendeleo na ustawi wa wananchi.

    Dk Mwinyi ametoa wito kwa wananchi kuhakikisha miundombinu inayojengwa inatumika na kutunzwa vizuri ili idumu na kutumika kwa muda mrefu kama ilivyokusudiwa.

    Amesema Tamasha la Kizimkazi litaendelea kuwa chachu na kutoa mchango muhimu wa kuwavutia wageni Zanzibar, kuhamasisha utalii wa ndani na shughuli za uwekezaji Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

    Sherehe hizo zimehudhuriwa pia na Rais wa zamani wa Guinea-Bissau, Umaro Sissoco Embalo, Makamu wa Rais, Dk Emmanuel Nchimbi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, na viongozi wengine wa kidini na kisiasa.

    Awali, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Hamida Mussa Khamis, amesema tamasha hilo limegusa maeneo yote ya kihuduma, ikiwemo afya, elimu na ujasiriamali.

    Kwa mujibu wa Hamida, wajasiriamali wadogo wa Mkoa wa Kusini Unguja, maeneo ya Kizimkazi na shehia jirani, wamepata ajira na fursa mbalimbali.

    “Mheshimiwa Rais Samia, tunakushukuru sana. Tamasha limewakutanisha na taasisi za fedha; sasa hivi wananchi wa maeneo haya wanakopesheka na wanakopeshwa na taasisi zetu, na wameanza kufanya biashara,” amesema Hamida.

    Hamida amesema vijana wa mkoa huo sasa wamefikia fursa za kiutalii, uwekezaji na kujiajiri katika kazi mbalimbali za amali.

    “Kupitia maonyesho ya mwaka huu, tumesajili jumla ya wafanyabiashara 129 waliohitaji kuonyesha biashara ama huduma.

    “Pia, tulikuwa na wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo ambao hawakuingia kwenye mabanda ya maonyesho, wasiopungua 200, hata yule mdogo ambaye alikuwa akiuza karanga, mikate, kachori na vitu kama hivyo,” amesema.

    Amesema tamasha limeendelea kuwaunganisha wanakusini, wana wa Kizimkazi na kuwakutanisha na watu mbalimbali kutoka ndani na nje ya Zanzibar.

    “Tamasha hili, kwetu sisi wana wa Kusini, tunasema linaimarisha Muungano wetu. Tunaendelea kuungana, na ndiyo maana leo hii tuna wageni wengi kutoka Tanzania Bara. Hii inaonyesha kwamba tamasha limelenga kuimarisha Muungano wetu, na sisi tunajivunia hilo,” amesema.

    Kwa mujibu wa mkuu huyo wa mkoa, tamasha hilo limewafanya waone thamani ya fursa zilizomo ndani ya mkoa wao.

  • Jaji Warioba atoa kauli sakata la Lissu

    Jaji Warioba atoa kauli sakata la Lissu

    Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe, Jaji Joseph Warioba amesema busara za kisiasa zinatakiwa kutumika ili kumwezesha Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia (Chadema), Tundu Lissu anayekabiliwa na kesi ya uhaini kuachiwa huru.

    Kauli ya Jaji Warioba imekuja baada ya siku mbili tangu wadau wa siasa na haki za binadamu, kueleza hatua nne za kiutu, ikiwemo kumuachia Lissu, katika kulirejesha Taifa pamoja baada ya matukio ya Oktoba 29, 2025.

    Jaji Warioba, mwanasheria na jaji wa siku nyingi na aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzia Novemba 5, 1985 hadi Novemba 9, 1990, amesema hayo katika Mahojiano la Mwandishi wa siku nyingi, Jenerali Ulimwengu.

    Amesema mamlaka aliyonayo Rais ya kutoa msamaha kwa wafungwa hayamaanishi kuingilia uhuru wa Mahakama, akieleza kuwa Rais anaweza kutumia mamlaka hayo pale anapoona kuna sababu za msingi za kuponya majeraha au kulinda masilahi mapana ya nchi.

    Amesema Mahakama inapomhukumu mtu, hata kwa adhabu kubwa kama kifungo cha muda mrefu au hukumu ya kifo, uamuzi huo unabaki kuwa wa Mahakama, lakini Katiba inampa Rais mamlaka ya kusamehe au kupunguza adhabu katika mazingira yanayofaa.

    “Mahakama imeamua, lakini Rais anaweza kusema huyu hapana. Ndiyo maana kila mwaka wakati wa siku ya Uhuru, hutolewa orodha ya watu ambao Rais amewasamehe. Anao uwezo huo,” amesema.

    Warioba amesema mamlaka hayo yanaweza kutumika pia katika mazingira ambayo nchi inahitaji kutuliza hali, kuponya majeraha na kufungua nafasi ya mazungumzo, akisisitiza kuwa hatua hiyo si kuingilia Mahakama, bali ni kutumia mamlaka aliyopewa Rais.

    “Mbowe alitiwa ndani lakini kwa sababau ya public interest (masilahi ya umma) na mambo yalivyokuwa, wakasema tumtoe ili tuweze kujadiliana, haikutoka sababu kwamba suala hili liko mahakamani hivyo hawawezi kuingilia mahakama.

    Akitoa mfano mwingine, amesema: “Mwaka jana wakati vijana wengi walikamatwa na kufikishwa mahakamani kutokana na vurugu za uchaguzi, Rais aliweza kuingilia kwa kuzingatia hali ya nchi na kuamua kuwa waachiliwe.”

    “Kwa nini katika hali Lissu ishindikane? Kwa sababu nchi iko katika hali fulani. Unaona ili tuponye majeraha haya, tuzungumze, ni vizuri huyu akaachwa kwa sababu ni mtu muhimu katika haya,” amesema.

    Amesema Tanzania haitakuwa nchi ya kwanza kutumia mamlaka hayo, akitoa mfano wa Afrika Kusini wakati wa utawala wa makaburu, ambapo baadhi ya watu walifungwa kutokana na misimamo yao ya kisiasa.

    Kauli ya Warioba inaungana na ile iliyowahi kutolewa na Julai 13, 2026 na mwanasiasa mkongwe na mwanazuoni wa uchumi, Profesa Anna Tibaijuka, aliyemshauri Rais Samia Suluhu Hassan kutumia hekima, busara na kuzingatia falsafa yake ya 4R aliyoasisi, kumwachia huru Lissu.

    Rais Samia alipoingia madarakani Machi 19, 2021 alitangaza kuongoza kwa kutumia falsafa za R nne, Reconciliation, Resilience, Reforms and Rebuilding, akimaanisha maridhiano, mabadiliko, ustahimilivu na kujenga upya.

    Kwa mujibu wa Tibajuka, kuendelea kwa kesi ya Lissu, na simulizi zinazoripotiwa na vyombo vya habari vya kimataifa, vinazidi kuibua hisia tofauti miongoni mwa vijana na kuathiri taswira ya Tanzania pamoja na masilahi yake katika jumuiya ya kimataifa.

    Ushauri huo wa Profesa ulienda sambamba na ule uliotolewa na Baraza la Mawaziri (CMAG) wa Jumuiya ya Madola, lililoipa Serikali ya Tanzania muda wa siku 30 kutafuta suluhisho la kisiasa na kisheria kuhusu kesi inayomkabili Lissu. Taarifa hiyo ilitolewa baada ya kikao cha 73 cha dharura cha CMAG kilichofanyika Julai 10, 2026.

    Katika mahojiano yake juzi yaliyofanywa na mwanahabari mkongwe Jenerali Ulimwengu na kurushwa na JU Post, Jaji Warioba amejenga hoja yake akirejea namna baadhi ya wanasiasa waliowahi kuwekwa gerezani, lakini Rais Samia akawatoa.

    Jaji Warioba alieleza namna Rais Samia alivyomtoa gerezani Mwenyekiti wa zamani wa Chadema, Freeman Mbowe aliyekuwa akikabiliwa na mashitaka ya ugaidi.

    “Mbowe aliwekwa ndani, kwa sababu ya masilahi ya umma na mambo yalivyokuwa, akatoka ili kujadiliana,” ameeleza Warioba.

    Julai 21, 2021 Mbowe alikamatwa na Polisi jijini Mwanza kisha kusafirishwa hadi Dar es Salaam kwa tuhuma za ugaidi.

    Agosti 16, 2021 Mbowe alishtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kwa makosa mbalimbali ikiwemo kufadhili vitendo vya ugaidi na alikaa ndani kwa miezi minane.

    Baadhi ya viongozi wa kisiasa walimwomba Rais Samia kumwachia Mbowe, miongoni mwao alikuwa Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe wakitaka kuingilia kati sakata la Mbowe, wakisema Rais anao uwezo huo.

    Novemba 13, 2025 akihutubia Bunge Rais Samia Suluhu aliviagiza vyombo vya ulinzi na usalama ikiwemo ofisi ya DPP kuchuja makosa ya vijana wanaoshtakiwa kwa makosa ya uhaini baada ya maandamano yaliyosababisha vurugu wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.

    Rais Samia alisema kwa wale vijana waliofanya makosa kwa kufuata mkumbo waachiwe huru.

    “Natambua kuna vijana wengi wamekamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhaini, hawakujua wanachokifanya,”

    “Wengine walifuata mkumbo, nikiwa kama mama navielekeza vyombo vya kisheria kuangalia makosa yaliyofanywa na vijana wetu, kwa wale waliofanya mambo kwa kufuata mkumbo na hawakudhamiria kufanya uhalifu wawafutie makosa yao,” alisema Rais Samia.

  • Kiswahili chazidi kujitanua duniani, watafiti kukutana Kampala

    Kiswahili chazidi kujitanua duniani, watafiti kukutana Kampala

    Dar es Salaam. Watafiti na wanataaluma wa Kiswahili wamepewa fursa ya kushiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu maendeleo ya lugha hiyo kupitia kongamano la Kiswahili litakalofanyika Kampala, nchini Uganda, wakati Kiswahili kikizidi kupanua ushawishi wake katika elimu, diplomasia, utamaduni na mawasiliano ya kimataifa.

    Fursa hiyo imetolewa na Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (Chaukidu), ambacho kimeongeza hadi Agosti 26, 2026, muda wa kutuma ikisiri za makala kwa ajili ya kongamano hilo.

    Uamuzi huo umetokana na maombi kutoka kwa wanachama na wadau mbalimbali wa Kiswahili waliotaka muda zaidi wa kukamilisha kazi zao na kuziwasilisha.

    Katika taarifa iliyosainiwa leo, Agosti 17, 2026, na Mkurugenzi wa Chaukidu, Dk Mussa Hans, chama hicho kimewataka wanachama na wadau ambao bado hawajawasilisha ikisiri kutumia muda huo wa nyongeza kukamilisha kazi zao na kuzifikisha kabla ya tarehe hiyo.

    Dk Hans amesema uamuzi huo umezingatia maombi yaliyowasilishwa na wanachama, huku akisisitiza kuwa muda huo unapaswa kutumiwa vizuri na wale ambao bado wanakamilisha kazi zao.

    Mbali na kuwasilisha ikisiri, Chaukidu imewakumbusha wanachama kuendelea kuimarisha uanachama wao kwa kulipa ada ya mwaka 2026, hatua inayolenga kuwezesha chama kuendelea na shughuli zake za kukuza na kuendeleza Kiswahili.

    Kongamano hilo linakuja wakati Kiswahili kikizidi kupata nafasi katika majukwaa ya kimataifa, hali inayoongeza hitaji la tafiti na mijadala ya kitaaluma kuhusu namna ya kukiendeleza na kukifanya kiendane na mabadiliko ya dunia.

    Akizungumza katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani yaliyofanyika Makao Makuu ya Unesco jijini Paris, Ufaransa, Julai 7, 2026, Waziri Mkuu Mwigulu Nchemba alisema kuna haja ya kutafuta mbinu mpya za kukieneza Kiswahili baada ya lugha hiyo kupata hadhi kubwa kimataifa.

    “Kadiri Kiswahili kinavyoendelea kupata hadhi ya kimataifa, ni muhimu sasa kuanza kutazama hatua inayofuata ya kukieneza duniani,” alisema.

    Alisema Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili ndani na nje ya Tanzania kupitia elimu, tafiti, uchapishaji, tafsiri, teknolojia za kidijitali na diplomasia ya lugha, kwa kushirikiana na Unesco, vyuo vikuu, nchi mbalimbali na taasisi za kimataifa.

    Kauli hiyo inaonesha umuhimu wa majukwaa ya kitaaluma kama kongamano la Chaukidu, ambayo huwapa watafiti nafasi ya kuwasilisha matokeo ya tafiti zao, kubadilishana maarifa na kujadili changamoto na fursa zinazolikabili Kiswahili katika dunia ya sasa.

    Kwa upande wa Unesco, Mkurugenzi Mkuu Khaled El-Enany amesisitiza nafasi ya Kiswahili katika kuwaunganisha watu na kuongeza fursa za elimu na maarifa.

    Katika Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani ya mwaka huu, Unesco iliweka mkazo katika kaulimbiu “Kiswahili kwa Amani, Mshikamano na Diplomasia ya Kiuchumi Duniani,” ikieleza kuwa lugha hiyo ina nafasi katika kukuza amani, mazungumzo, utambulisho wa kitamaduni, elimu, ushirikiano wa kikanda na mahusiano ya kimataifa.

    Naye Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Saidi Othman Yakub, alisema maadhimisho hayo yaliwakutanisha zaidi ya washiriki 300 kutoka nchi 16 duniani, huku shughuli mbalimbali zikilenga kuendeleza na kukitangaza Kiswahili kimataifa.

    Unesco inaeleza kuwa Kiswahili kina zaidi ya wazungumzaji milioni 200 katika Afrika Mashariki, Kati na Kusini na maeneo mengine duniani, huku Siku ya Kiswahili Duniani ikiwa sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa na matumizi ya lugha hiyo kimataifa.

    Kwa msingi huo, watafiti na wanataaluma wanaoshiriki kongamano hilo wanatarajiwa kuwa sehemu ya mjadala mpana kuhusu mustakabali wa Kiswahili, ikiwamo nafasi yake katika elimu, teknolojia, uchumi, utamaduni na diplomasia.

    Kwa Chaukidu, kuongeza muda wa kuwasilisha ikisiri hadi Agosti 26 ni nafasi kwa watafiti ambao bado hawajakamilisha kazi zao kujiunga na jukwaa hilo na kuchangia maarifa mapya yanayoweza kuimarisha nafasi ya Kiswahili ndani na nje ya Afrika.

  • Wateja wa simu, vifaa vya umeme wanavyopigwa Kariakoo

    Wateja wa simu, vifaa vya umeme wanavyopigwa Kariakoo

    Dar es Salaam. Simu, vifaa vya umeme vinavyowatesa wanunuzi vuta picha unanunua simu kwenye duka, ukipewa boksi, risiti na hata dhamana ya miezi kadhaa, lakini baada ya siku chache kifaa kinaanza kuganda, betri kuisha haraka au kamera kupoteza ubora.

    Huo ni uzoefu ambao baadhi ya wanunuzi wa simu na vifaa vya umeme wameueleza, wakisema changamoto hizo zimekuwa zikiwafanya kuwa na wasiwasi kuhusu hali halisi ya bidhaa wanazonunua.

    Malalamiko hayo hayahusu simu pekee, bali pia baadhi ya vifaa vya umeme ikiwamo majokofu, televisheni, pasi na majagi, ambavyo baadhi ya wanunuzi wanasema huanza kupata hitilafu muda mfupi baada ya manunuzi.

    Uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa katika biashara ya simu na vifaa vya umeme, zipo bidhaa mpya, zilizotumika na nyingine ambazo zimewahi kufanyiwa ukarabati kabla ya kurejea sokoni.

    Changamoto kubwa inayojitokeza ni kwamba wakati mwingine mnunuzi haelezwi kwa uwazi historia ya bidhaa anayoinunua, hali inayoweza kusababisha malalamiko pale kifaa kinapopata hitilafu.

    Mkazi wa Malamba Mawili, Dar es Salaam, Shida Mbwana, anasema alifika kununua simu ya Samsung akiwa na Sh400,000, wakati simu mpya aliyokuwa akiihitaji ikiuzwa Sh540,000.

    Anasema baada ya kueleza kiasi alichokuwa nacho, alionyeshwa simu iliyotumika kutoka Dubai kwa Sh380,000.

    “Tulikuwa tunahitaji simu nzuri ya Samsung, lakini tulipofika tukawaambia tuna Sh400,000 tukaonyeshwa nyingine iliyotumika kwa Sh380,000 na tukaambiwa imetoka Dubai,” anasema.

    Anasema walipewa dhamana ya miezi mitatu, lakini baada ya wiki moja kamera ilianza kutoa picha zisizo na ubora huku betri ikiisha chaji haraka.

    Waliporudi dukani, anasema waliambiwa simu ilifanyiwa majaribio kabla ya kuondoka na huenda waliiangusha nyumbani.

    Tatizo kama hilo lilimkuta Khalfan Mussa, mkazi wa Morogoro, anayesema alibadilisha simu na kuongeza fedha, lakini baada ya wiki mbili kifaa kilianza kusimama na hata simu ikiita, hakikubali kupokea.

    “Nimejifunza ukinunua simu ni vizuri uwe na mtu anayeyajua maduka vizuri. Nimeshawahi kupewa simu isiyofanya kazi vizuri na niliporudisha nikaambiwa ni makosa yangu,” anasema.

    Mfanyabiashara wa simu, Sheila Mjata, anasema biashara ya kubadilishana simu maarufu kama top-up imekuwa ikiwasaidia wananchi kupata vifaa bora kwa gharama wanazoweza kuzimudu.

    Anasema mteja hupeleka simu aliyokuwa akitumia, thamani yake hukadiriwa na kisha kuongeza fedha ili kupata nyingine yenye thamani kubwa zaidi.

    Kwa mujibu wake, baadhi ya simu zinazopokelewa huwa na maboksi, chaja na vifaa vyake vya awali, huku zenye hitilafu ndogo zikifanyiwa marekebisho kabla ya kuuzwa tena.

    Hata hivyo, anasisitiza kuwa mnunuzi anapaswa kufahamishwa kama simu ni mpya au imeshatumika.

    “Bei ya simu iliyotumika haiwezi kuwa sawa na mpya. Maelezo sahihi ni muhimu ili kuepusha malalamiko baadaye na kuitana matapeli,” anasema.

    Mfanyabiashara mwingine, Hassan Ramadhani, anasema katika duka lao huuza simu mpya na zilizotumika, lakini huzitenganisha ili mteja ajue anachonunua.

    “Zilizotumika huwa wazi na tumezipanga tofauti na bei zake ni za chini, zipo hadi za Sh130,000,” anasema.

    Hata hivyo, anasema baadhi ya simu hufanya kazi vizuri dukani, lakini baada ya siku kadhaa mteja hurudi akilalamikia programu kutofanya kazi au chaji kuisha haraka.

    Hata hivyo kuna wanaosema baadhi ya simu hurudishwa sokoni zikiwa zimetumiwa sana.

    “Nilinunua simu hapa sokoni Arusha kweli niliambiwa ni zilizotumika Dubai, ila nilipoinunua nilibaini ilitumika sana na ninahisi ni hizi za top up, mtu anaitumia ikimsumbua anakwenda kuibadili analipa pesa kidogo anapewa nyingine,”anasema Akida Mrosso.

    “Siku wanatumia kichaka cha simu used (zilizotumika)kutoka Dubai kuuza hizi wanazozipata kwa wanaotop up, zinakuwa zimetumika sana na ukitumia kidogo inaharibika na haikarabatiki tena,”anasema Sikudhani Juma, mkazi wa Kilosa.

    Akizungumzia ukarabati wa simu, fundi wa simu Mtaa wa Aggrey Dar es Salaam, Mansour Pembe, anasema ukarabati ni sehemu ya kawaida ya biashara hiyo, akieleza kuwa hubadilisha skrini, vioo, nyumba za simu, betri na vipuri vingine.

    “Baada ya kutengenezwa, baadhi huuzwa tena kwenye maduka au hata na mafundi wenyewe,” anasema.

    Kwa mujibu wake, tatizo si bidhaa kufanyiwa ukarabati, bali mnunuzi kutofahamishwa kuwa kifaa alichonunua kimewahi kutumika au kufanyiwa marekebisho.

    Mfanyabiashara wa vifaa vya umeme, Abbas Mahamoud, anasema baadhi ya wateja huchagua bidhaa zilizotumika kwa sababu ya bei kuwa nafuu.

    “Si kila mtu anaweza kununua bidhaa mpya. Mtu anaweza kuja na Sh250,000 wakati jokofu jipya ni Sh350,000, hapo tunamwonyesha lililotumika linalolingana na fedha zake,” anasema.

    Maria Godfrey anasema amewahi kununua friji ndogo iliyoharibika muda mfupi baadaye, jambo lililomfanya kuwa mwangalifu zaidi anaponunua vifaa vilivyotumika.

    Mtaalamu wa uchumi, Sophia Mussa, anasema biashara ya bidhaa zilizotumika inaweza kuwasaidia watu wa viwango tofauti vya kipato kupata vifaa wanavyohitaji.

    Anasema changamoto inaanza pale bidhaa iliyotumika au iliyofanyiwa ukarabati inapouzwa kama mpya bila kumweleza mnunuzi historia yake.

    “Kuuza bidhaa iliyotumika si tatizo ikiwa mteja anaelezwa hali yake kabla ya manunuzi. Tatizo linakuwa pale inapouzwa kama mpya bila taarifa sahihi,” anasema.

    Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limesema limebaini wimbi la matukio ya utapeli yanayowalenga wananchi kupitia shughuli mbalimbali za kiuchumi.

    Akizungumza na waandishi wa habari Jumanne, Agosti 4, 2026, Kamanda wa Kanda hiyo, Jumanne Muliro, alisema baadhi ya watuhumiwa hutumia mbinu mbalimbali kuwahadaa wananchi na kujipatia fedha kwa udanganyifu.

    Alisema wamekamatwa watuhumiwa wanaohusika na kuvunja nyumba, kuiba na kununua mali za wizi, zikiwemo simu, luninga, pikipiki, laptop na redio.

    Kamanda Muliro aliwataka wananchi kutoa taarifa zenye viashiria vya kihalifu ili zifanyiwe kazi.

    Haji Adam, fundi simu na mtaalamu wa teknolojia  anasema hakuna kipimo kimoja kinachoweza kuthibitisha kwa uhakika kuwa simu imetumika, lakini mnunuzi anaweza kufanya ukaguzi maeneo kadhaa kabla ya kuinunua.

    Anashauri kwanza kukagua afya ya betri, kwa kuwa baadhi ya simu huonyesha uwezo wake uliobaki na historia ya matumizi. Kwa iPhone, taarifa hizo hupatikana kupitia Settings > Battery > Battery Health & Charging. Ikiwa simu inayodaiwa kuwa mpya ina uwezo wa betri uliopungua, anasema mnunuzi anapaswa kuwa makini.

    Kwa baadhi ya simu za Android, taarifa za betri hupatikana kwenye sehemu ya Battery, ingawa hatua hutofautiana kulingana na aina na toleo la simu. Mnunuzi anaweza pia kuangalia battery cycle count ikiwa kifaa kinaonyesha taarifa hiyo, kwani idadi kubwa inaweza kuashiria matumizi ya muda mrefu.

    Aidha, anashauri kuangalia Battery Usage ili kuona programu zilizotumika na historia ya matumizi. Simu mpya kabisa kwa kawaida haitakuwa na historia ya matumizi ya muda mrefu.

    Pia, mnunuzi akague tundu la kuchajia, chaja na kebo kwa kuangalia mikwaruzo, uchafu au alama za kuchakaa zinazoweza kuonyesha matumizi ya muda mrefu.

    Mwisho, anashauri kuangalia kama simu ina akaunti, picha, programu, faili au mipangilio iliyowekwa na mtumiaji mwingine. Simu mpya kwa kawaida huanza kwenye hatua ya awali kwa kila program.

  • Wanawake wanufaika na maonyesho ya uvuvi

    Wanawake wanufaika na maonyesho ya uvuvi

    Rukwa. Maonyesho ya sekta ya uvuvi yameanza kuleta matokeo chanya kwa kuwaunganisha wavuvi, wanawake, wasindikaji, wawekezaji na wanunuzi, hatua inayowawezesha kupata masoko mapya na kuongeza thamani ya bidhaa zao.

    Mtaalamu wa masuala ya uvuvi na maendeleo ya jamii, Profesa Esther Ishengoma, amesema maonyesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu kwa makundi ambayo hayajapata nafasi ya kutosha katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

    Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili, Agosti 16, 2026, Profesa Ishengoma amesema lengo kuu la maonyesho hayo ni kuwawezesha wavuvi, hasa wanawake wanaojihusisha na usindikaji na uuzaji wa bidhaa za uvuvi, kukutana moja kwa moja na wanunuzi, wawekezaji na wasindikaji wengine.

    “Lengo letu kuu lilikuwa kuwapa fursa wavuvi, hasa wanawake wanaojihusisha na usindikaji na uuzaji wa bidhaa za uvuvi, waweze kuonyesha bidhaa zao moja kwa moja kwa wanunuzi na wawekezaji bila kupitia mawakala,” amesema.

    Amesema wanawake na wavuvi wadogo wana mchango mkubwa katika usalama wa chakula na uendelevu wa rasilimali za uvuvi, licha ya kukabiliwa na changamoto za masoko.

    “Tuliamua kuwapa nafasi kwa sababu ndio walio wengi katika sekta, lakini pia ndio wanaokabiliwa na changamoto kubwa zaidi za masoko. Mwanamke anapopata soko zuri, anaweza kuboresha lishe ya familia nzima. Mvuvi anapopata mkataba mzuri, anapunguza uvuvi haramu kwa sababu anakuwa na kipato cha uhakika,” amesema.

    Kwa mujibu wa Profesa Ishengoma, maonyesho hayo tayari yameanza kuleta matokeo, yakiwemo baadhi ya washiriki kupata wateja wa hoteli, mikataba ya kusambaza bidhaa madukani na kukutana na taasisi za fedha na zinazotoa mafunzo ya uongezaji thamani.

    Amesema baadhi ya wanawake wamepata ujuzi wa ufungaji na ubora wa bidhaa, huku wengine wakianzisha vikundi vya uzalishaji ili kuongeza uwezo wa kupata masoko makubwa.

    FISH4ACP yaongeza thamani

    Programu ya FISH4ACP ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) ni miongoni mwa mipango inayosaidia kuimarisha uwezo wa wadau wa sekta ya uvuvi nchini.

    Programu hiyo inalenga kuifanya minyororo ya thamani ya uvuvi na ufugaji wa viumbe wa majini katika nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki kuwa endelevu, ikitekelezwa na FAO na washirika wake kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya na Wizara ya Shirikisho ya Ujerumani ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (BMZ).

    Kupitia ushirikiano na Wizara ya Uvuvi, FISH4ACP imekuwa ikiwasaidia wasindikaji wadogo kupata mafunzo kuhusu usafi, ubora wa bidhaa na taratibu za kupata vibali vya kusafirisha mazao nje ya nchi.

    Wanawake na vijana katika mwambao wa Ziwa Tanganyika mkoani Rukwa, Katavi na Kigoma wamewezeshwa kuanzisha shughuli za kuongeza thamani, ikiwemo usindikaji wa dagaa, kukaanga samaki kwa teknolojia safi na kufungasha bidhaa kwa viwango vinavyokubalika katika masoko ya kimataifa.

    Mgeni Lubinsha wa Kata ya Kabwe, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa, ambaye ni mvuvi na mchakataji wa mazao ya majini, amesema, “Tulikuwa tunategemea soko la mtaani. Baada ya mafunzo na kushiriki maonyesho, sasa nina oda kutoka mataifa mbalimbali, ikiwemo Kenya. Haya ni mabadiliko makubwa kwetu.

    Amesema awali dagaa walikuwa wakianikwa chini na kuuzwa kwa bei ndogo, lakini sasa wanatumia vifungashio bora, teknolojia za kisasa za ukaushaji na vikundi vya wanawake vinavyosindika dagaa kuwa unga na bidhaa za lishe.

    Mdhibiti Ubora wa Masoko ya Mazao ya Uvuvi na mtoa leseni za kusafirisha mazao ya uvuvi nje ya nchi, Theresia Malobya, amesema leseni hizo ni muhimu katika kukuza biashara na uchumi wa ndani.

    Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Wavuvi, Francis Lubavu, amesema baada ya wanachama wake kushiriki maonyesho mwaka jana, mapato yao yaliongezeka kwa asilimia 40, huku baadhi ya watoto wakirejea shuleni na wanawake kupata mitaji.

  • Sura mbili mbio za uchaguzi Kenya, Ruto akimrushia kijembe Kenyatta

    Sura mbili mbio za uchaguzi Kenya, Ruto akimrushia kijembe Kenyatta

    Dar es Salaam. Malumbano ya kisiasa nchini Kenya yameendelea kupamba moto kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, baada ya Rais William Ruto kuwatuhumu baadhi ya wapinzani wake kuwa wanatumwa na “sponsor” ambaye hakumtaja, lakini maelezo yake yakionekana kumlenga Rais mstaafu, Uhuru Kenyatta.

    Ruto alitoa kauli hiyo Agosti 13, 2026, mjini Eldoret, Uasin Gishu County, alipozungumza na wananchi baada ya kuhudhuria shughuli katika KDF Recruits Training School (RTS), ambako aliongoza sherehe ya kuhitimu kwa kundi la kwanza la mwaka 2025.

    Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanazungumzia kijembe hicho kilichotolewa na Ruto kuwa kinachangamsha siasa za Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, ambapo hoja mbalimbali zitatolewa majukwaani, huku mwisho wa siku wananchi wakiwa ndio wataamua.

    Katika hotuba yake, Ruto aligusia utendaji wa Serikali ya zamani katika miradi ya nyumba za gharama nafuu (Affordable Housing), bima ya afya kwa wote (Universal Health Coverage) na elimu, akidai kuwa mdhamini huyo wa wapinzani wake alishindwa kutekeleza mambo hayo alipokuwa madarakani.

    Ingawa hakumtaja kwa jina, maelezo yake yalionekana kumlenga moja kwa moja mtangulizi wake, Kenyatta, ambaye Ruto aliwahi kuwa mshirika wake wa kisiasa akiwa Naibu Rais, kabla ya wawili hao kutofautiana kisiasa.

    Ruto, pia, alidai kuwa mdhamini huyo amekwenda kupanga ‘vibaraka’ wake na kuwatuma kushindana naye kuelekea uchaguzi wa 2027, huku akisema hana wasiwasi na wapinzani hao.

    Huku akishangiliwa na wananchi, Ruto alisema: “Kila kiongozi anapimwa na ile kazi amefanya, hakuna mtu atakuja kututapeli hapa ati atwambie, ‘oh, sijui kasongo one term, must go’, ati alafu tumpatie kazi, yaani ufala bana.

    “Mimi ninawauliza watu wa Eldoret, si nyinyi ni Wakenya? Si mmewahi kupiga kura? Si nyinyi ni mafundi wa siasa? Si mnajua viongozi wote?

    “Nataka niwaulize, mkipima wale watu, yule sponsor wao, yule sponsor wao si alishindwa na maneno ya affordable housing? Si alishindwa na mambo ya Universal Health Coverage? Si alishindwa na maneno ya kusomesha watoto wetu?

    “Sasa ameenda kupanga vibaraka wake, ati anatuma hapa watu, ati waje washindane na mimi, hawa watu nitawaosha asubuhi na mapema,” amesema Ruto.

    Ameongeza kuwa: “Wale watu mmesikia mipango yao? Mmesikia ajenda yao? Mmesikia sera yao? Mmesikia maono yao? Oh, kumbe mnawajua? Wale majamaa hawana mpango… sera… ajenda… maono… hata akili hawana kabisa.”

    Sura mbili za siasa za Kenya

    Kauli ya Ruto imeongeza mjadala kuhusu sura inayochukua ushindani wa kisiasa nchini Kenya, hasa wakati wanasiasa wanapoanza kujenga hoja kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

    Mchambuzi wa masuala ya kisiasa, Profesa Mohammed Makame, amesema malumbano ya aina hiyo ni sehemu ya ushindani wa kisiasa katika mfumo wa vyama vingi, ambapo pande zinazoshindana hutumia hoja mbalimbali kujenga ushawishi kwa wananchi na kuimarisha nafasi zao kuelekea uchaguzi.

    Amesema malumbano hayo yanaweza kuwa na sura mbili; kwanza, yanaweza kutumiwa kuonesha uimara wa chama au kiongozi wa kisiasa na kutafuta uungwaji mkono wa wananchi ili kurejea madarakani.

    “Vilevile, yanaweza kujikita katika utekelezaji wa ilani na sera, ambapo kila upande hujaribu kuonesha kwa nini unastahili kupewa ridhaa ya wananchi,” amesema.

    Amesema vyama vya upinzani kwa kawaida hujikita katika kuonesha udhaifu wa chama kilichopo madarakani, ikiwamo kukosoa utekelezaji wa ilani na kuunganisha hoja hizo na hali halisi inayowakabili wananchi katika masuala ya kijamii na kiuchumi.

    “Kwa upande wa Rais Ruto, bila shaka ana nia ya kuendelea na kugombea, hivyo anapambana na vitu vyote viwili. Kwa wale wanaomuunga mkono, watakuwa wakilinda na kutetea yale aliyoyafanya na mabadiliko aliyoyaleta,” amesema.

    Amesema Ruto na wafuasi wake, pia, wanahitaji kulinda uimara wa chama chao na kujenga mtaji wa wanachama ambao ni muhimu katika uchaguzi mkuu, huku upande wa pili ukijikita katika kutafuta madaraka kwa kuonyesha mapungufu ya Serikali iliyopo.

    Makame amesema katika mazingira hayo, ukosoaji unaweza kuwa wa aina mbili, ikiwamo ule unaochambua kwa kina ukweli na matokeo ya utekelezaji wa Serikali, na ule wa kisiasa unaolenga kujenga uhalali wa kisiasa wa upinzani kwa kuwaaminisha wananchi kuwa Serikali iliyopo haijafanya vya kutosha.

    “Lakini pia kuna kukosoa political, kwa maana ya kutengeneza legitimacy (uhalali) ya upinzani kwamba aliyepo madarakani hakuweza kufanya kitu,” amesema.

    Amesema mazingira ya kisiasa Kenya yanaweza kuathiriwa na masuala ya kikanda na siasa za makabila, ambayo kwa muda mrefu yamekuwa sehemu ya mijadala ya kisiasa nchini humo.

    “Kauli zinazotolewa na Ruto zinaweza kutafsiriwa kama sehemu ya mkakati wa kujilinda kisiasa kwa kuonesha mambo ambayo Serikali yake imefanikiwa kufanya katika kipindi alichokuwa madarakani, hasa ikiwa ana mpango wa kuomba ridhaa ya wananchi kwa muhula mwingine.

    “Anapomwangalia aliyetoka madarakani, naye anamwangalia mpinzani kama ni mpinzani, kwa hiyo ruling party (chama tawala) inakuwa opposition party (chama cha upinzani),” amesema.

    Profesa Makame amesema hali hiyo inafanya hata chama kilicho madarakani kuendelea kumtazama mpinzani kama tishio linalopaswa kuzuiwa kupata nafasi ya kuingia madarakani, akibainisha kuwa kauli kama hizo zinaweza kuendelea kuongezeka kadiri uchaguzi wa 2027 unavyokaribia.

  • JKCI, CCBRT zapokea Sh200 milioni mbio za CRDB

    JKCI, CCBRT zapokea Sh200 milioni mbio za CRDB

    Dar es Salaam. Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Hospitali ya CCBRT zimepokea Sh200 milioni zilizotokana na mbio za hisani za CRDB Bank Marathon, fedha zinazolenga kuboresha huduma za afya na kuongeza upatikanaji wa matibabu kwa makundi yenye uhitaji.

    Katika hafla ilifanyika jana jijini Dar es Salaam, kila taasisi ilikabidhiwa Sh100 milioni, huku tukio hilo likiambatana na ujumbe wa kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi mara kwa mara na kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

    Mbio hizo zilihusisha washiriki wa kilomita tano, 10, 21 na 42 pamoja na mbio za baiskeli za kilomita 65, zikivutia maelfu ya wananchi kutoka makundi mbalimbali nchini.

    Mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, ambaye alisisitiza umuhimu wa kuendeleza shughuli zinazowakutanisha wananchi na kuimarisha afya zao ili waweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

    Hemed ambaye alimwakilisha waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba alisema ukiratibu Watanzania kufanya mazoezi unakuwa umeokoa fedha nyingi kwa sababu wagonjwa wengi wanaibiwa kwa mazoezi.

    “Kazi hii ambayo tumeifanya leo (jana) kuhakikisha Watanzania wamefanya mazoezi, tumeokoa fedha nyingi za Watanzania kwa sababu zaidi ya asilimia 40 hawakai ndani, wanatibiwa kisaikolojia tu kuwa wanatakiwa kufanya mazoezi,” alisema.

    Alisema uchumi wa Tanzania unategemea taasisi za fedha na CRDB imeonesha kwa vitendo na wanachangia mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

    “Kazi hii ambayo CRDB wameifanya inapaswa kuwa endelevu na inalindwa,” alisema Hemed huku akigusia ushiriki wa watu wengi kwenye mbio hizo ni ishara kwamba nchi ipo salama.

    Kwa upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk Juma Malik Akil, alisema Serikali itaendelea kuunga mkono mipango inayochangia ustawi wa jamii, akieleza kuwa mbio hizo zimekuwa chachu ya kuhamasisha mshikamano, afya na maendeleo ya wananchi.

    Naibu Waziri wa Afya, Dk Florence Samizi, akiambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Grace Magembe, walishiriki katika mbio hizo na kusisitiza kuwa afya kinga ndiyo msingi wa kupunguza mzigo wa magonjwa nchini.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk Abdulmajid Nsekela, alisema CRDB Bank Marathon imeendelea kuwa zaidi ya mashindano ya riadha, bali ni jukwaa linalounganisha michezo na dhamira ya kuleta mabadiliko yenye manufaa kwa jamii.

    Alisema kupitia mbio hizo, Benki ya CRDB imeendelea kutekeleza falsafa yake ya kurudisha kwa jamii kwa kusaidia sekta ya afya na makundi yenye uhitaji, huku kila mshiriki akiwa sehemu ya safari ya kubadilisha maisha ya Watanzania.

    “Safari ya CRDB Bank Marathon imeendelea kuonyesha kuwa michezo inaweza kuwa daraja la kuleta mabadiliko chanya katika jamii. Kila mwaka tumeshuhudia ongezeko la ushiriki na mchango mkubwa zaidi kwa sekta ya afya,” alisema.

    Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Foundation, Oswald Urassa, alimshukuru mgeni rasmi pamoja na washiriki na wadhamini wote kwa kuendelea kuiunga mkono mbio hiyo.

    Alisema bodi itaendelea kusimamia sera na miongozo itakayoiwezesha taasisi hiyo kuongeza ufanisi katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa jamii, hususan sekta ya afya.

    Kwa niaba ya wadhamini, Ofisa Mkuu wa Fedha wa Sanlam Allianz Tanzania, Samwel Mika, aliyemwakilisha Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, alisema wanafarijika kuwa sehemu ya safari ya CRDB Bank Marathon kutokana na mchango wake katika kugusa maisha ya wananchi.

    Aliahidi kuwa Sanlam Allianz Tanzania itaendelea kushirikiana na CRDB Bank Foundation kuhakikisha mbio hizo zinaendelea kuleta matokeo chanya kupitia miradi ya afya na maendeleo ya jamii.

    Mbali na kuchangisha fedha, mbio hizo zimeendelea kuwa jukwaa la kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kufanya mazoezi, kuzingatia lishe bora na kuchukua hatua za mapema katika kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.

    Wizara ya Afya ilieleza kuwa ushiriki wake katika mbio hizo unaendana na mkakati wa kuimarisha afya kinga na kuongeza ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya nchini.

  • Katoro: Mji wa fursa unaochanua kwa dhahabu, biashara na watu

    Katoro: Mji wa fursa unaochanua kwa dhahabu, biashara na watu

    Geita. Kuna miji ambayo huijui mpaka uambiwe, lakini kuna miji ambayo ukifika mara moja, unaelewa kwa nini watu wanaizungumzia. Katoro ni mmoja wapo.

    Mwezi uliopita, jina la mji huo lilivuka mipaka ya kawaida ya biashara na uchimbaji dhahabu na kuingia kwenye gumzo la kitaifa baada ya kufanyika kwa sherehe ya kifahari ya kumuaga Monalisa Buyamba, binti wa mfanyabiashara na mchimbaji dhahabu, Sylivester Buyamba, maarufu ‘GSM wa Katoro.’

    Helikopta iliyomfuata Monalisa nyumbani na kumpeleka kwenye ukumbi wa sherehe, pamoja na zawadi ya hundi ya Sh1.04 bilioni, vilifanya wengi waliokuwa hawaijui Katoro waanze kujiuliza: Katoro ni mji wa aina gani?

    Kwa nini watu wana pesa kiasi hicho? Na ni nini kinachoufanya mji huo uwe na mvuto mkubwa kiasi hiki? Wengine wanaita Kariakoo ya Geita.

    Jibu lake halipo kwenye harusi pekee, lipo kwenye dhahabu, samaki, biashara ya jumla, usafirishaji, kilimo, watu wanaohama kutoka maeneo mbalimbali na kasi ya mji unaokua kuliko miundombinu yake.

    Kwa mtu ambaye hajawahi kufika Katoro, mji huo unaweza kuonekana kama kituo kingine cha biashara Kanda ya Ziwa. Ukiingia unakuta ni mji wenye mchanganyiko wa shughuli na watu kutoka maeneo mbalimbali.

    Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro inaundwa na kata tatu za Nyamigota, Ludete na Katoro. Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, maeneo hayo yalikuwa na jumla ya wakazi 231,332.

    Hata hivyo, ongezeko la watu kutokana na kuzaliwa na uhamiaji kutoka maeneo mengine limeifanya idadi hiyo kutajwa kuwa imevuka watu 300,000.

    Katoro iko takribani kilomita 42 kutoka Geita mjini, safari inayoweza kuchukua dakika 30 hadi 40 kwa mujibu wa hali ya usafiri. Kutoka Mwanza ni karibu kilomita 167, Bukoba kilomita 258, Biharamulo kilomita 92, Chato kilomita 74 na Bukombe kilomita 103.

    Uwepo wa Uwanja wa Ndege wa Chato, uliopo takribani kilomita 61 kutoka Katoro, pamoja na Uwanja wa Ndege wa Mwanza, uliopo zaidi ya kilomita 170, nao umeongeza njia za kuufikia mji huo.

    Baada ya kuzinduliwa kwa Daraja la JP Magufuli katika eneo la Busisi, usafirishaji kwa barabara umeendelea kupata msukumo zaidi, hasa kwa biashara zinazounganisha Kanda ya Ziwa na maeneo ya Magharibi.

    Ukifika Katoro, baadhi ya mitaa utakayosikia ikitajwa mara kwa mara ni California, Kilimanjaro, Stamico, Mji Mwema, Mchongomani, Mtaa wa Afya, Merelani na Kilimahewa. Kinachovutia zaidi si majina ya mitaa pekee, ni kasi ya shughuli zilizopo.

    Asubuhi, wafanyabiashara wanafungua maduka. Sokoni, wanawake wanawahi mbogamboga, samaki, ndizi na nafaka. Magari yanaingia na kutoka, pikipiki zinabeba abiria na mizigo, na wafanyabiashara kutoka mikoa jirani wanafika kutafuta bidhaa za jumla.

    Katikati ya yote hayo, kuna dhahabu ambayo ni injini kubwa ya uchumi wa eneo hilo. Migodi inayopatikana katika maeneo yanayozunguka Katoro, ikiwamo Msasa, Buckreef, Nyarugusu, Nyaruyeye na Rwamugasa, imekuwa ikichochea mwingiliano wa watu na fedha.

    Ndiyo maana Katoro si tu mahali pa kuishi; kwa watu wengi, ni mahali pa kutafuta fursa. Mji huo umejijengea nafasi kama soko la bidhaa za jumla kwa wafanyabiashara kutoka Geita na mikoa jirani, ikiwamo Kagera na Kigoma.

    Katika eneo linalotambulika kama Soko la Kariakoo la Katoro, mfanyabiashara anaweza kupata simu, vifaa vya umeme, vifaa vya muziki, vifaa vya ushonaji, vitambaa, nguo na bidhaa nyingine za matumizi.

    Kwa upande wa chakula, Soko la Katoro-CCM ndilo moja ya kitovu kikubwa. Huko ndipo bidhaa kama nafaka, ndizi, viazi, mihogo, magimbi, matunda na samaki hupatikana.

    Katoro inasifika kwa kuwa na matawi ya benki zaidi ya matano, hali inayofanya uhakika wa usalama kifedha kuwa mkubwa.

    Uwepo wa vijiwe vya nyama choma, gym za mazoezi, sauna, supermarket, vimeutofautisha mji huo na maeneo mengine katika ukanda huo. Licha ya makao makuu ya mkoa huo kuwa Geita Mjini, Katoro ndiyo moja ya eneo lenye mwingiliano wa watu na biashara kuliko kwingineko.

    Sababu Katoro kuchangamka

    Beatrice John, mkazi wa Merelani na mfanyabiashara wa samaki katika Soko la Samaki Katoro-CCM, anasema uchimbaji wa madini una athari ya moja kwa moja kwenye biashara yake.

    Anaeleza fedha zinazopatikana migodini huingia kwenye mzunguko wa biashara mjini Katoro na kuufanya mji huo kuchangamka.

    “Wachimbaji wanapopata pesa kule, lazima huku Katoro pachangamke, kwa sababu kama samaki unauza Sh8,000, unaweza kumuuzia mteja kwa Sh9,000 au Sh10,000 na hakatai, yeye anafika analipa,” anasema.

    David Charles, mkazi wa Katoro anayefanya biashara ya nafaka na samaki kwa zaidi ya miaka 20, anasema samaki ni moja ya biashara zinazozungusha fedha kwa kasi mjini hapo.

    Anasema kila asubuhi hupokea magari matatu hadi matano pamoja na zaidi ya pikipiki 100 zinazoleta samaki kutoka maeneo ya ziwani. Kufikia saa tano asubuhi, anasema, mzigo mkubwa huwa tayari umenunuliwa na wafanyabiashara husubiri awamu nyingine inayofika mchana na jioni.

    “Biashara ya samaki inalipa kuliko ujasiriamali mwingine ulioko hapa. Hata mwenye duka, mimi ninayefanya ujasiriamali wa samaki, ananifuata mimi, kuna uzalishaji sana kwenye samaki,” anaeleza.

    Kwa mtazamo wake, ukiondoa dhahabu yenye thamani kubwa, samaki ni miongoni mwa shughuli zinazoweka fedha kwenye mifuko ya watu wengi kwa wakati mmoja, lakini biashara hiyo ina misimu yake. Kipindi cha kiangazi, upatikanaji wa samaki huwa mgumu zaidi ikilinganishwa na msimu wa masika.

    Hata baiskeli inazungusha uchumi wa Katoro

    Mkazi wa Rumasa, Matumbate Emmanuel, anaendesha baiskeli ya abiria, maarufu ‘daladala’. Kazi hiyo, anasema, imemsaidia kumudu maisha ya familia yake yenye watoto saba na mke, na kwa siku anaweza kupata kati ya Sh20,000 na Sh25,000.

    Mkazi wa Kilimahewa, Abel Kasanda, ni mmoja wa watu ambao hadithi ya Katoro imegusa maisha yao moja kwa moja. Akiuza vyombo vya kupikia kwa miaka mitatu, anasema aliingia kwenye biashara akiwa hana mtaji mkubwa wala mali.

    “Nilianza nikiwa mkono mtupu kwenye hii biashara ya umachinga wa vyombo, sikuwa na nyumba wala kiwanja, lakini kwa sasa namshukuru Mungu nimeshanunua kiwanja na kuanza ujenzi, boma lipo, bado kuezeka tu,” anasema.

    Kasanda anasema msimu mzuri wa biashara yake ni kiangazi, wakati baadhi ya wateja kutoka nje ya mji wanapokuwa wamevuna na kuuza mazao yao.

    Katoro, mji wa wahamiaji na tamaduni tofauti

    Katoro si mji wa kabila moja. Wasukuma, Wasumbwa na Wazinza ni miongoni mwa jamii za mwanzo kuishi katika eneo hilo, lakini kadiri biashara, uchimbaji na usafiri vilivyokua, watu kutoka maeneo mbalimbali wameendelea kuingia.

    Wachaga, Wajita, Waha, Wakurya, Wahaya na Wajaruwo ni miongoni mwa jamii zinazopatikana kwa wingi.

    Hii ndiyo sababu unaweza kuingia kwenye biashara moja ukakutana na mtu kutoka Kagera, mwingine Kigoma, mwingine Mwanza, huku anayekuuzia bidhaa akiwa mwenyeji wa Geita.

    Ukuaji wa Katoro hauonekani kwenye maduka pekee, unaonekana pia kwenye huduma za afya.

    Inakadiriwa kuwa kati ya watoto 900 na 1,000 huzaliwa kila mwezi, huku Kituo cha Afya Katoro kikitajwa kuhudumia wastani wa wanawake 33 wanaojifungua kwa siku.

    Ongezeko hilo la watu limeongeza mahitaji ya huduma za kijamii na kuufanya mji huo uwe na hospitali yenye hadhi ya wilaya iliyopo Mtaa wa Afya, pamoja na kituo cha afya cha Serikali Katoro-CCM na vituo binafsi.

    Usalama ulivyofungua biashara

    Mji wenye watu wengi na biashara nyingi unahitaji usalama. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Safia Jongo, anasema usalama wa Geita umeimarika kutokana na ushiriki wa wananchi kupitia mfumo wa Polisi Jamii.

    “Tunazifanyia kazi taarifa kutoka kwa jamii na wahalifu sugu waliokuwa wanasumbua ndani ya mkoa wetu, hatua mbalimbali za kisheria zimechukuliwa na matokeo yake ndiyo haya. Mkoa wa Geita tunaendelea kula bata saa 24, lakini wananchi wanafanya shughuli zao za kiuchumi,” anasema.

    Kasi ya ujenzi holela na ongezeko la watu limefanya baadhi ya maeneo ya Katoro kuwa na changamoto ya barabara na mitaro. Baadhi ya barabara huwa ngumu kupitika, huku katika maeneo mengine wananchi wakilalamikiwa kwa kuziba mitaro.

    Changamoto hiyo huwa kubwa zaidi wakati wa dharura, hasa pale moto au tukio jingine linapotokea na magari yanahitaji kufika kwa haraka.

    Barabara ya Katoro-Bukombe, yenye urefu wa zaidi ya kilomita 58, nayo imekuwa kilio cha wafanyabiashara na wachuuzi.

    Kwa mujibu wa Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Geita, Hosea Machaka, anasema ujenzi wa barabara hiyo wenye thamani ya Sh10.9 bilioni ulikuwa umefikia asilimia 48 wakati wa taarifa hii.

    Kukamilika kwake kunatarajiwa kurahisisha usafirishaji na kuongeza zaidi mwingiliano wa kibiashara kati ya maeneo hayo.

  • Ujumbe muhimu kwa malezi ya mtoto

    Ujumbe muhimu kwa malezi ya mtoto

    Dar es Salaam. Mtoto anayekulia katika mazingira yenye kila kitu, akipewa simu ya kisasa, kusoma shule nzuri na kushiriki burudani mbalimbali, bado anaweza kukosa maarifa muhimu ya maisha ikiwa hajawahi kukutana na mazingira yanayomsaidia kuelewa dunia inayomzunguka.

    Wataalamu wa saikolojia wanaeleza kuwa kabla mtoto hajafikisha miaka 13, mzazi ana nafasi kubwa ya kumjengea uwezo wa kufikiri, kuuliza maswali, kufanya uamuzi, kuwa na huruma na kuelewa tofauti za maisha kupitia uzoefu wa moja kwa moja.

    Badala ya kusubiri mtoto awe kijana ndipo aanze kujifunza kuhusu fedha, kazi, historia, utamaduni na maisha ya watu wengine, wazazi wanashauriwa kutumia miaka hiyo kumpeleka katika maeneo mbalimbali.

    Maktaba inaweza kuwa lango la mtoto kuelekea dunia ambayo hawezi kuiona katika mazingira yake ya kawaida.

    Kumpeleka maktaba humfundisha kuwa maarifa hayapatikani kupitia simu au mwalimu pekee, bali pia kupitia vitabu na kujisomea.

    Makumbusho nayo humkutanisha na historia, sanaa, utamaduni na simulizi za jamii mbalimbali.

    Akizungumza na Mwananchi, mwanasaikolojia Amina Msuya anasema uzoefu huo hujenga udadisi na uwezo wa mtoto kuuliza maswali badala ya kukubali kila jambo bila kutafakari.

    Shamba, soko na supermarket

    Mzazi anashauriwa kumpeleka mtoto shambani ili aone chakula kinapotoka kabla hakijafika mezani.

    “Aone mbegu ikipandwa, mazao yakitunzwa na kuvunwa. Hii humsaidia kuthamini kazi na chakula badala ya kuona kila kitu kinapatikana kwa urahisi,” anasema Amina.

    Katika soko, mtoto anaweza kujifunza biashara, mawasiliano na namna watu wanavyotafuta kipato, huku supermarket ikiwa darasa la fedha.

    Mtaalamu wa uchumi, Jesca Magolanga, anasema mzazi anaweza kumpa mtoto kiasi maalumu cha fedha na kumruhusu achague bidhaa, hatua inayomsaidia kujifunza bajeti, kufanya uchaguzi na kujizuia kununua vitu vinavyopita uwezo wake.

    Ziara ya benki inaweza kuwa mwanzo wa mazungumzo kuhusu kuweka akiba, matumizi na kupanga fedha.

    Kadhalika, mtoto akipelekwa mahali mzazi au ndugu anapofanya kazi anaweza kuona uhusiano kati ya elimu, ujuzi, kazi na kipato.

    “Mtoto anapopewa fursa ya kuona watu wakifanya kazi, huanza kuelewa mapema kuwa mafanikio yanahitaji juhudi, nidhamu na uwajibikaji,” anasema Jesca.

    Hospitali, zimamoto na polisi

    Hospitali inaweza kumfundisha mtoto umuhimu wa afya, huruma na kuwathamini watu wanaowahudumia wengine.

    Kituo cha zimamoto kinampa nafasi ya kuona watu wanaokabiliana na hatari kwa ajili ya kuwaokoa wengine, huku kituo cha polisi kikimsaidia kuelewa usalama, sheria, wajibu wa raia na kujiepusha na vitendo vya uhalifu.

    Hata hivyo, wataalamu wanashauri ziara hizo zifuatane na maelezo yanayoendana na umri wa mtoto ili zisijenge hofu, bali uelewa.

    Mtoto anaweza kujifunza kuhusu imani, maadili, huduma na mshikamano kupitia ziara katika nyumba ya ibada.

    Akizungumzia hilo, Sheikh Khamis Mataka anasema ni muhimu kwa wazazi kuwapeleka watoto kwenye nyumba za ibada ili wajifunze matendo mema na kuwa na hofu ya Mungu.

    Katika kituo cha jamii au taasisi inayosaidia watu wenye mahitaji, mtoto anaweza kuona kuwa si kila mtu anakulia katika mazingira yanayofanana.

    “Tuwapeleke huko wakaone maisha yalivyo, lakini tusiwafundishe kuwadharau walio katika hali duni. Lengo liwe kumjengea huruma na kutambua kuwa utu haupimwi kwa mali,” anasema Sheikh Mataka.

    Sanaa, michezo na mazingira

    Kumpeleka mtoto kwenye ukumbi wa sanaa humsaidia kuona ubunifu, muziki, uigizaji na usimulizi wa hadithi kwa vitendo.

    Tamasha la utamaduni humfanya aone kuwa utamaduni si jambo la kusoma kwenye kitabu pekee, wakati michezo humfundisha kazi ya pamoja, nidhamu, ushindani na kuheshimu mpinzani.

    Aidha, ufukwe, mlima, msitu au hifadhi humsaidia mtoto kuondoka kwenye skrini na kukutana na mazingira ya asili.

    Wataalamu wa saikolojia wanaeleza kuwa mazingira hayo yanaweza kuchochea udadisi na ubunifu kwa sababu mtoto hujifunza kupitia kuona, kugusa na kuchunguza.

    Chuo kikuu, maeneo ya kihistoria

    Mzazi asisubiri mtoto amalize sekondari ndipo aanze kuzungumza naye kuhusu chuo kikuu na taaluma.

    Ziara ya chuo kikuu inaweza kumsaidia kuanza kuona uwezekano wa maisha yake ya baadaye na kutambua taaluma mbalimbali.

    Vilevile, kumpeleka kwenye eneo la kihistoria na kumsimulia kilichotokea hapo hufanya historia iwe uzoefu halisi.

    Makaburi na historia ya familia

    Makaburi yanaweza kuwa sehemu ya mazungumzo yanayolingana na umri kuhusu maisha, kifo, kumbukumbu na urithi. Hata hivyo, mazungumzo hayo yasitumike kumtisha mtoto.

    Mzazi pia anaweza kumpeleka katika mji alikokulia, nyumbani kwa babu na bibi, biashara ya familia au sehemu ambako wazazi walikulia.

    Hii humsaidia mtoto kuelewa kuwa maisha yake ni sehemu ya simulizi kubwa lililotangulia kuzaliwa kwake.

    Moja ya safari muhimu zaidi inaweza kuwa kwenda sehemu ambayo mtoto hajawahi kufika. Mji mwingine, mazingira tofauti au jamii yenye utamaduni mwingine vinaweza kumlazimisha kuangalia, kuuliza, kuzoea na kujifunza.

    Malezi bora si kumkinga mtoto dhidi ya dunia kila wakati, bali kumtayarisha kuikabili dunia kwa uelewa.

    Kabla hajafikisha miaka 13, mtoto anaweza kuwa amejifunza kuhusu fedha, kazi, historia, utamaduni, mazingira, huruma, afya, imani, huduma kwa jamii na thamani ya maisha ikiwa mzazi atampa nafasi ya kujifunza nje ya darasa.