Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Tatoa yatishia kupaki malori | Mwananchi

By admin
August 18, 2026 3 Min Read
Comments Off on Tatoa yatishia kupaki malori | Mwananchi

Dar es Salaam. Wakati Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam akianzisha operesheni ya kukamata malori yanayoegeshwa kwenye  hifadhi za barabara, Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa) kimetishia kusitisha shughuli za usafirishaji endapo Serikali  haitashughulikia changamoto zinazowakabili.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Tatoa, Elias Lukumay, alipokuwa akizungumzia agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, la kuanzisha operesheni dhidi ya malori yanayoegeshwa kwenye hifadhi za barabara.

Agosti 11, 2026, Chalamila aliliagiza Jeshi la Polisi kupitia Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa, kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), kuajiri vijana watakaosaidia katika operesheni ya kuwakamata madereva wa malori wanaokiuka utaratibu kwa kuegesha katika maeneo yaliyotengwa kwa matumizi mengine.
Chalamila alisema hatua hiyo inalenga kukabiliana na uholela katika Jiji la Dar es Salaam na kuhakikisha maeneo ya barabara yanatumika kwa mujibu wa utaratibu. Alisema agizo hilo pia linawahusu wamiliki wa mabasi.
Hata hivyo, Tatoa imeeleza operesheni za kukamata malori si suluhisho la kudumu, ikitaka Serikali ikae pamoja na wadau wa sekta hiyo ili kujadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili.



Akizungumza  jijini Dar es Salaam leo Agosti 18, 2026, Lukumay amesema wamiliki wa malori wanakabiliwa na kero mbalimbali, zikiwemo kukamatwa kwa magari, madereva kuvamiwa na kupokonywa namba za magari na malalamiko kuhusu mizani ya Iringa na Mikumi.

Amesema wamiliki wa malori hawapingi usimamizi wa Serikali, bali wanataka utekelezaji wa sheria uende sambamba na mazungumzo yatakayosaidia kutatua changamoto zinazojitokeza katika shughuli zao.

“Mnatupitisha kwenye njia ngumu kila kukicha, kero ni zilezile. Naamini katika njia ya maelewano kama itashindikana, hapo tuko tayari kuyapaki haya malori mpaka hapo tutakapokubaliana,” amesema Lukumay.

Amesema kusitisha shughuli za malori kunaweza kuathiri sekta nyingine zinazotegemea usafirishaji wa bidhaa, hususan Bandari ya Dar es Salaam, biashara ya mafuta na shughuli za wafanyabiashara wanaosafirisha bidhaa ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Lukumay, sekta ya usafirishaji pia ni chanzo cha ajira kwa madereva, wapakuaji na makundi mengine yanayohusika katika mnyororo wa usafirishaji.

Amesema Serikali na wamiliki wa malori wanapaswa kujenga utaratibu wa mazungumzo ya kudumu ili kuepusha migogoro na kuhakikisha shughuli za usafirishaji zinaendelea bila kuathiri uwekezaji na maeneo mengine ya  kiuchumi.

Lukumay amezitaka mamlaka husika kupunguza utegemezi wa operesheni za kukamata malori na badala yake kuweka mfumo wa ushirikiano unaozingatia sheria, usalama wa barabara na masilahi ya sekta ya usafirishaji.

Akisimulia changamoto wanazokutana nazo hadi kulazimika kuegesha malori katika hifadhi za barabara, mmoja wa madereva, Elias Mwaningo, amesema tatizo kubwa ni ukosefu wa maeneo maalumu ya kuegesha.

Mwaningo alitoa kauli hiyo mbele ya Chalamila wakati mkuu huyo wa mkoa alipofanya ziara katika maeneo ya Kurasini na kushuhudia malori yakiwa yameegeshwa kwenye hifadhi ya barabara.

“Changamoto ni nyingi. Tunaleta mizigo mingi, lakini kasi ya kuipokea kwenye ICD ni ndogo, kiasi kwamba msongamano wa malori unakuwa mkubwa na tunakosa hata sehemu ya kwenda kujisaidia haja ndogo,” amesema.

Kwa mujibu wa Mwaningo, madereva pia wanakabiliwa na changamoto katika maeneo wanapopeleka mizigo, ikiwemo vitendo vya rushwa na ucheleweshaji wa upakuaji.

Amesema wakati mwingine gari linaweza kukaa hadi wiki bila kuruhusiwa kushusha mzigo, huku magari yaliyowasili baadaye yakipewa kipaumbele cha kushusha mizigo.

 “Kuna wakati gari inamaliza hadi wiki hairuhusiwi kwenda kushusha mzigo, badala yake anachukuliwa aliyefika leo kwenda kushusha bila kujali kuna wengine waliojipanga kwenye mstari,” amesema.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

TBS YALENGA VIFAA BORA NA MATUMIZI SALAMA YA UMEME KUPITIA MEPS

Next

WRRB, MIKOA NA HALMASHAURI KUIMARISHA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA

Recent Posts

  • Serikali yatoa siku nane kwa wazalishaji saruji kushusha bei
  • Mchengerwa ataja vipaumbele sita kupunguza vifo vya mama, mtoto
  • Babu adai kupigwa ngwara na mwalimu Bahi
  • Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi
  • Mwili wa mtoto wa miaka saba wakutwa shimoni Tabora

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme