Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi

By admin
August 18, 2026 3 Min Read
Comments Off on Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi

Arusha. “Mali ya baba inanitoa roho, bora nikae pembeni, niinusuru roho yangu mimi…” Hicho ndicho kibwagizo cha wimbo ‘Kilio cha Mtu Mzima’ wa OTTTU Jazz Band kilichotumiwa na Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Mbulu, Mosses Ntumengwa, kuanza uamuzi wa mgogoro wa ardhi uliowakutanisha ndugu wawili waliokuwa wakigombea shamba waliloachiwa na baba yao.

Kwa kutumia ujumbe wa wimbo huo unaogusia migogoro na maumivu yanayoweza kujitokeza katika kugawana au kugombea mali ya wazazi, Ntumengwa alionyesha namna mali ya familia inavyoweza kugeuka chanzo cha uhasama na kuvunja undugu.

Katika shauri hilo, Baraza limemtangaza Tlaka’ari Bura kuwa mmiliki halali wa ekari 11 za ardhi zilizopo Kitongoji cha Labom, Kijiji cha Mighaw, Kata ya Endahagichan, huku ndugu yake, Matle Bura, akitangazwa kuwa mvamizi wa eneo hilo.



Mwenyekiti Ntumengwa amefananisha mgogoro huo na maudhui ya wimbo huo na kueleza kuwa  ujumbe wake unafundisha kuwa mali au ardhi zilizoachwa na wazazi baada ya kufariki dunia kamwe zisifikishe mahali ndugu kupoteza utu, undugu, upendo na hata kugharimu maisha kwa sababu ya ugomvi, chuki na mifarakano kutokana na mali hizo.

Mwenyekiti huyo ameeleza kuwa wadaawa katika shauri hilo ambao ni ndugu wa damu, Baraza liliwapa nafasi ya kumaliza mgogoro huo kwa njia ya suluhu ili amani na upendo vidumu kati yao, lakini juhudi hizo hazikufanikiwa.

Mwenyekiti huyo amesema kutokana na sababu hiyo Baraza halina namna nyingine bali kuwaamua wadaawa kwa mujibu wa sheria, ili baada ya hukumu wachukue kapu na kuvuna wenyewe kila walichokipanda katika ushahidi wao.

“Kwani Baraza halina mikono, jembe na shamba la kulima pale ndugu wanapogombana ili mwishoni lichukue kapu na kuvuna. Na hii ni kulingana na methali ya Waswahili isemayo “ndugu wakigombana shika jembe ukalime, wakipatana chukua kapu ukavune,”ameeleza Mwenyekiti huyo.

Katika maombi hayo ya ardhi namba 7/2026,Tlaka’ari alidai mbele ya Baraza kuwa baba yao, Bura Gitiye alimpa eneo hilo Septemba 20,1991 na alilitumia kwa kilimo cha mahindi, maharage na alizeti toka mwaka  1991 hadi 2026, (miaka 35).

Amedai mgogoro ulianza mwaka 2024 baada ya ndugu yake kuvamia eneo hilo kwa kulima na trekta na kuwa mgogoro huo ulipelekwa kwenye ofisi za Kijiji cha Mighaw kwa ajili ya suluhu, lakini ilishindikana na ukaibuka tena mwaka 2025 .

Amedai mwaka jana mdaiwa alifyeka vichaka na kutengeneza boma huku akidai kuwa eneo hilo alipewa na wazee jambo ambalo sio la kweli, na kuwa mgogoro huo uliwahi kupelekwa kwenye Baraza la Kata ya Endahagichan kwa ajili ya suluhu lakini ilishindikana.

Mdai aliliomba Baraza kuwa atamkwe yeye ndiye mmiliki halali wa eneo hilo, Baraza litoe zuio la kudumu na amri stahiki kwa mdaiwa, wafanyakazi wake wote na wale wote wanaofanya kazi chini yake kutoingilia tena eneo la mgogoro.

Kwa upande wake mdaiwa, aliwasilisha utetezi wake mbele ya Baraza hilo huku akiomba maombi haya yatupiliwe mbali, na eneo la mgogoro litamkwe kuwa ni   la kurithi na wadaawa katika shauri na kuwa mdaiwa afidiwe gharama zake alizozitumia.

Mashahidi wa Tlaka’ari walieleza Baraza kuwa walishuhudia baba yao akimpatika Tlaka’ari eneo hilo na amekuwa akilitumia kwa muda mrefu bila mgogoro.

Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote, Mwenyekiti  amesema  Tlaka’ari amethibitisha  madai yake ya umiliki wa eneo  hilo kuwa alilipata baada ya kupewa na baba yake mzazi.

Baraza lilisema ushahidi huo uliungwa mkono na ndugu zake, Askwari Bura na Charles Bura, waliodai kushuhudia baba yao akimpa Tlaka’ari eneo hilo, pamoja na Kwaslema Matle aliyethibitisha kuwa Tlaka’ari alikuwa akilitumia eneo hilo kwa muda mrefu.

Kuhusu Matle, Baraza lilisema ushahidi wake haukuwa na nguvu, huku mashahidi wake wakitoa maelezo yaliyokinzana kuhusu chanzo cha umiliki.

“Baada ya kuona na maoni ya wazee wa baraza ambao wameona maombi hayo ya mdai yakubaliwe na mdai atamkwe kuwa mmiliki halali na mdaiwa atamkwe kuwa mvamizi na abakie eneo alilokuwa akilitumia.”

 “Baraza hili linatoa amri zifuatazo, maombi ya mdai yana mashiko na yanakubaliwa, mdai anatamkwa kuwa ndiye mmiliki halali wa eneo la mgogoro. Mdaiwa anatamkwa kuwa ni mvamizi kwenye eneo la mgogoro mali ya mdai na kwa kuwa wadaawa nia ndugu moja, kila upande utabeba gharama zake,”amesema Mwenyekiti.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Mwili wa mtoto wa miaka saba wakutwa shimoni Tabora

Next

Babu adai kupigwa ngwara na mwalimu Bahi

Recent Posts

  • Serikali yatoa siku nane kwa wazalishaji saruji kushusha bei
  • Mchengerwa ataja vipaumbele sita kupunguza vifo vya mama, mtoto
  • Babu adai kupigwa ngwara na mwalimu Bahi
  • Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi
  • Mwili wa mtoto wa miaka saba wakutwa shimoni Tabora

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme