Blog

  • Sura mbili mbio za uchaguzi Kenya, Ruto akimrushia kijembe Kenyatta

    Sura mbili mbio za uchaguzi Kenya, Ruto akimrushia kijembe Kenyatta

    Dar es Salaam. Malumbano ya kisiasa nchini Kenya yameendelea kupamba moto kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, baada ya Rais William Ruto kuwatuhumu baadhi ya wapinzani wake kuwa wanatumwa na “sponsor” ambaye hakumtaja, lakini maelezo yake yakionekana kumlenga Rais mstaafu, Uhuru Kenyatta.

    Ruto alitoa kauli hiyo Agosti 13, 2026, mjini Eldoret, Uasin Gishu County, alipozungumza na wananchi baada ya kuhudhuria shughuli katika KDF Recruits Training School (RTS), ambako aliongoza sherehe ya kuhitimu kwa kundi la kwanza la mwaka 2025.

    Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanazungumzia kijembe hicho kilichotolewa na Ruto kuwa kinachangamsha siasa za Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, ambapo hoja mbalimbali zitatolewa majukwaani, huku mwisho wa siku wananchi wakiwa ndio wataamua.

    Katika hotuba yake, Ruto aligusia utendaji wa Serikali ya zamani katika miradi ya nyumba za gharama nafuu (Affordable Housing), bima ya afya kwa wote (Universal Health Coverage) na elimu, akidai kuwa mdhamini huyo wa wapinzani wake alishindwa kutekeleza mambo hayo alipokuwa madarakani.

    Ingawa hakumtaja kwa jina, maelezo yake yalionekana kumlenga moja kwa moja mtangulizi wake, Kenyatta, ambaye Ruto aliwahi kuwa mshirika wake wa kisiasa akiwa Naibu Rais, kabla ya wawili hao kutofautiana kisiasa.

    Ruto, pia, alidai kuwa mdhamini huyo amekwenda kupanga ‘vibaraka’ wake na kuwatuma kushindana naye kuelekea uchaguzi wa 2027, huku akisema hana wasiwasi na wapinzani hao.

    Huku akishangiliwa na wananchi, Ruto alisema: “Kila kiongozi anapimwa na ile kazi amefanya, hakuna mtu atakuja kututapeli hapa ati atwambie, ‘oh, sijui kasongo one term, must go’, ati alafu tumpatie kazi, yaani ufala bana.

    “Mimi ninawauliza watu wa Eldoret, si nyinyi ni Wakenya? Si mmewahi kupiga kura? Si nyinyi ni mafundi wa siasa? Si mnajua viongozi wote?

    “Nataka niwaulize, mkipima wale watu, yule sponsor wao, yule sponsor wao si alishindwa na maneno ya affordable housing? Si alishindwa na mambo ya Universal Health Coverage? Si alishindwa na maneno ya kusomesha watoto wetu?

    “Sasa ameenda kupanga vibaraka wake, ati anatuma hapa watu, ati waje washindane na mimi, hawa watu nitawaosha asubuhi na mapema,” amesema Ruto.

    Ameongeza kuwa: “Wale watu mmesikia mipango yao? Mmesikia ajenda yao? Mmesikia sera yao? Mmesikia maono yao? Oh, kumbe mnawajua? Wale majamaa hawana mpango… sera… ajenda… maono… hata akili hawana kabisa.”

    Sura mbili za siasa za Kenya

    Kauli ya Ruto imeongeza mjadala kuhusu sura inayochukua ushindani wa kisiasa nchini Kenya, hasa wakati wanasiasa wanapoanza kujenga hoja kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

    Mchambuzi wa masuala ya kisiasa, Profesa Mohammed Makame, amesema malumbano ya aina hiyo ni sehemu ya ushindani wa kisiasa katika mfumo wa vyama vingi, ambapo pande zinazoshindana hutumia hoja mbalimbali kujenga ushawishi kwa wananchi na kuimarisha nafasi zao kuelekea uchaguzi.

    Amesema malumbano hayo yanaweza kuwa na sura mbili; kwanza, yanaweza kutumiwa kuonesha uimara wa chama au kiongozi wa kisiasa na kutafuta uungwaji mkono wa wananchi ili kurejea madarakani.

    “Vilevile, yanaweza kujikita katika utekelezaji wa ilani na sera, ambapo kila upande hujaribu kuonesha kwa nini unastahili kupewa ridhaa ya wananchi,” amesema.

    Amesema vyama vya upinzani kwa kawaida hujikita katika kuonesha udhaifu wa chama kilichopo madarakani, ikiwamo kukosoa utekelezaji wa ilani na kuunganisha hoja hizo na hali halisi inayowakabili wananchi katika masuala ya kijamii na kiuchumi.

    “Kwa upande wa Rais Ruto, bila shaka ana nia ya kuendelea na kugombea, hivyo anapambana na vitu vyote viwili. Kwa wale wanaomuunga mkono, watakuwa wakilinda na kutetea yale aliyoyafanya na mabadiliko aliyoyaleta,” amesema.

    Amesema Ruto na wafuasi wake, pia, wanahitaji kulinda uimara wa chama chao na kujenga mtaji wa wanachama ambao ni muhimu katika uchaguzi mkuu, huku upande wa pili ukijikita katika kutafuta madaraka kwa kuonyesha mapungufu ya Serikali iliyopo.

    Makame amesema katika mazingira hayo, ukosoaji unaweza kuwa wa aina mbili, ikiwamo ule unaochambua kwa kina ukweli na matokeo ya utekelezaji wa Serikali, na ule wa kisiasa unaolenga kujenga uhalali wa kisiasa wa upinzani kwa kuwaaminisha wananchi kuwa Serikali iliyopo haijafanya vya kutosha.

    “Lakini pia kuna kukosoa political, kwa maana ya kutengeneza legitimacy (uhalali) ya upinzani kwamba aliyepo madarakani hakuweza kufanya kitu,” amesema.

    Amesema mazingira ya kisiasa Kenya yanaweza kuathiriwa na masuala ya kikanda na siasa za makabila, ambayo kwa muda mrefu yamekuwa sehemu ya mijadala ya kisiasa nchini humo.

    “Kauli zinazotolewa na Ruto zinaweza kutafsiriwa kama sehemu ya mkakati wa kujilinda kisiasa kwa kuonesha mambo ambayo Serikali yake imefanikiwa kufanya katika kipindi alichokuwa madarakani, hasa ikiwa ana mpango wa kuomba ridhaa ya wananchi kwa muhula mwingine.

    “Anapomwangalia aliyetoka madarakani, naye anamwangalia mpinzani kama ni mpinzani, kwa hiyo ruling party (chama tawala) inakuwa opposition party (chama cha upinzani),” amesema.

    Profesa Makame amesema hali hiyo inafanya hata chama kilicho madarakani kuendelea kumtazama mpinzani kama tishio linalopaswa kuzuiwa kupata nafasi ya kuingia madarakani, akibainisha kuwa kauli kama hizo zinaweza kuendelea kuongezeka kadiri uchaguzi wa 2027 unavyokaribia.

  • JKCI, CCBRT zapokea Sh200 milioni mbio za CRDB

    JKCI, CCBRT zapokea Sh200 milioni mbio za CRDB

    Dar es Salaam. Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Hospitali ya CCBRT zimepokea Sh200 milioni zilizotokana na mbio za hisani za CRDB Bank Marathon, fedha zinazolenga kuboresha huduma za afya na kuongeza upatikanaji wa matibabu kwa makundi yenye uhitaji.

    Katika hafla ilifanyika jana jijini Dar es Salaam, kila taasisi ilikabidhiwa Sh100 milioni, huku tukio hilo likiambatana na ujumbe wa kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi mara kwa mara na kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

    Mbio hizo zilihusisha washiriki wa kilomita tano, 10, 21 na 42 pamoja na mbio za baiskeli za kilomita 65, zikivutia maelfu ya wananchi kutoka makundi mbalimbali nchini.

    Mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, ambaye alisisitiza umuhimu wa kuendeleza shughuli zinazowakutanisha wananchi na kuimarisha afya zao ili waweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

    Hemed ambaye alimwakilisha waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba alisema ukiratibu Watanzania kufanya mazoezi unakuwa umeokoa fedha nyingi kwa sababu wagonjwa wengi wanaibiwa kwa mazoezi.

    “Kazi hii ambayo tumeifanya leo (jana) kuhakikisha Watanzania wamefanya mazoezi, tumeokoa fedha nyingi za Watanzania kwa sababu zaidi ya asilimia 40 hawakai ndani, wanatibiwa kisaikolojia tu kuwa wanatakiwa kufanya mazoezi,” alisema.

    Alisema uchumi wa Tanzania unategemea taasisi za fedha na CRDB imeonesha kwa vitendo na wanachangia mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

    “Kazi hii ambayo CRDB wameifanya inapaswa kuwa endelevu na inalindwa,” alisema Hemed huku akigusia ushiriki wa watu wengi kwenye mbio hizo ni ishara kwamba nchi ipo salama.

    Kwa upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk Juma Malik Akil, alisema Serikali itaendelea kuunga mkono mipango inayochangia ustawi wa jamii, akieleza kuwa mbio hizo zimekuwa chachu ya kuhamasisha mshikamano, afya na maendeleo ya wananchi.

    Naibu Waziri wa Afya, Dk Florence Samizi, akiambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Grace Magembe, walishiriki katika mbio hizo na kusisitiza kuwa afya kinga ndiyo msingi wa kupunguza mzigo wa magonjwa nchini.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk Abdulmajid Nsekela, alisema CRDB Bank Marathon imeendelea kuwa zaidi ya mashindano ya riadha, bali ni jukwaa linalounganisha michezo na dhamira ya kuleta mabadiliko yenye manufaa kwa jamii.

    Alisema kupitia mbio hizo, Benki ya CRDB imeendelea kutekeleza falsafa yake ya kurudisha kwa jamii kwa kusaidia sekta ya afya na makundi yenye uhitaji, huku kila mshiriki akiwa sehemu ya safari ya kubadilisha maisha ya Watanzania.

    “Safari ya CRDB Bank Marathon imeendelea kuonyesha kuwa michezo inaweza kuwa daraja la kuleta mabadiliko chanya katika jamii. Kila mwaka tumeshuhudia ongezeko la ushiriki na mchango mkubwa zaidi kwa sekta ya afya,” alisema.

    Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Foundation, Oswald Urassa, alimshukuru mgeni rasmi pamoja na washiriki na wadhamini wote kwa kuendelea kuiunga mkono mbio hiyo.

    Alisema bodi itaendelea kusimamia sera na miongozo itakayoiwezesha taasisi hiyo kuongeza ufanisi katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa jamii, hususan sekta ya afya.

    Kwa niaba ya wadhamini, Ofisa Mkuu wa Fedha wa Sanlam Allianz Tanzania, Samwel Mika, aliyemwakilisha Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, alisema wanafarijika kuwa sehemu ya safari ya CRDB Bank Marathon kutokana na mchango wake katika kugusa maisha ya wananchi.

    Aliahidi kuwa Sanlam Allianz Tanzania itaendelea kushirikiana na CRDB Bank Foundation kuhakikisha mbio hizo zinaendelea kuleta matokeo chanya kupitia miradi ya afya na maendeleo ya jamii.

    Mbali na kuchangisha fedha, mbio hizo zimeendelea kuwa jukwaa la kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kufanya mazoezi, kuzingatia lishe bora na kuchukua hatua za mapema katika kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.

    Wizara ya Afya ilieleza kuwa ushiriki wake katika mbio hizo unaendana na mkakati wa kuimarisha afya kinga na kuongeza ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya nchini.

  • Katoro: Mji wa fursa unaochanua kwa dhahabu, biashara na watu

    Katoro: Mji wa fursa unaochanua kwa dhahabu, biashara na watu

    Geita. Kuna miji ambayo huijui mpaka uambiwe, lakini kuna miji ambayo ukifika mara moja, unaelewa kwa nini watu wanaizungumzia. Katoro ni mmoja wapo.

    Mwezi uliopita, jina la mji huo lilivuka mipaka ya kawaida ya biashara na uchimbaji dhahabu na kuingia kwenye gumzo la kitaifa baada ya kufanyika kwa sherehe ya kifahari ya kumuaga Monalisa Buyamba, binti wa mfanyabiashara na mchimbaji dhahabu, Sylivester Buyamba, maarufu ‘GSM wa Katoro.’

    Helikopta iliyomfuata Monalisa nyumbani na kumpeleka kwenye ukumbi wa sherehe, pamoja na zawadi ya hundi ya Sh1.04 bilioni, vilifanya wengi waliokuwa hawaijui Katoro waanze kujiuliza: Katoro ni mji wa aina gani?

    Kwa nini watu wana pesa kiasi hicho? Na ni nini kinachoufanya mji huo uwe na mvuto mkubwa kiasi hiki? Wengine wanaita Kariakoo ya Geita.

    Jibu lake halipo kwenye harusi pekee, lipo kwenye dhahabu, samaki, biashara ya jumla, usafirishaji, kilimo, watu wanaohama kutoka maeneo mbalimbali na kasi ya mji unaokua kuliko miundombinu yake.

    Kwa mtu ambaye hajawahi kufika Katoro, mji huo unaweza kuonekana kama kituo kingine cha biashara Kanda ya Ziwa. Ukiingia unakuta ni mji wenye mchanganyiko wa shughuli na watu kutoka maeneo mbalimbali.

    Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro inaundwa na kata tatu za Nyamigota, Ludete na Katoro. Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, maeneo hayo yalikuwa na jumla ya wakazi 231,332.

    Hata hivyo, ongezeko la watu kutokana na kuzaliwa na uhamiaji kutoka maeneo mengine limeifanya idadi hiyo kutajwa kuwa imevuka watu 300,000.

    Katoro iko takribani kilomita 42 kutoka Geita mjini, safari inayoweza kuchukua dakika 30 hadi 40 kwa mujibu wa hali ya usafiri. Kutoka Mwanza ni karibu kilomita 167, Bukoba kilomita 258, Biharamulo kilomita 92, Chato kilomita 74 na Bukombe kilomita 103.

    Uwepo wa Uwanja wa Ndege wa Chato, uliopo takribani kilomita 61 kutoka Katoro, pamoja na Uwanja wa Ndege wa Mwanza, uliopo zaidi ya kilomita 170, nao umeongeza njia za kuufikia mji huo.

    Baada ya kuzinduliwa kwa Daraja la JP Magufuli katika eneo la Busisi, usafirishaji kwa barabara umeendelea kupata msukumo zaidi, hasa kwa biashara zinazounganisha Kanda ya Ziwa na maeneo ya Magharibi.

    Ukifika Katoro, baadhi ya mitaa utakayosikia ikitajwa mara kwa mara ni California, Kilimanjaro, Stamico, Mji Mwema, Mchongomani, Mtaa wa Afya, Merelani na Kilimahewa. Kinachovutia zaidi si majina ya mitaa pekee, ni kasi ya shughuli zilizopo.

    Asubuhi, wafanyabiashara wanafungua maduka. Sokoni, wanawake wanawahi mbogamboga, samaki, ndizi na nafaka. Magari yanaingia na kutoka, pikipiki zinabeba abiria na mizigo, na wafanyabiashara kutoka mikoa jirani wanafika kutafuta bidhaa za jumla.

    Katikati ya yote hayo, kuna dhahabu ambayo ni injini kubwa ya uchumi wa eneo hilo. Migodi inayopatikana katika maeneo yanayozunguka Katoro, ikiwamo Msasa, Buckreef, Nyarugusu, Nyaruyeye na Rwamugasa, imekuwa ikichochea mwingiliano wa watu na fedha.

    Ndiyo maana Katoro si tu mahali pa kuishi; kwa watu wengi, ni mahali pa kutafuta fursa. Mji huo umejijengea nafasi kama soko la bidhaa za jumla kwa wafanyabiashara kutoka Geita na mikoa jirani, ikiwamo Kagera na Kigoma.

    Katika eneo linalotambulika kama Soko la Kariakoo la Katoro, mfanyabiashara anaweza kupata simu, vifaa vya umeme, vifaa vya muziki, vifaa vya ushonaji, vitambaa, nguo na bidhaa nyingine za matumizi.

    Kwa upande wa chakula, Soko la Katoro-CCM ndilo moja ya kitovu kikubwa. Huko ndipo bidhaa kama nafaka, ndizi, viazi, mihogo, magimbi, matunda na samaki hupatikana.

    Katoro inasifika kwa kuwa na matawi ya benki zaidi ya matano, hali inayofanya uhakika wa usalama kifedha kuwa mkubwa.

    Uwepo wa vijiwe vya nyama choma, gym za mazoezi, sauna, supermarket, vimeutofautisha mji huo na maeneo mengine katika ukanda huo. Licha ya makao makuu ya mkoa huo kuwa Geita Mjini, Katoro ndiyo moja ya eneo lenye mwingiliano wa watu na biashara kuliko kwingineko.

    Sababu Katoro kuchangamka

    Beatrice John, mkazi wa Merelani na mfanyabiashara wa samaki katika Soko la Samaki Katoro-CCM, anasema uchimbaji wa madini una athari ya moja kwa moja kwenye biashara yake.

    Anaeleza fedha zinazopatikana migodini huingia kwenye mzunguko wa biashara mjini Katoro na kuufanya mji huo kuchangamka.

    “Wachimbaji wanapopata pesa kule, lazima huku Katoro pachangamke, kwa sababu kama samaki unauza Sh8,000, unaweza kumuuzia mteja kwa Sh9,000 au Sh10,000 na hakatai, yeye anafika analipa,” anasema.

    David Charles, mkazi wa Katoro anayefanya biashara ya nafaka na samaki kwa zaidi ya miaka 20, anasema samaki ni moja ya biashara zinazozungusha fedha kwa kasi mjini hapo.

    Anasema kila asubuhi hupokea magari matatu hadi matano pamoja na zaidi ya pikipiki 100 zinazoleta samaki kutoka maeneo ya ziwani. Kufikia saa tano asubuhi, anasema, mzigo mkubwa huwa tayari umenunuliwa na wafanyabiashara husubiri awamu nyingine inayofika mchana na jioni.

    “Biashara ya samaki inalipa kuliko ujasiriamali mwingine ulioko hapa. Hata mwenye duka, mimi ninayefanya ujasiriamali wa samaki, ananifuata mimi, kuna uzalishaji sana kwenye samaki,” anaeleza.

    Kwa mtazamo wake, ukiondoa dhahabu yenye thamani kubwa, samaki ni miongoni mwa shughuli zinazoweka fedha kwenye mifuko ya watu wengi kwa wakati mmoja, lakini biashara hiyo ina misimu yake. Kipindi cha kiangazi, upatikanaji wa samaki huwa mgumu zaidi ikilinganishwa na msimu wa masika.

    Hata baiskeli inazungusha uchumi wa Katoro

    Mkazi wa Rumasa, Matumbate Emmanuel, anaendesha baiskeli ya abiria, maarufu ‘daladala’. Kazi hiyo, anasema, imemsaidia kumudu maisha ya familia yake yenye watoto saba na mke, na kwa siku anaweza kupata kati ya Sh20,000 na Sh25,000.

    Mkazi wa Kilimahewa, Abel Kasanda, ni mmoja wa watu ambao hadithi ya Katoro imegusa maisha yao moja kwa moja. Akiuza vyombo vya kupikia kwa miaka mitatu, anasema aliingia kwenye biashara akiwa hana mtaji mkubwa wala mali.

    “Nilianza nikiwa mkono mtupu kwenye hii biashara ya umachinga wa vyombo, sikuwa na nyumba wala kiwanja, lakini kwa sasa namshukuru Mungu nimeshanunua kiwanja na kuanza ujenzi, boma lipo, bado kuezeka tu,” anasema.

    Kasanda anasema msimu mzuri wa biashara yake ni kiangazi, wakati baadhi ya wateja kutoka nje ya mji wanapokuwa wamevuna na kuuza mazao yao.

    Katoro, mji wa wahamiaji na tamaduni tofauti

    Katoro si mji wa kabila moja. Wasukuma, Wasumbwa na Wazinza ni miongoni mwa jamii za mwanzo kuishi katika eneo hilo, lakini kadiri biashara, uchimbaji na usafiri vilivyokua, watu kutoka maeneo mbalimbali wameendelea kuingia.

    Wachaga, Wajita, Waha, Wakurya, Wahaya na Wajaruwo ni miongoni mwa jamii zinazopatikana kwa wingi.

    Hii ndiyo sababu unaweza kuingia kwenye biashara moja ukakutana na mtu kutoka Kagera, mwingine Kigoma, mwingine Mwanza, huku anayekuuzia bidhaa akiwa mwenyeji wa Geita.

    Ukuaji wa Katoro hauonekani kwenye maduka pekee, unaonekana pia kwenye huduma za afya.

    Inakadiriwa kuwa kati ya watoto 900 na 1,000 huzaliwa kila mwezi, huku Kituo cha Afya Katoro kikitajwa kuhudumia wastani wa wanawake 33 wanaojifungua kwa siku.

    Ongezeko hilo la watu limeongeza mahitaji ya huduma za kijamii na kuufanya mji huo uwe na hospitali yenye hadhi ya wilaya iliyopo Mtaa wa Afya, pamoja na kituo cha afya cha Serikali Katoro-CCM na vituo binafsi.

    Usalama ulivyofungua biashara

    Mji wenye watu wengi na biashara nyingi unahitaji usalama. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Safia Jongo, anasema usalama wa Geita umeimarika kutokana na ushiriki wa wananchi kupitia mfumo wa Polisi Jamii.

    “Tunazifanyia kazi taarifa kutoka kwa jamii na wahalifu sugu waliokuwa wanasumbua ndani ya mkoa wetu, hatua mbalimbali za kisheria zimechukuliwa na matokeo yake ndiyo haya. Mkoa wa Geita tunaendelea kula bata saa 24, lakini wananchi wanafanya shughuli zao za kiuchumi,” anasema.

    Kasi ya ujenzi holela na ongezeko la watu limefanya baadhi ya maeneo ya Katoro kuwa na changamoto ya barabara na mitaro. Baadhi ya barabara huwa ngumu kupitika, huku katika maeneo mengine wananchi wakilalamikiwa kwa kuziba mitaro.

    Changamoto hiyo huwa kubwa zaidi wakati wa dharura, hasa pale moto au tukio jingine linapotokea na magari yanahitaji kufika kwa haraka.

    Barabara ya Katoro-Bukombe, yenye urefu wa zaidi ya kilomita 58, nayo imekuwa kilio cha wafanyabiashara na wachuuzi.

    Kwa mujibu wa Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Geita, Hosea Machaka, anasema ujenzi wa barabara hiyo wenye thamani ya Sh10.9 bilioni ulikuwa umefikia asilimia 48 wakati wa taarifa hii.

    Kukamilika kwake kunatarajiwa kurahisisha usafirishaji na kuongeza zaidi mwingiliano wa kibiashara kati ya maeneo hayo.

  • Ujumbe muhimu kwa malezi ya mtoto

    Ujumbe muhimu kwa malezi ya mtoto

    Dar es Salaam. Mtoto anayekulia katika mazingira yenye kila kitu, akipewa simu ya kisasa, kusoma shule nzuri na kushiriki burudani mbalimbali, bado anaweza kukosa maarifa muhimu ya maisha ikiwa hajawahi kukutana na mazingira yanayomsaidia kuelewa dunia inayomzunguka.

    Wataalamu wa saikolojia wanaeleza kuwa kabla mtoto hajafikisha miaka 13, mzazi ana nafasi kubwa ya kumjengea uwezo wa kufikiri, kuuliza maswali, kufanya uamuzi, kuwa na huruma na kuelewa tofauti za maisha kupitia uzoefu wa moja kwa moja.

    Badala ya kusubiri mtoto awe kijana ndipo aanze kujifunza kuhusu fedha, kazi, historia, utamaduni na maisha ya watu wengine, wazazi wanashauriwa kutumia miaka hiyo kumpeleka katika maeneo mbalimbali.

    Maktaba inaweza kuwa lango la mtoto kuelekea dunia ambayo hawezi kuiona katika mazingira yake ya kawaida.

    Kumpeleka maktaba humfundisha kuwa maarifa hayapatikani kupitia simu au mwalimu pekee, bali pia kupitia vitabu na kujisomea.

    Makumbusho nayo humkutanisha na historia, sanaa, utamaduni na simulizi za jamii mbalimbali.

    Akizungumza na Mwananchi, mwanasaikolojia Amina Msuya anasema uzoefu huo hujenga udadisi na uwezo wa mtoto kuuliza maswali badala ya kukubali kila jambo bila kutafakari.

    Shamba, soko na supermarket

    Mzazi anashauriwa kumpeleka mtoto shambani ili aone chakula kinapotoka kabla hakijafika mezani.

    “Aone mbegu ikipandwa, mazao yakitunzwa na kuvunwa. Hii humsaidia kuthamini kazi na chakula badala ya kuona kila kitu kinapatikana kwa urahisi,” anasema Amina.

    Katika soko, mtoto anaweza kujifunza biashara, mawasiliano na namna watu wanavyotafuta kipato, huku supermarket ikiwa darasa la fedha.

    Mtaalamu wa uchumi, Jesca Magolanga, anasema mzazi anaweza kumpa mtoto kiasi maalumu cha fedha na kumruhusu achague bidhaa, hatua inayomsaidia kujifunza bajeti, kufanya uchaguzi na kujizuia kununua vitu vinavyopita uwezo wake.

    Ziara ya benki inaweza kuwa mwanzo wa mazungumzo kuhusu kuweka akiba, matumizi na kupanga fedha.

    Kadhalika, mtoto akipelekwa mahali mzazi au ndugu anapofanya kazi anaweza kuona uhusiano kati ya elimu, ujuzi, kazi na kipato.

    “Mtoto anapopewa fursa ya kuona watu wakifanya kazi, huanza kuelewa mapema kuwa mafanikio yanahitaji juhudi, nidhamu na uwajibikaji,” anasema Jesca.

    Hospitali, zimamoto na polisi

    Hospitali inaweza kumfundisha mtoto umuhimu wa afya, huruma na kuwathamini watu wanaowahudumia wengine.

    Kituo cha zimamoto kinampa nafasi ya kuona watu wanaokabiliana na hatari kwa ajili ya kuwaokoa wengine, huku kituo cha polisi kikimsaidia kuelewa usalama, sheria, wajibu wa raia na kujiepusha na vitendo vya uhalifu.

    Hata hivyo, wataalamu wanashauri ziara hizo zifuatane na maelezo yanayoendana na umri wa mtoto ili zisijenge hofu, bali uelewa.

    Mtoto anaweza kujifunza kuhusu imani, maadili, huduma na mshikamano kupitia ziara katika nyumba ya ibada.

    Akizungumzia hilo, Sheikh Khamis Mataka anasema ni muhimu kwa wazazi kuwapeleka watoto kwenye nyumba za ibada ili wajifunze matendo mema na kuwa na hofu ya Mungu.

    Katika kituo cha jamii au taasisi inayosaidia watu wenye mahitaji, mtoto anaweza kuona kuwa si kila mtu anakulia katika mazingira yanayofanana.

    “Tuwapeleke huko wakaone maisha yalivyo, lakini tusiwafundishe kuwadharau walio katika hali duni. Lengo liwe kumjengea huruma na kutambua kuwa utu haupimwi kwa mali,” anasema Sheikh Mataka.

    Sanaa, michezo na mazingira

    Kumpeleka mtoto kwenye ukumbi wa sanaa humsaidia kuona ubunifu, muziki, uigizaji na usimulizi wa hadithi kwa vitendo.

    Tamasha la utamaduni humfanya aone kuwa utamaduni si jambo la kusoma kwenye kitabu pekee, wakati michezo humfundisha kazi ya pamoja, nidhamu, ushindani na kuheshimu mpinzani.

    Aidha, ufukwe, mlima, msitu au hifadhi humsaidia mtoto kuondoka kwenye skrini na kukutana na mazingira ya asili.

    Wataalamu wa saikolojia wanaeleza kuwa mazingira hayo yanaweza kuchochea udadisi na ubunifu kwa sababu mtoto hujifunza kupitia kuona, kugusa na kuchunguza.

    Chuo kikuu, maeneo ya kihistoria

    Mzazi asisubiri mtoto amalize sekondari ndipo aanze kuzungumza naye kuhusu chuo kikuu na taaluma.

    Ziara ya chuo kikuu inaweza kumsaidia kuanza kuona uwezekano wa maisha yake ya baadaye na kutambua taaluma mbalimbali.

    Vilevile, kumpeleka kwenye eneo la kihistoria na kumsimulia kilichotokea hapo hufanya historia iwe uzoefu halisi.

    Makaburi na historia ya familia

    Makaburi yanaweza kuwa sehemu ya mazungumzo yanayolingana na umri kuhusu maisha, kifo, kumbukumbu na urithi. Hata hivyo, mazungumzo hayo yasitumike kumtisha mtoto.

    Mzazi pia anaweza kumpeleka katika mji alikokulia, nyumbani kwa babu na bibi, biashara ya familia au sehemu ambako wazazi walikulia.

    Hii humsaidia mtoto kuelewa kuwa maisha yake ni sehemu ya simulizi kubwa lililotangulia kuzaliwa kwake.

    Moja ya safari muhimu zaidi inaweza kuwa kwenda sehemu ambayo mtoto hajawahi kufika. Mji mwingine, mazingira tofauti au jamii yenye utamaduni mwingine vinaweza kumlazimisha kuangalia, kuuliza, kuzoea na kujifunza.

    Malezi bora si kumkinga mtoto dhidi ya dunia kila wakati, bali kumtayarisha kuikabili dunia kwa uelewa.

    Kabla hajafikisha miaka 13, mtoto anaweza kuwa amejifunza kuhusu fedha, kazi, historia, utamaduni, mazingira, huruma, afya, imani, huduma kwa jamii na thamani ya maisha ikiwa mzazi atampa nafasi ya kujifunza nje ya darasa.

  • Miaka 10 ya kusubiri mradi, wananchi wabebeshwa zigo la gharama – 1

    Miaka 10 ya kusubiri mradi, wananchi wabebeshwa zigo la gharama – 1

    Dar es Salaam. Wakati Serikali ikiendelea kutenga mabilioni ya fedha ili kukamilisha Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida, wananchi wameendelea kubeba mzigo wa gharama za matibabu kwa kulazimika kuuza mifugo, mashamba na mali nyingine kugharimia safari, malazi na matibabu nje ya mkoa.

    Hali hiyo inatokana na kutokamilika kwa jengo la ghorofa tatu la hospitali hiyo, lililoanza kujengwa mwaka wa fedha 2016/17. Kwa mujibu wa mkataba, mradi huo ulitakiwa kuwa umekamilika Juni 2019.

    Mamia ya wagonjwa wanalazimika kufunga safari kwenda Hospitali ya Benjamin Mkapa iliyopo mkoani Dodoma, Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando (Mwanza), Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini-KCMC (Kilimanjaro) na Hospitali ya Taifa Muhimbili (Dar es Salaam) kufuata huduma za kibingwa.

    Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Mwananchi, safari hizo za kusaka huduma, malazi na gharama za matibabu zimesababisha baadhi ya familia kuwa maskini na pia kuhatarisha maisha ya wapendwa wao.

    Christina Hamis (69), mkazi wa kijiji cha Muhintiri, Ikungi mkoani Singida, anasema alilazimika kuhamia Dodoma, alikopanga chumba kwa zaidi ya miaka miwili tangu mwaka 2024, ili mtoto wake apate huduma ya kusafisha damu (dialisisi).

    Anasema aliuza ng’ombe, shamba na kibanda chake ili kugharimia matibabu, usafiri na malazi.

    “Niliuza kila nilichokuwa nacho. Mwisho nilishindwa kuendelea na matibabu kwa sababu sikuwa na uwezo tena,” anasimulia.

    Anasema iwapo huduma zingepatikana kwa wakati huo, mtoto wake angeweza kugundulika tatizo lake mapema na kupata matibabu kabla hali haijawa mbaya. Kijana wake alifariki dunia Mei 16, 2026, baada ya kuishiwa fedha za dialisisi.

    Wakati Hamis akieleza hayo, tayari huduma ya dialisisi imeanza kupatikana katika hospitali hiyo kuanzia Julai 2026.

    “Tunateseka sana. Mgonjwa akihitaji daktari bingwa wa magonjwa ya moyo, figo au uchunguzi wa vipimo vikubwa, mara nyingi tunaambiwa twende Benjamin Mkapa Dodoma, KCMC, Bugando au Muhimbili. Safari ni ndefu na gharama ni kubwa kiasi kwamba baadhi ya wagonjwa wanashindwa hata kufika,” anasema Hamisi Mussa, mkazi wa Manispaa ya Singida.

    Kwa upande wake, mkazi wa Ikungi, Anna Mghamba, anasema: “Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ilitakiwa kutupunguzia adha ya kusafiri mikoa mingine, lakini bado wagonjwa wengi wanapewa rufaa. Familia zinauza mifugo na mali nyingine ili kumudu usafiri, malazi na matibabu.”

    Kwa mujibu wa mkazi wa Iramba, Paulo Mwalimu, kuna wagonjwa wanaohatarishiwa maisha kwa kusubiri rufaa au fedha za kwenda hospitali nyingine.

    “Tunaiomba Serikali ikamilishe miundombinu na kuajiri madaktari bingwa wa kutosha ili wananchi wa Singida wapate huduma karibu na makazi yao badala ya kutumia siku nzima njiani kwenda kutafuta matibabu,” anasema.

    Mbunge wa Singida Mjini (CCM), Yagi Kiaratu, anasema huduma za kibingwa ni changamoto ya muda mrefu na imekuwa mzigo mkubwa kwa wananchi wa Singida na mikoa jirani.

    Anasema changamoto hiyo ilichochea juhudi za kuanzishwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, huku wazo la ujenzi likiasisiwa mwaka 2015 na Dk Parseko Kone, aliyekuwa mkuu wa Mkoa wa Singida wakati huo.

    “Pamoja na kuanza ujenzi wa baadhi ya majengo muhimu, mradi ulipitia vipindi vya kusuasua kabla ya Serikali kuhuisha utekelezaji wake kupitia fedha za mradi wa Uviko-19,” anasema Kiaratu, aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Singida na diwani wa Majengo (2020–2025) kabla ya kuchaguliwa kuwa mbunge.

    Kiaratu anasema kuchelewa kukamilika kwa miundombinu hiyo kuliwalazimu wagonjwa wengi kusafiri umbali mrefu kwenda kutafuta huduma katika hospitali za Dodoma, Makiungu, Bugando na Muhimbili, jambo lililowaongezea gharama za matibabu, usafiri na malazi.

    Anasema hali hiyo ilikuwa ngumu zaidi kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za mara kwa mara, ikiwamo dialisisi.

    Anaeleza kuanza kwa huduma hiyo Singida kumepunguza kwa kiasi kikubwa adha kwa wagonjwa na familia zao.

    Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida, Dk Munaji Kamtande, anasema licha ya kutokamilika kwa ujenzi wa majengo hayo, hospitali tayari imeongeza huduma za kibingwa, zikiwamo za upasuaji wa mifupa, upasuaji wa ubongo, upasuaji wa mfumo wa mkojo kwa wanaume, maabara za kisasa na CT Scan.

    Anasema huduma za dialisisi zimeanza kutolewa Julai 2026, hivyo wagonjwa wengi hawatalazimika kusafiri hadi Dodoma kwa ajili ya matibabu hayo.

    Hata hivyo, anakiri kuwa baadhi ya huduma, ikiwamo MRI na matibabu maalumu ya saratani, bado zinahitaji wagonjwa kupewa rufaa kwenda hospitali za juu zaidi.

    Anasema kukamilika kwa jengo jipya kutapanua uwezo wa hospitali kutoa huduma zaidi za kibingwa na kupunguza kwa kiasi kikubwa rufaa zinazotolewa nje ya mkoa.

    Hospitali hiyo ikikamilika, inatarajiwa kuwa na wodi za watoto, wanawake na magonjwa ya ndani, pamoja na ICU, EMD, vyumba vya upasuaji, maabara za kisasa na huduma nyingine za kibingwa. Huduma hizo zinatarajiwa kupunguza utegemezi wa wakazi wa Kanda ya Kati kwa hospitali za Dodoma, Bugando na Muhimbili.

    Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Jessica Lebba, anasema ujenzi umekuwa ukitekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha serikalini.

    Anasema mradi kwa sasa unatekelezwa katika awamu ya tatu, huku uongozi wa mkoa na hospitali ukiendelea kufuatilia maendeleo yake ili kuhakikisha unakamilika kwa ubora unaotakiwa.

    “Kukamilika kwa mradi huu kutaimarisha kwa kiasi kikubwa huduma za kibingwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida na kupunguza rufaa zinazotolewa sasa kwenda hospitali nyingine,” anasema.

    Dk Lebba anasema kwa sasa hospitali inatoa zaidi ya huduma 10 za kibingwa, lakini baada ya jengo kukamilika, inatarajiwa kufikia lengo la kutoa huduma zote 17 za kibingwa na kuwa kituo kikubwa cha utoaji wa huduma hizo kwa wakazi wa Kanda ya Kati.

    Athari za ucheleweshaji wa miradi

    Daktari bingwa wa magonjwa ya upasuaji, Mugisha Nkoronko, anasema huduma za afya zinapokuwa mbali na wananchi huleta adha na gharama kubwa, huku baadhi ya wagonjwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta matibabu ambayo wangepaswa kuyapata karibu na maeneo wanayoishi.

    Vilevile, anasema huongeza hatari kwa wagonjwa, hasa wanaohitaji huduma za haraka na za kibingwa.

    Dk Nkoronko anasema uwekezaji katika vituo vya afya ni jambo muhimu kwa sababu unasaidia kupunguza umbali ambao wananchi hulazimika kusafiri wanapohitaji huduma.

    Anasema uwekezaji haupaswi kuishia kwenye ujenzi wa majengo pekee, bali unatakiwa kwenda sambamba na upatikanaji wa vifaa tiba na rasilimali watu wa kutosha katika maeneo ambako wananchi wanapatikana.

    Ni mtazamo wake kuwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida inapaswa kuimarishwa ili kutoa huduma zinazohitajika na kupunguza mzigo wa wagonjwa wanaolazimika kwenda mikoa mingine kupata huduma za kibingwa.

  • Wajenzi wanavyokiuka vibali vya ujenzi, hatari kwa watumiaji

    Wajenzi wanavyokiuka vibali vya ujenzi, hatari kwa watumiaji

    Dar es Salaam. Baadhi ya wamiliki wa majengo jijini Dar es Salaam wamekuwa wakibadilisha mipango ya ujenzi baada ya kupata vibali, ikiwamo kuongeza idadi ya ghorofa, hali ambayo wataalamu wanaonya inaweza kuathiri usalama wa majengo na watumiaji.

    Kumbukumbu mbaya ni Novemba 16, 2024, ambapo jengo liliporomoka Mtaa wa Mchikichi na Congo, Kariakoo, Dar es Salaam, na kusababisha vifo vya watu 20, huku zaidi ya 50 wakiokolewa.

    Tukio kama hilo lilitokea Machi 29, 2013, Mtaa wa Indira Gandhi, Posta jijini Dar es Salaam, ambapo jengo la ghorofa 16 liliporomoka, ambalo liliombewa kibali cha ghorofa 10. Kuporomoka huko kulisababisha vifo vya watu zaidi ya 15 na kujeruhi wengine.

    Aliyekuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Ilala, Kheri Kessy, alisema mwaka 2007 walitoa kibali cha ujenzi wa ghorofa 10 kwa jengo hilo la Posta, ambazo zilikuwa zinafuatiliwa na mkaguzi hadi zilipofikia mwisho, hivyo uongezekaji wa ghorofa sita hawakuutambua.

    Novemba 2025, Ofisa wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, aliyeomba jina lake lisitajwe, aliliambia Mwananchi mamlaka hiyo hutoa vibali kwa kuzingatia ramani na michoro inayowasilishwa na mwombaji.

    Hata hivyo, alisema baadhi ya wamiliki hubadilisha mipango wanapoanza ujenzi na kuongeza ghorofa tofauti na walizoomba na kupewa kibali.

    Alitoa mfano wa jengo moja eneo la Kariakoo, ambalo mmiliki wake aliomba kibali cha kujenga ghorofa tano, lakini wakati wa ujenzi akaongeza hadi ghorofa 10.

    “Tumewahi kumpiga faini mmiliki mmoja wa jengo Kariakoo baada ya kubaini aliomba kibali cha ghorofa tano, lakini akajenga ghorofa 10,” alisema ofisa huyo alipozungumza na Mwananchi ilipokuwa ikiandaa habari maalumu kuhusu matumizi ya majengo ya Kariakoo yasiyokamilika.

    Hoja hiyo inaakisi kauli ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC), Albert Chalamila, ya Agosti 6, 2026, kueleza kubaini ukiukaji wa masharti ya ujenzi wakati wa ukaguzi.

    Chalamila alisema kuna majengo ambayo vibali vyake vilitolewa kwa idadi ndogo ya ghorofa, lakini yalipofikiwa katika maeneo ya ujenzi yalikuwa yamejengwa zaidi ya idadi iliyoidhinishwa.

    Katika mfano alioutoa, alisema jengo moja lilipewa kibali cha ghorofa sita, lakini lilikuwa limejengwa hadi ghorofa 13.

    Kutokana na hali hiyo, aliamuru mmiliki na mjenzi wakamatwe, huku uchunguzi wa kitaalamu ukiendelea kubaini kama msingi wa jengo hilo ulikuwa umeandaliwa kuhimili ghorofa hizo.

    Itakumbukwa, baada ya jengo la Kariakoo kuporomoka na kuua watu 20, Rais Samia Suluhu Hassan, alipotembelea eneo la tukio saa chache baada ya kuwasili nchini akitokea Brazil, alisema Serikali haitasita kubomoa majengo yote ya Kariakoo iwapo tume iliyoundwa kuchunguza usalama wake itashauri ifanyike hivyo.

    Sambamba na hilo, mkuu huyo wa nchi aliwasihi watendaji wa Serikali kuwajibika kwa nafasi zao, hasa katika mchakato wa utoaji vibali vya ujenzi, akitaka visimamiwe.

    Rais aliagiza iundwe tume kuchunguza majengo yote, na tayari waziri mkuu wa wakati huo, Kassim Majaliwa, ameunda ikiwa na wajumbe 19, akibainisha matokeo yatakayopatikana yatawekwa wazi kwa wananchi.

    Pamoja na kuwekwa wazi, alieleza iwapo tume hiyo itashauri majengo yote sokoni hapo yavunjwe, hatasita kufanya hivyo. Pia, Rais Samia alisema anatambua uwepo wa ripoti za tume mbalimbali, ikiwemo ya mwaka 2013, akisema uchunguzi unaofanywa utazingatia pia mapendekezo ya tume hiyo.

    Mpaka sasa, ripoti ya tume hiyo ya wajumbe 19 haifahamiki kama ilishamaliza kazi na, kama imemaliza, ilibaini kitu gani.

    Kifungu cha 33 cha Sheria ya Mipango Miji ya mwaka 2007 kinahusu hitaji la kupata kibali cha ujenzi kutoka mamlaka husika, huku Kifungu cha 36 kikihusu kumbukumbu za maombi na vibali vya ujenzi.

    Kanuni za mwaka 2018 zinaweka utaratibu wa udhibiti na ukaguzi wa majengo, hivyo mwenye kibali cha kujenga idadi ya ghorofa husika hawezi kuongeza ghorofa nyingine tofauti na mpango ulioidhinishwa bila kufuata utaratibu wa kufanya mabadiliko na kupata idhini inayotakiwa.

    Aidha, Kanuni ya 34 inaweka masharti kuhusu ukaguzi wa jengo lililokamilika na utoaji wa cheti cha matumizi, hatua ambayo inaweza kubaini tofauti kati ya ramani iliyoidhinishwa na jengo lililojengwa.

    Wakili Fatma Kibakala anasema kibali hutolewa kwa kuzingatia nyaraka na michoro iliyowasilishwa, hivyo mwenye jengo anapaswa kujenga kulingana na kilichoidhinishwa.

    “Ukipata kibali kwa msingi wa ramani fulani, wajibu wako ni kujenga kwa kuzingatia kile kilichoidhinishwa. Kama unataka kubadilisha, unatakiwa kuwasilisha mabadiliko kwa mamlaka husika na kupata idhini inayotakiwa,” anasema Fatma.

    Anasema faini pekee haiwezi kuondoa wajibu wa kuhakikisha jengo ni salama.

    “Adhabu ya ukiukaji wa masharti ya kibali ni suala moja, lakini usalama wa jengo ni suala jingine. Mmiliki anapaswa kuhakikisha mabadiliko yote yanafuata taratibu na jengo lina uwezo wa kutumika kwa usalama,” anasema.

    Mtaalamu wa ujenzi, Dorcas Msabila, anasema kuongeza ghorofa si sawa na kuongeza vyumba ndani ya nyumba kwa sababu kila sakafu mpya huongeza mzigo unaobebwa na msingi, nguzo na mihimili.

    Anasema wakati wa usanifu wa jengo, mhandisi hufanya hesabu kulingana na mzigo ambao mfumo wa jengo unatarajiwa kubeba.

    “Ukiwa umebuni jengo kwa idadi fulani ya ghorofa, hesabu za kihandisi zinazingatia mzigo wa jengo hilo. Ukiongeza ghorofa bila kufanya tathmini na usanifu mpya, huwezi kusema moja kwa moja kwamba jengo lina uwezo wa kubeba mzigo huo,” anasema Msabila.

    Msabila anasema kabla ya kuongeza sakafu, mhandisi anapaswa kuchunguza uwezo wa msingi, nguzo, mihimili na ubora wa vifaa vilivyotumika.

    Anasema tathmini inaweza kuonesha kama jengo linaweza kubeba mzigo mpya au linahitaji uimarishaji wa kimuundo kabla ya kuendelea kutumika.

    Mtaalamu wa ramani, Herison Amani, naamani ndiyo msingi wa kuhakikisha jengo linajengwa kwa kuzingatia mpango uliothibitishwa.

    “Ukiwa umeidhinishiwa ghorofa nne, halafu ukaongeza nyingine bila kurekebisha ramani na kupata idhini, unakuwa umeondoka kwenye mpango uliokuwa umeidhinishwa,” anasema Amani.

    Anasema mabadiliko hayo yanapaswa kuonyeshwa kwenye michoro mipya na kuchunguzwa na wataalamu wa usanifu na uhandisi kabla ya ujenzi kuendelea, kwani ubadilishwaji wa idadi ya ghorofa si mabadiliko madogo; ni lazima mfumo mzima wa jengo uangaliwe upya.

    Mkandarasi wa majengo Kariakoo, Emmanuel Kambi, anasema hali hiyo inachangiwa na mmiliki baada ya kuona mfuko wake unaweza kuongeza idadi ya majengo tofauti na ramani ya awali.

    “Tunajua ni kosa kuongeza kitu chochote wakati wa ujenzi tofauti na maelekezo ya ramani, lakini tunafanya kazi kwa matakwa ya mmiliki, kwani kazi yetu ni kutekeleza kile anachohitaji mteja kwa wakati huo,” anasema Kambi.

    Anasema kingine kinachochangia ni kutokuwepo kwa ukaguzi wa mara kwa mara, kwani yapo majengo yanakaguliwa mtu akishamaliza hatua fulani, kisha wanakuja kuweka alama za kusimamisha au kubomoa.

    Serikali imeonya wamiliki na waendelezaji wa majengo wanaojenga kinyume na michoro na vibali vilivyoidhinishwa, ikisema hatua hiyo ni ukiukaji wa sheria na inaweza kuhatarisha usalama wa majengo.

    Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Dk Festo Dugange, anasema kabla ya kuanza ujenzi, mjenzi anatakiwa kufuata taratibu, ikiwamo kupata michoro ya jengo, kuidhinishwa na mamlaka husika na kupata kibali cha ujenzi.

    Anasema kibali huzingatia mambo mbalimbali, ikiwamo aina ya jengo, eneo linapojengwa, ukubwa wake, idadi ya ghorofa, aina ya udongo na, kwa baadhi ya miradi, tathmini ya athari za mazingira.

    Dk Dugange anasema mjenzi anapaswa kujenga kulingana na kibali alichopewa na hawezi kuomba ghorofa mbili, kisha kuongeza ghorofa nyingine bila kupata idhini ya mamlaka husika.

    “Ukiomba kibali cha ghorofa mbili, huwezi kujenga ghorofa tatu. Hilo ni kosa kisheria,” anasema.

    Anasema Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masharti ya vibali vya ujenzi, huku wataalamu wa Serikali wakifanya ukaguzi katika maeneo mbalimbali kuhakikisha ujenzi unazingatia sheria, ubora na viwango vinavyotakiwa.

    Anasema ikibainika jengo linajengwa kinyume na kibali, hatua huchukuliwa, ikiwamo kusimamisha ujenzi na kuchukua hatua za kisheria kulingana na aina ya ukiukwaji.

    Pia, anasisitiza umuhimu wa serikali za mitaa kushiriki katika ufuatiliaji wa ujenzi unaoendelea katika maeneo yao.

    Anasema viongozi na watendaji wa serikali za mitaa wana wajibu wa kufuatilia shughuli za ujenzi na kutoa taarifa pale wanapoona ukiukwaji wa taratibu.

    Anasema ufuatiliaji hufanyika hatua kwa hatua ili kuhakikisha kile kilichoombwa na kuidhinishwa ndicho kinachojengwa. 

  • Jamhuri yafunga ushahidi kesi ya Lissu

    Jamhuri yafunga ushahidi kesi ya Lissu

    Dar es Salaam. Jamhuri imefunga ushahidi wake katika kesi ya uhaini  inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tundu Lissu, 

    Jamhuri imefunga ushahidi huo leo Jumatatu Agosti 17, 2026 baada ya kuwaita mashahidi 17 kati ya 30 waliokuwa wameorodheshwa.

    Katika kesi hiyo Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini kinyume na kifungu cha 39(2) (d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, linalotokana na maneno aliyoyatamka kuhusiana na kusudio la kuzuia kufanyika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

    Anadaiwa kuwa Aprili 3, 2025, jijini Dar es Salaam, akiwa raia wa Tanzania, kwa nia ya uchochezi alishawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, kwa kutamka na kuandika maneno ya kumshinikiza kiongozi mkuu wa Serikali ya Tanzania, kuwa:-

    “Wakisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli…, kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi, tutahamasisha uasi, hivyo ndivyo namna ya kupata mabadiliko… kwa hiyo tunaenda kikinukisha…, sana sana huu uchaguzi tutaenda kuuvuruga kwelikweli… tunaenda kukinukisha vibaya sana…”

    Kesi hiyo inasikilizwa na Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam na jopo la majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, Jaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde, ilipangwa kuendelea leo kwa ushahidi wa upande wa Jamhuri.

    Hata hivyo baada ya kesi kuitwa Jamhuri kupitia mwendesha mashtaka Wakili wa Serikali  Mkuu Ajuaye Nzegeli ameieleza Mahakama kuwa baada ya kupitia ushahidi uliokwishawasilishwa na kuangalia ushahidi wa mashahidi waliosalia wameona ushahidi waliokwishawasilishwa unatosheleza.

    “Hivyo tunapenda kuitaarifu Mahakama hii tukufu kuwa upande wa Jamhuri unafunga ushahidi wake kwa mashahidi 17”, amesema Wakili Nzegeli.

    Baada ya Jamhuri kufunga ushahidi wake sasa kesi imeingia katika hatua ya pili ambapo pande zote zinawasilisha hoja kuishawishi mahakama kama mshtakiwa kwa ushahidi huo ana kesi ya kujibu au la.

    Kwa sasa ameanza mshtakiwa Lissu kuwasilisha hoja zake kuishawishi Mahakama kuwa upande wa mashtaka umeshindwa kuonesha kuwa kuna kesi ya kumfanya ajitetee, kabla ya upande wa mashtaka kujibu hoja hizo kuionesha Mahakama kuwa imeweza kujenga kesi kiasi cha kumlazimu mshtakiwa kujitetea kabla ya kutoa hukumu.

  • Lissu alivyoishawishi Mahakama hana kesi ya kujibu, aomba fidia

    Lissu alivyoishawishi Mahakama hana kesi ya kujibu, aomba fidia

    Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, amewasilisha hoja za kisheria akiishawishi Mahakama Kuu kuwa hana kesi ya kujibu katika shtaka la uhaini linalomkabili, akiiomba imuachilie huru na iamuru alipwe fidia.

    Lissu amewasilisha hoja hizo leo Jumatatu, Agosti 17, 2026, baada ya upande wa Jamhuri kufunga ushahidi wake katika kesi hiyo.

    Jamhuri imefunga ushahidi baada ya kuwaita mashahidi 17 kati ya 30 waliokuwa wameorodheshwa kutoa ushahidi.

    Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini kinyume na kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, linalotokana na maneno aliyodaiwa kuyatamka kuhusu kusudio la kuzuia Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

    Anadaiwa kuwa Aprili 3, 2025, jijini Dar es Salaam, akiwa raia wa Tanzania, kwa nia ya uchochezi alishawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa 2025, kwa kutamka na kuandika maneno ya kumshinikiza kiongozi mkuu wa Serikali, akisema: “Wakisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli…, kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi, tutahamasisha uasi, hivyo ndivyo namna ya kupata mabadiliko…, kwa hiyo tunaenda kikinukisha…, sana sana huu uchaguzi tutaenda kuuvuruga kwelikweli…, tunaenda kukinukisha vibaya sana…”

    Kesi hiyo inasikilizwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, mbele ya jopo la majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, Jaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.

    Baada ya kesi kuitwa leo, Wakili wa Serikali Mkuu, Ajuaye Nzegeli, aliiambia Mahakama kuwa baada ya kupitia ushahidi uliowasilishwa na ushahidi wa mashahidi waliosalia, Jamhuri imeona uliopo unatosheleza.

    “Hivyo tunapenda kuitaarifu Mahakama hii tukufu kuwa upande wa Jamhuri unafunga ushahidi wake kwa mashahidi 17,” amesema Nzegeli.

    Baada ya Jamhuri kufunga ushahidi, iliomba fursa ya kuwasilisha hoja za kisheria iwapo kwa kuzingatia ushahidi uliowasilishwa Lissu ana kesi ya kujibu. Ombi hilo liliungwa mkono na Lissu na Mahakama ikatoa fursa kwa pande zote kuwasilisha hoja, huku Lissu akiwa wa kwanza kabla ya Jamhuri kujibu.

    Katika hoja zake, Lissu amesema ushahidi wa mashahidi 17 umeshindwa kujenga kesi dhidi yake kiasi cha kumlazimisha kujitetea.

    Ameanza kwa kurejea maamuzi ya Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki katika kesi za Grey Likungu Mataka na wenzake dhidi ya Jamhuri na Hatibu Gandhi na wenzake.

    Amesema kesi hizo ziliweka masharti matatu ya kuthibitisha uhaini: kwanza, mshtakiwa kuwa na utiifu kwa Jamhuri ya Muungano; pili, kuwa na nia ya kutenda uhaini; na tatu, nia hiyo ithibitishwe kwa maandishi au matendo ya wazi.

    Amesema suala la utiifu halina mjadala kwa kuwa amekubali kuwa ni raia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo hoja ni iwapo kulikuwa na nia ya kutenda uhaini na kama nia hiyo ilithibitishwa kwa maandishi au matendo ya wazi.

    Amesema katika kesi ya Grey Likungu, Jaji Mkuu wa wakati huo, Francis Nyalali, alisisitiza kuwa hatia ya uhaini inahitaji uthibitisho wa matendo ya wazi, nia ya kutenda uhaini na utiifu wa mtuhumiwa kwa Jamhuri ya Muungano.

    Kwa mujibu wa Lissu, katika kesi ya Hatibu Gandhi, Mahakama ya Rufani ilijiuliza iwapo maneno matupu ya mshtakiwa yanaweza kutengeneza kosa la uhaini na ikaweka msimamo kuwa maneno matupu si matendo ya wazi, isipokuwa yanaelezea kitendo cha uhaini.

    Amesema kitendo cha uhaini kinaweza kuwa ni kuelekeza namna ya kupindua Serikali na hatua za kutekeleza hilo, si kusema tu mtu anataka kupindua Serikali. Hata hivyo, amesema Mahakama ilieleza kuwa msimamo wa maneno matupu hautumiki kwa mshtakiwa mmoja bali unaweza kuwa tofauti kwa watu wengi ambapo maneno yanaweza kujenga njama ya kufanya uhaini.

    Akirejea ushahidi uliotolewa katika kesi yake, Lissu amesema Jamhuri haijathibitisha nia ya kutenda uhaini.

    Amesema kifungu alichoshtakiwa nacho kinahusu kuhamasisha watu waitishe Serikali, Bunge au Mahakama, na nia hiyo lazima ithibitishwe kwa maandishi au matendo ya wazi.

    Amesema katika maneno yanayodaiwa kuwa ya uhaini, Serikali, Bunge wala Mahakama havikutajwa.

    “Katika mashahidi wote 17 kila aliyezungumzia maneno hayo nilimuuliza Serikali imetajwa humo? Haimo,” amesema.

    Ameongeza kuwa Serikali ina maana ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Halmashauri, huku akisema kila shahidi aliulizwa kama alimtaja Rais, waziri mkuu au mkuu wa mkoa na hakuna aliyethibitisha.

    Amesema uchaguzi unasimamiwa na Tume ya Uchaguzi, si Serikali, hivyo kwa kuangalia hati ya mashtaka, Serikali haiwezi kutishiwa kwa kuzuia uchaguzi.

    Pia amedai maneno ya kuzuia uchaguzi na kukinukisha hayamo katika orodha ya makosa ya jinai chini ya Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2025, Sheria ya Kanuni ya Adhabu au sheria nyingine nchini.

    “Kwa hiyo uthibitisho wa uhaini kama ilivyowekwa kwenye kesi ya Grey na Gandhi haupo na kwa hakika hakuna ushahidi wa nia ya kutenda kosa lolote kwa mujibu wa sheria zinazojulikana Tanzania,” amesema.

    Lissu amesema katika kesi hiyo anashtakiwa peke yake kwa kutoa maneno, ilhali Mahakama ya Rufani katika kesi ya Gandhi ilisema hakuna kosa la maneno kwa mshtakiwa mmoja.

    “Kwa hiyo waheshimiwa majaji kama ushahidi uliotolewa umeshindwa kuthibitisha kesi ya kutenda kosa la uhaini, nitajitetea kwa lipi? Kwa hoja hiyo peke yake sina kesi ya kujibu,” amesema.

    Kuhusu madai ya uchapishaji wa maneno hayo kwenye Jambo TV, Lissu amesema Jamhuri ilipaswa kuwasilisha video na ripoti ya uchunguzi wa video hizo, lakini hakuna shahidi kati ya 17 aliyewasilisha vielelezo hivyo.

    Amesema Jamhuri iliahidi kuwasilisha nyaraka tisa, zikiwemo video clips na ripoti ya uchunguzi, lakini havikuwasilishwa. Kwa hiyo, amesema mashahidi walieleza tu kuwa waliona video bila kuiwasilisha mahakamani.

    Lissu amesema kati ya mashahidi 17, shahidi wa 17 pekee ndiye aliyekuwepo kwenye mkutano ambako alitamka maneno hayo, huku wengine 16 wakiwa mashahidi wa kusikia.

    Amesema shahidi huyo alisema yeye na wenzake watano walirekodi na kuchapisha video, hivyo hakuna ushahidi kwamba Lissu ndiye aliyeichapisha.

    Kuhusu madai kwamba yeye ndiye aliyeitisha mkutano, Lissu amesema shahidi huyo alieleza kuwa mwaliko ulitolewa na Ofisa Habari wa Chadema, Brenda Lupia, na kwamba hakumuona Lissu akifanya maandalizi ya mkutano huo.

    Kwa sababu hizo, Lissu ameiomba Mahakama imuachilie huru bila kumtaka kujitetea na, ikiwa itaridhika kuwa hana kesi ya kujibu, itoe uamuzi huo leo ili asirudi gerezani, huku uamuzi wa maandishi ukitolewa baadaye.

    Pia ameiomba Mahakama iamuru alipwe fidia, akisema amekaa gerezani kwa siku 496 kwa mashtaka anayodai hayana msingi wa kisheria na kwamba sheria inaipa Mahakama mamlaka ya kutoa fidia.

  • Hello world!

    Welcome to WordPress. This is your first post. Edit or delete it, then start writing!