NSSF WAWAFIKIA BODABODA CHUNYA KWA FURSA KUJALI MAISHA YAO.

 

NA JOSEA SINKALA, MBEYA.

Mfuko wa Taifa wa hifadhi ya jamii (NSSF) ambao hutoa hifadhi ya jamii kwa wanachama walioajiriwa na waliojiajiri sasa imeendelea kutoa elimu na fursa mbalimbali kwa jamii ikiwemo program ya skimu ya Taifa ya hifadhi ya jamii kwa wananchi waliojiajiri ili kuwaendeleza kwenye shughuli za kiuchumi.

Akizungumza mkoani Mbeya afisa mwandamizi wa NSSF kutoka mkoani humo bwana Ibrahim Nganga, amesema katika kufikia maendeleo endelevu na hususani kuelekea dira ya maendeleo ya Taifa mwaka 2050 Serikali kupitia mfuko huo imeamua kulifikia kundi madereva bodaboda katika Halmashauri ya wilaya ya Chunya ili kuwapatia fursa ya kujiunga na mfuko huo kwa ajili ya maisha yao bora ya sasa na baadaye.

Amesema madereva hao hukumbana na changamoto mbalimbali wawapo kazini hivyo kushindwa kumudu utunzaji wa fedha, gharama za matibabu na mahitaji mengine watakayosaidika kutokana na uwekezaji kwenye mfuko huo wa hifadhi ya jamii.

Hata hivyo afisa mwandamizi huyo wa NSSF amewaomba madereva katika maeneo mbalimbali kuchangamkia fursa hiyo kwa faida yao, familia zao na Taifa kwa ujumla ikiwemo kunufaika na pensheni kama za uzeeni, za ulemavu, uzazi na mafao ya matibabu.

Makamu wa rais mbaroni kwa ulanguzi wa dawa za kulevya

Monrovia. Aliyekuwa Makamu wa Rais wa Liberia, Jewel Howard Taylor, amekamatwa na Jeshi la Polisi nchini humo na kufunguliwa mashtaka ya kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya, utakatishaji fedha na makosa mengine yanayohusishwa na mtandao wa kimataifa wa usafirishaji wa dawa za kulevya.

Kukamatwa kwa Howard Taylor, kunakuja baada ya mamlaka ya Liberia kutangaza kukamata  kokeini yenye thamani ya takriban dola milioni 317 (Sh808.4 bilioni) iliyokuwa ikielekea barani Ulaya mwezi mmoja uliopita.

Taarifa kutoka  Wizara ya Sheria ya Liberia imeeleza  kuwa, Howard Taylor, aliyekuwa Makamu wa Rais wakati wa utawala wa Rais wa zamani George Weah kuanzia mwaka 2018 hadi 2024, alikamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Roberts akiwa katika harakati za kuondoka nchini humo.

“Polisi wamewashtaki raia watatu wa kigeni  wawili wa Kroatia na mmoja wa Ukraine ambao walikuwa sehemu ya mtandao na Howard Taylor ili kupisha uchunguzi kwa ajili ya kuwachukuia hatua za kisheria,”imeeleza taarifa hiyo.

Mbali na tuhuma za ulanguzi wa dawa za kulevya na utakatishaji fedha, kiongozi huyo pia anakabiliwa na  tuhuma za kuingiza  dawa zinazodhibitiwa nchini humo bila kibali kutoka mamlaka husika, kushawishi kutendwa kwa uhalifu dhidi ya serikali. Serikali ya Liberia imesema inaendelea na uchunguzi ili kubaini ukweli wa tuhuma hizi ambazo ni  juhudi za kukabiliana na mitandao ya kimataifa ya biashara ya dawa za kulevya huku ikiahidi kuhakikisha mchakato wa kisheria unaendelea bila kuingiliwa kisiasa.

Kwa upande wake, Wakili wa Howard Taylor, Kabineh Ja’neh amekiri kuwa mteja anashikiliwa na mamlaka za kiusalama nchini humo na wataendelea akifikishwa mahakamani.

“Yupo chini ya ulinzi wa polisi wa taifa wa Liberia usiku na  tunategema  kuendelea na suala hilo mara tutakapopata shtaka rasmi,”amesema.

Ikumbukwe kuwa Rais wa Liberia, Joseph Boakai, alipoingia madarakani Januari 2024, aliahidi kuimarisha mapambano dhidi ya ufisadi na kuhakikisha matumizi ya rasilimali za umma yanafanyika kwa uwazi na uwajibikaji.

Ahadi hiyo imekuwa miongoni mwa vipaumbele vya utawala wake katika juhudi za kurejesha imani ya wananchi kwa taasisi za serikali.

Na tangu aingie madarakani, serikali ya Boakai imechukua hatua mbalimbali zinazolenga kuwawajibisha watumishi na viongozi wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo vya ufisadi.

Hatua hizo zimehusisha kuimarisha uchunguzi na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya baadhi ya viongozi wa zamani, ikiwa ni sehemu ya juhudi za serikali kupambana na ufisadi na kuimarisha utawala wa sheria.

Imeandikwa na Elidaima Mangela kwa msaada wa mashirika ya habari.

BODABODA LUPATINGATINGA WAFIKIWA, ‘UKIUMIA KICHWA HAKUNA KICHWA BANDIA’.

 

Na Josea Sinkala, Mbeya.

Huko mkoani Mbeya, madereva wa pikipiki za magurudumu mawili (Bodaboda) wameelezwa kuwa baadhi yao bado ni changamoto katika kutii sheria za usalama barabarani hatua inayochochea kuendelea kutokea kwa ajali zisizo na ulazima na kugharimu maisha ya bodaboda.

Kwa mujibu wa Afande Deo wa kituo cha Polisi Lupatingatinga wilayani Chunya mkoani Mbeya, madereva wengi wamekuwa wakiendesha vyombo vyao kwa uzembe na bila kujijali na kusababisha ajali mbalimbali.

Baadhi ya madereva wanatajwa kutokuwa na leseni, kuendesha pikipiki bila kuvaa kofia ngumu (helmet) huku baadhi wakitumiwa katika matukio ya uhalifu jambo ambalo Polisi imeonya na kuwaomba madereva bodaboda kutokuwa chachu ya uhalifu.

Kwa upande wake kaimu Katibu wa bodaboda wilaya ya Chunya amewashauri madereva wenzako kuacha makusudi na kuzingatia mafunzo ambayo wamekuwa wakipewa mara kadhaa ikiwa ni pamoja na kujitokeza kwenye mafunzo ambayo yamekuwa yakiitishwa kwa faida yao wenyewe.

Namna huduma za mawasiliano zinavyotumiwa na Watanzania

Sekta ya mawasiliano nchini imeendelea kukua kwa kasi katika robo mwaka iliyoishia Juni 2026, huku ongezeko la laini za simu, matumizi ya intaneti na huduma za fedha mtandao likiashiria kukua kwa huduma za kidijitali katika shughuli mbalimbali.

Takwimu zilizotolewa katika ripoti robo mwaka ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zinaonyesha kuwa jumla ya laini za simu hai ilifikia milioni 116.95 hadi Juni mwaka huu, sawa na ongezeko la asilimia 4.51 ndani ya robo mwaka ulioishia Juni 2026.

Idadi hiyo imeifanya Tanzania kuwa na kiwango cha upenyaji wa mawasiliano cha zaidi ya asilimia 167, hali inayotokana kwa kiasi kikubwa na matumizi ya laini zaidi ya moja kwa mtu mmoja au taasisi.

Vodacom iliendelea kuwa kinara wa soko ikiwa na asilimia 33 ya usajili huo, ikifuatiwa na Yas yenye asilimia 28.6, Airtel asilimia 20.5, Halotel asilimia 16.4 na TTCL asilimia 1.5.

Hata hivyo pamoja na ukuaji huo takwimu zinaonyesha bado kuna pengo la kijinsia katika matumizi ya huduma hizo kwani wanaume walikuwa na usajili wa P2P milioni 59.48 ikilinganishwa na milioni 56.24 za wanawake.

Kwa upande wa kijiografia, Dar es Salaam iliendelea kuongoza kwa kuwa na usajili milioni 21.53, ikifuatiwa na Mwanza milioni 7.75, Arusha milioni 7.04, Mbeya milioni 6.73 na Dodoma milioni 6.24.

Kupiga simu kuliongezeka ila SMS zinapungua

Licha ya kuongezeka kwa matumizi ya huduma zinazotumia intaneti, simu za sauti bado zimeendelea kuwa muhimu, huku matumizi yake yakiongezeka katika robo mwaka hiyo.

Takwimu zinaonyesha matumizi ya simu za ndani yaliongezeka kwa asilimia 7.44, kutoka dakika bilioni 45.44 katika robo mwaka iliyoishia Machi hadi dakika bilioni 48.82 Juni.

Ongezeko hilo lilitokana na kuongezeka kwa simu zinazopigwa ndani ya mtandao mmoja (on-net) kwa asilimia 5.68 na zile zinazopigwa kutoka mtandao mmoja kwenda mwingine (off-net) kwa asilimia 9.23. Simu za kimataifa nazo ziliongezeka.

Tofauti na simu za sauti, matumizi ya ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) yalibaki karibu katika kiwango kilekile, huku yakipungua kwa kiasi kidogo.

Matumizi ya SMS za ndani yalishuka kwa asilimia 0.05, kutoka ujumbe bilioni 55.08 Machi hadi bilioni 55.05 Juni.

Mwelekeo huo unaakisi mabadiliko ya tabia za watumiaji, ambao sasa wanazidi kutumia WhatsApp, mitandao ya kijamii na programu nyingine za mawasiliano yanayotumia intaneti.

“Sina haja ya kujiunga na SMS siku hizi maana na chati zaidi kwa kutumia Whatsapp na Telegram, nikishakuwa na bado natuma tu, intaneti ndiyo ya muhimu ukiwa nayo unafanya vingi, unaperuzi pia hata kupiga simu,” anasema Aneth Jackson Mkazi wa Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo matumizi ya intaneti nayo yaliongezeka kwa asilimia 6.48, kutoka milioni 58.97 Machi hadi milioni 62.79 Juni, na kufikisha kiwango cha upenyaji wa intaneti asilimia 89.7.

Huduma za intaneti kupitia mitandao ya simu ya kasi ziliendelea kutawala, zikiwa na usajili milioni 37.58, huku 2G ikiwa na usajili milioni 24.63.

Matumizi ya intaneti yaliongezeka kwa asilimia 11.65, kutoka petabyte 932 hadi petabyte 1,041 katika robo mwaka hiyo. Matumizi makubwa zaidi yalikuwa katika mitandao ya kijamii ya YouTube, TikTok, Facebook, Instagram na WhatsApp.

Upatikanaji wa 5G kwa wakazi uliongezeka kutoka asilimia 32.83 Machi hadi asilimia 34.18 Juni, huku upatikanaji wake kijiografia ukiongezeka kutoka asilimia 11.04 hadi 11.34.

Kwa upande wa 4G, upatikanaji kwa wakazi ulifikia asilimia 94.39, kutoka asilimia 94.32, wakati upatikanaji kijiografia ulifikia asilimia 77.53.

Hata hivyo pamoja na upatikanaji mpana wa mitandao, umiliki wa simu janja bado ni kikwazo katika kuongeza matumizi ya huduma za kidijitali.

Upenyaji wa simu janja uliongezeka kutoka asilimia 42.50 Machi hadi asilimia 44.74 Juni, huku simu janja milioni 31.34 zikiwa zimeunganishwa kwenye mitandao ya waendeshaji huku simu za kawaida zikiwa bado kwenye soko, zikiwa milioni 58.40 na kiwango cha upenyaji cha asilimia 83.38.

Miamala ya simu yashika kasi

Eneo lililoonyesha ukuaji mkubwa zaidi ni huduma za fedha mtandao. Idadi ya akaunti hai za fedha mtandao iliongezeka kwa asilimia 7.5, kutoka milioni 80.98 Machi hadi milioni 87.05 Juni.

M-Pesa iliendelea kutawala soko kwa ukubwa ikiwa na asilimia 40.6 ya usajili (Yaani kila kati ya watu 10 wanaotumia huduma za miamala wanaotumia M-Pesa ni wanne), ikifuatiwa na Mixx by Yas yenye asilimia 32, Airtel Money asilimia 16.4 na HaloPesa asilimia 10.1.

Kwa pamoja, M-Pesa, Mixx by Yas na Airtel Money zilidhibiti takriban asilimia 89 ya usajili wa huduma za fedha mtandao. Ukuaji huo haukuishia kwenye idadi ya akaunti. Jumla ya miamala ya fedha mtandao iliongezeka kwa asilimia 5.38 katika robo mwaka, kufikia bilioni 2.10, kutoka bilioni 1.99 Machi.

Kwa mwezi Juni pekee, watoa huduma walirekodi miamala milioni 710.99, kutoka milioni 679.19 Aprili, katika miamala hiyo M-Pesa pia iliongoza kwa miamala milioni 286.41, ikifuatiwa na Mixx by Yas milioni 228.59 na Airtel Money milioni 129.14.

Akizungumzia ripoti ya kipindi kama hicho ya Vodacom Mkurugenzi wake Philip Besiimire alisema huduma za miamala ya simu na ongezeko la matumizi ya intaneti katika soko la Mawasiliano vimekuwa na mchango mkubwa katika mapato ya kampuni hiyo.

Alisema katika kipindi hiki cha mwaka uliopita, wateja wa M-Pesa waliongezeka kwa asilimia 22.6, jambo linalodhirisha namna matumizi ya fedha kidijitali yanavyozidi kusimika mizizi katika maisha ya kila siku.

“M-Pesa ni nyenzo muhimu katika kuendeleza ujumuishaji wa kifedha nchini Tanzania kupitia suluhisho za kisasa kama mikopo ya kidijitali, usimamizi wa uwekezaji na utajiri, akiba za vikundi na huduma za malipo ya kidijitali,” alieleza Besiimire.

Kwa upande mwingine alisema mapato yatokanayo na huduma za intaneti yaliongezeka kwa asilimia 29.5, yakichochewa zaidi na ongezeko la mamilioni ya watumiaji wa huduma za data, ikiwa ni zaidi ya asilimia 25 ya data ikilinganishwa na ripoti ya mwaka uliopita.

“Matumizi ya simu janja pia yameendelea kuongezeka kwa kasi kubwa kupitia mkakati wetu endelevu wa kuongeza matumizi ya simu janja nchini Tanzania, tumefanikisha kufikisha mtandao wetu kwa watumiaji wa simu janja milioni 11.5,” Alisema Besiimire.

Uchaguzi wa wenye ‘kofia mbili’ Moshi Mjini waibua mtafaruku

Dar/Moshi. Ni mtikisiko. Ndiyo kauli unayoweza kutumia kuelezea kinachoendelea katika wilaya ya kichama ya Moshi Mjini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya uongozi kuagiza ufanyike uchaguzi kujaza nafasi za viongozi wanaoshikilia kofia mbili za uongozi.

Makada mbalimbali waliohojiwa na gazeti hili leo Agosti 19, 2026, wamedai agizo hilo likitekelezwa nchini, litagusa hadi viongozi wa kitaifa na hivyo wameshauri usitishwe na kusubiri uchaguzi wa ndani ya chama mwakani.

“Moshi haijatulia. Unapoleta hoja ya kujaza nafasi kwa wenye kofia mbili ya uenyekiti wa kata na udiwani, unafanya watu wahoji mbona kuna viongozi wa kitaifa wana kofia mbili? Ni wenyeviti na wabunge,” alidai kada mmoja.

“Tayari kuna hisia kwamba ipo agenda ya siri ya hiki kinachoendelea. Kwa nini Moshi Mjini tu ambayo inanyemelewa na bundi? Ili kutuliza mtafaruku na hisia mbaya, CCM Makao Makuu waseme kama hili jambo ni la nchi nzima.”

Agizo hilo la CCM Moshi Mjini limeibua taharuki huku wakihoji kama lina baraka za uongozi wa juu wa chama hicho, kwa kuwa wapo viongozi wa kitaifa kama Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu.

Mbali na Chatanda, wametolea mfano wa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Patrick Mwalunenge, ambaye pia ni Mbunge wa Mbeya Mjini, wakihoji kwa nini kushikilia nafasi mbili za uenyekiti na ubunge hakuna uchaguzi unafanyika kujaza nafasi yake.

Orodha hiyo ni ndefu kuanzia viongozi wa kitaifa hadi wale wa ngazi ya kata.

Hata hivyo, uongozi wa CCM mkoani Kilimanjaro umefafanua sababu za uamuzi huo.

Katika wilaya ya Moshi Mjini, Kata ya Kiusa, ambaye diwani wake ni Khalid Shekoloa, na Soweto, ambayo diwani wake ni Paul Maile, ndiyo wanaoshikilia nafasi ya udiwani na wakati huohuo mwenyekiti wa kata, nafasi ambazo zimetakiwa kujazwa.

Barua ya Agosti 12, 2026, yenye kumbukumbu CW/MSM/KK/Vol.V/95 iliyosainiwa na Katibu wa Wilaya, Amos Shimba, inaeleza kuwa maagizo ya kujaza nafasi hizo ni kwa mujibu wa Ibara ya 129 ya Katiba ya CCM, toleo la Mei 2025.

Shimba, kupitia barua hiyo iliyotumwa kwa makatibu wa kata wa CCM Wilaya ya Moshi Mjini, amesema katiba inaelekeza wakati wowote kunapotokea nafasi wazi miongoni mwa viti vyovyote vya CCM, kikao husika kijaze nafasi hiyo bila kuchelewa.

“Mnaelekezwa kusimamia na kuratibu chaguzi za kujaza nafasi wazi za uongozi wa CCM ngazi ya shina, tawi na kata ambazo uchujaji na uteuzi wa mwisho wa wagombea huishia ngazi ya mkoa,” inasema barua hiyo na kuongeza:

“Aidha, mnakumbushwa kuepuka kasoro zote zinazogusa maadili ya chama na za utendaji ambazo zinaweza kusababisha watu wasiostahiki kuchaguliwa, kupenya kwenye nafasi hizi za uongozi ama kwa rushwa, upendeleo au hila.”

“Kanuni na maadili ya chama yazingatiwe kwa ukamilifu na vikao vyote vinavyochuja na kuteua wagombea wa chaguzi za kujaza nafasi wazi katika ngazi husika vinapaswa kukamilika ifikapo tarehe 30.09.2026,” inasisitiza barua hiyo.

Gazeti hili limeona tangazo lililobandikwa Kata ya Kiusa likiwatangazia wanachama wote wenye sifa za uongozi kuanzia Agosti 17 hadi Agosti 23, 2026 kuchukua fomu kwenye ofisi ya kata.

Tangazo hilo linasema nafasi inayogombewa ni mwenyekiti wa CCM kata.

Tangu uchaguzi mkuu wa 2025, Jimbo la Moshi Mjini halijawahi kutulia huku baadhi ya viongozi wa CCM wakituhumiwa kuendekeza makundi na kuanza kutengeneza safu ya uongozi kuelekea uchaguzi wa ndani wa CCM 2027.

Kwa mujibu wa chanzo kimoja ndani ya CCM, safu hizo zinatengenezwa kwa malengo ya mwaka 2030 na uchaguzi wa ndani wa CCM mwakani.

Alipotafutwa kuzungumzia hilo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi amesema walichokifanya ni kutekeleza maelekezo kutoka mamlaka za juu za chama.

Ameeleza nafasi walizoelekeza zijazwe ni kuanzia tawi, shina hadi kata, akisisitiza maelekezo hayo hayahusu Wilaya ya Moshi pekee, bali Tanzania nzima.

“Siyo Moshi pekee, kila eneo nchi nzima. Sisi tumepokea maelekezo kwamba nafasi zote zilizopo wazi zijazwe kuanzia shina, tawi hadi kata,” amesema.

Alipoulizwa iwapo kujaza nafasi hizo kunahusisha pia nyadhifa za wilaya, mikoa na Taifa, Boisafi amesema hilo si sehemu ya maelekezo na kama litakuwepo, utatangazwa utaratibu wake.

Hata hivyo, Shekoloa ambaye ni mwenyekiti wa CCM wa kata hiyo na diwani wa kata hiyo, alipoulizwa na gazeti hili leo Agosti 19, 2026 amesema:

“Ni kweli kuna uchaguzi wa kujaza nafasi yangu, lakini kwa mujibu wa kanuni na taratibu za chama, hatuna maelekezo yoyote rasmi kutoka ngazi za juu kwa sababu tukiangalia, kwa mfano, Mwenyekiti wa UWT (Chatanda) pia ni Mbunge,” alieleza.

“Nenda kule Mbeya pia. Mwenyekiti wa CCM wa mkoa ndiye Mbunge wa Mbeya Mjini. Mwenyekiti wa UWT Taifa ni mbunge. Kuna watu lukuki, naweza hata kukutumia orodha ya nchi nzima. Hatusikii kama kuna kuachia nafasi moja.”

Wadau wataka mfumo maalumu kudhibiti ucheleweshaji miradi ya afya – 4

Dar es Salaam. Serikali inapaswa kuanzisha mfumo maalumu wa kitaifa wa kusimamia miradi ya afya, utakaohakikisha fedha zinatolewa kwa wakati, uwezo wa wakandarasi unathibitishwa kabla ya kupewa kazi na mikataba inasimamiwa kwa karibu hadi mradi unapokamilika na kuanza kutoa huduma.

Hayo ni miongoni mwa mapendekezo yanayotolewa na wataalamu wa afya, viongozi wa kisiasa, wananchi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), wakisisitiza kuwa suluhisho la ucheleweshaji wa miradi ya afya linahitaji mabadiliko katika mfumo mzima wa utekelezaji, badala ya kutegemea hatua za dharura baada ya mradi kusuasua.

Mfumo huo unapendekezwa uwe na uwezo wa kuonesha kwa wakati maendeleo ya kila mradi, fedha zilizotengwa na zilizotolewa, kiwango cha utekelezaji, changamoto zinazoukabili na hatua zinazopaswa kuchukuliwa pale ratiba inapokiukwa.

Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk Alex Msoka, anasema Serikali inapaswa kuanza kwa kufanya tathmini ya haraka ya miradi yote ya hospitali iliyochelewa nchini ili kubaini hali halisi kabla ya kuamua hatua za kuchukua.

“Jambo la kwanza ni kufanyika kwa tathmini ya haraka ya miradi yote ya hospitali iliyochelewa, ikiwamo kubaini asilimia ya utekelezaji, sababu za uchelewaji, fedha zilizotumika na fedha zinazohitajika kukamilisha mradi,” anasema.

Baada ya tathmini hiyo, anapendekeza miradi yenye umuhimu mkubwa kwa wananchi ipewe kipaumbele, iwe na muda maalumu wa kukamilika na mpango wa utekelezaji unaoweza kupimwa na kufuatiliwa.

Kwa Dk Msoka, mfumo huo haupaswi kuishia katika kujua mradi umefikia wapi, bali unatakiwa kuweka wazi nani anawajibika kwa kila hatua na nini kinapaswa kufanyika pale mkandarasi au taasisi inayohusika inaposhindwa kutekeleza wajibu wake.

Anasema pale mkandarasi anaposhindwa kutekeleza majukumu yake, hatua za kimkataba zinapaswa kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria bila kusubiri ucheleweshaji uongezeke na kuathiri gharama na muda wa mradi.

Pendekezo lingine ni kubadili mfumo wa upangaji na utoaji wa fedha za miradi ya afya.

Wadau wanataka Serikali ijiridhishe kabla ya kuanza mradi kwamba ina mpango wa fedha unaoweza kuufikisha hadi kukamilika, badala ya kuanza ujenzi bila uhakika wa mtiririko wa fedha.

Kwa mujibu wa hoja zinazotolewa, utoaji wa fedha unapaswa kuendana na ratiba ya ujenzi na hatua zilizofikiwa, huku malipo yakifanyika kwa kazi iliyotekelezwa na kuthibitishwa.

Mbunge wa Singida Mjini, Yagi Kiaratu, anasema Serikali inapaswa kutoa kipaumbele kwa kukamilisha miradi iliyoanza kabla ya kuanzisha mingine.

 “Ushauri wangu kwa Serikali ni ichukue jitihada za kuhakikisha kwanza miradi ya zamani inakamilika kuliko kuanzisha mingine. Tukimaliza iliyopo ndipo tuanze mingine kulingana na mahitaji,” anasema.

Kiaratu anasema utoaji wa fedha kwa awamu ndogo ndogo unaweza kuchangia miradi kusuasua na kuongeza gharama, hivyo utekelezaji wa bajeti unapaswa kwenda sambamba na upatikanaji wa fedha kwa wakati.

Kuhusu mikataba, mapendekezo ya CAG yanaweka mkazo katika hatua ambayo mara nyingi huamua hatima ya mradi kabla hata ujenzi haujaanza, katika uchaguzi wa mkandarasi.

CAG, Charles Kichere, anasisitiza umuhimu wa kuzingatia taratibu za ununuzi na kufanya tathmini ya kutosha ya uwezo wa mkandarasi kabla ya kumpa mkataba.

Kwa mantiki hiyo, bei ya chini pekee haipaswi kuwa msingi wa uteuzi. Uwezo wa kifedha, kitaalamu na kiutendaji wa mkandarasi kutekeleza mradi kwa muda uliokubaliwa unapaswa kuthibitishwa.

CAG pia anapendekeza usimamizi na ufuatiliaji wa mikataba uimarishwe ili kuhakikisha kazi zinatekelezwa kwa mujibu wa masharti, gharama na muda uliokubaliwa.

Pale mkandarasi anaposhindwa kutekeleza wajibu wake, hatua stahiki zichukuliwe kwa mujibu wa mkataba na sheria za ununuzi.

Teknolojia itumike katika ufuatiliaji

Mbunge Kiaratu anapendekeza Serikali kutumia mifumo ya kidijitali kufuatilia maendeleo ya miradi kwa wakati halisi.

Kwa mfumo huo, taarifa za utekelezaji, matumizi ya fedha na hatua iliyofikiwa zinaweza kupatikana kutoka ngazi ya eneo la mradi hadi Serikali Kuu.

“Mfumo huo ni mzuri kwa sababu unaleta uwazi. Rai yangu ni uboreshwe vizuri na usomane kuanzia chini mpaka juu. Tukienda hapo, kila kitu kitakuwa wazi na usimamizi utakuwa rahisi,” anasema.

Mfumo wa aina hiyo unaweza pia kusaidia kubaini mapema mradi unaoanza kutoka kwenye ratiba, badala ya kusubiri ucheleweshaji uwe mkubwa ndipo uongozi uchukue hatua.

Wadau pia wanataka taarifa za miradi ziwe wazi kwa wananchi wanaotarajia kunufaika na huduma hizo.

Rehema Jonas, mkazi wa Singida, anasema wananchi wanapaswa kujua mradi umefikia hatua gani, muda uliopangwa wa kukamilika na namna fedha za umma zinavyotumika.

“Serikali inapaswa kuhakikisha mikataba inasimamiwa ipasavyo na hatua zinachukuliwa kwa wale wanaochelewesha utekelezaji bila sababu za msingi. Wananchi tunahitaji kuona miradi inayotumia fedha za umma inakamilika na kuanza kutoa huduma,” anasema.

Kwa mtazamo wake, uwazi wa taarifa unaweza kuongeza shinikizo la uwajibikaji na kupunguza sintofahamu kuhusu matumizi ya fedha za umma.

Singida iwe kipimo cha utekelezaji

Mapendekezo hayo yanapata uzito katika Mkoa wa Singida, ambako ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa umekuwa sehemu ya mjadala kuhusu ucheleweshaji wa miradi ya afya.

Badala ya kuangalia mradi huo kama changamoto ya Singida pekee, wadau wanaona unapaswa kuwa sehemu ya tathmini pana ya namna miradi ya afya inavyopangwa, kufadhiliwa na kusimamiwa nchini.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Jessica Lebba, anasema uongozi wa mkoa na hospitali umeweka mkakati wa kuhakikisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa unakamilika ndani ya muda wa mkataba na kwamba ukaguzi wa mara kwa mara unafanyika kufuatilia kasi na ubora wa kazi.

Kwa mujibu wa Dk Lebba, kukamilika kwa hospitali hiyo kutasaidia kupunguza gharama za rufaa na safari za wagonjwa, huku wananchi wakipata huduma za kibingwa karibu na maeneo yao.

Katika ngazi ya jamii, Kamati za Afya za Vituo vya Huduma za Afya (HFGC) zinaweza kuwa sehemu ya mfumo huo wa ufuatiliaji.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk Grace Magembe, anasema kamati hizo zinapaswa kupata mafunzo ya awali kuhusu usimamizi wa ujenzi, upokeaji wa miradi na ufuatiliaji wa ubora wa kazi.

Anasema pia zinapaswa kushirikishwa katika hatua muhimu za miradi, ikiwamo uchaguzi wa wakandarasi na makabidhiano.

Hii inaweza kuongeza ufuatiliaji kutoka ngazi ya jamii na kuwezesha changamoto kubainika mapema kabla hazijageuka kuwa ucheleweshaji mkubwa.

Kwa wananchi, kipimo cha mwisho cha mafanikio ya mradi wa afya si kukamilika kwa jengo pekee, bali uwezo wake wa kuanza kutoa huduma zilizokusudiwa.

Rama Rashid, mkazi wa Singida Mjini, anasema Serikali inapaswa kuwa na mkakati maalumu kwa miradi ya afya kwa sababu inahusisha moja kwa moja maisha ya wananchi.

“Miradi kama hospitali haipaswi kusubiri muda mrefu kukamilika kwa sababu kila siku wananchi wanahitaji huduma,” anasema.

Rais wa MAT, Dk Msoka, anaongeza kuwa uboreshaji wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida unapaswa kwenda sambamba na kuwepo kwa muunganiko mzuri wa huduma za afya na usafiri ili wagonjwa waweze kufika hospitalini kwa wakati.

Kwa hiyo, mfumo unaopendekezwa unapaswa kuanzia kabla ya ujenzi kwenye upangaji na bajeti na kuendelea hadi hospitali inapokabidhiwa, kuwekewa vifaa, wataalamu na kuanza kutoa huduma.

Hapo ndipo suluhisho la ucheleweshaji wa miradi ya afya linapoweza kutoka kwenye kufuatilia tatizo baada ya kutokea na kwenda kwenye kuzuia tatizo kabla halijatokea.

Badala ya Serikali kusubiri mradi uchelewe, mfumo huo utawezesha kubaini mapema upungufu wa fedha, udhaifu wa mkandarasi, kuchelewa kwa malipo au changamoto nyingine na kuchukua hatua kabla gharama haijawa kubwa zaidi.

Kwa Dk Msoka, huo ndio msingi wa mfumo wa kitaifa wa usimamizi wa miradi ya afya unaopaswa kuzingatia mahitaji halisi ya wananchi, bajeti ya mradi hadi kukamilika na kuanza kutoa huduma, pamoja na uwajibikaji wa wazi kwa kila taasisi na kiongozi mwenye dhamana.

Sakata la mabasi Stendi ya Magufuli bado moto

Dar es Salaam. Amri ya Serikali ya kuzuia mabasi ya mikoani kupakia na kushusha abiria nje ya Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli, Mbezi Luis, imeanza kung’ata na kuzua mvutano, baada ya viongozi wa kampuni moja ya usafirishaji kukamatwa na kufikishwa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila.

Mkurugenzi na meneja wa kampuni ya Tilisho jana, Jumatano Agosti 19, 2026, walifikishwa mbele ya Chalamila wakiwa wamefungwa pingu, wakituhumiwa kukiuka agizo la Serikali na kuendelea na utaratibu wa kupakia abiria nje ya kituo hicho.

Viongozi hao walikamatwa wakati wa ukaguzi uliofanywa na viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa lengo la kuhakikisha utekelezaji wa agizo la Chalamila alilolitoa Agosti 11, 2026, likitaka mabasi yote ya mikoani kuanza na kumalizia safari katika Kituo cha Magufuli.

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando, alisema viongozi hao walikamatwa baada ya mamlaka kubaini basi la kampuni hiyo likifanya shughuli za usafirishaji eneo la Riverside, Ubungo kinyume na agizo la Serikali.

Alisema mamlaka zililifunga basi hilo kwa mnyororo, lakini mmiliki wake alipofika eneo hilo alifungua mnyororo huo na kuliondoa.

Mkurugenzi wa kampuni ya mabasi ya Tilisho na meneja wake wakiwa wanapelekwa kwa Mkuu wa Mkoa na pungu mkononi baada ya kukiuka agizo la mabasi yake kwenda kituo Cha Magufuli.

“Wakati tunafanya ukaguzi tulilikuta basi la Tilisho Riverside. Tulilifunga mnyororo kwa sababu lilikuwa linafanya shughuli ambazo Serikali imeagiza zifanyike Kituo cha Magufuli. Mmiliki alipofika alifungua mnyororo na kuliondoa,” amesema Msando.

Baada ya kusikiliza maelezo ya tukio hilo, Chalamila aliwasamehe viongozi hao, lakini akasema hatua hiyo iwe fundisho kwa kampuni nyingine zitakazojaribu kukaidi agizo la Serikali.

Alisema Serikali haitaruhusu baadhi ya wamiliki wa mabasi kuanzisha vituo vyao katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam kwa masilahi binafsi, wakati Serikali imewekeza zaidi ya Sh50 bilioni kujenga Kituo cha Magufuli.

“Latra, kwa yeyote atakayekaidi kutekeleza agizo la kushusha na kupakia abiria hapa, futa vibali vyote,” amesema Chalamila.

Alisema utekelezaji wa agizo hilo unalenga kuweka utaratibu katika shughuli za usafirishaji wa mabasi ya mikoani, huku akitaka mamlaka husika kuhakikisha hakuna kampuni inayoruhusiwa kuendesha vituo visivyo rasmi katika maeneo mengine ya jiji.

Aidha, Chalamila amepiga marufuku mabasi kuegesha au kushusha abiria katika eneo la Shekilango, akisema kampuni zitakazobainika kufanya hivyo zitachukuliwa hatua za kisheria.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila alivyopokelewa leo Agosti 19, 2026 Kituo Kikuu cha mabasi cha Magufuli

Hatua hiyo imekuja wakati utekelezaji wa agizo la kurejesha shughuli zote za mabasi ya mikoani katika Kituo cha Magufuli ukiendelea kuzua mjadala miongoni mwa wamiliki wa mabasi na wadau wa usafirishaji; baadhi wakieleza changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wake.

Hata hivyo, Chalamila amesema Serikali iko tayari kusimamia agizo hilo na kuhakikisha uwekezaji uliofanywa katika Kituo cha Magufuli unatumika ipasavyo kwa manufaa ya abiria na sekta ya usafirishaji.

Abiria washushwa, mabasi madogo yatumika

Utekelezaji wa agizo hilo umeanza kuleta mabadiliko katika usafirishaji wa abiria na baadhi ya mabasi ambayo awali yalikuwa yakipakia au kushusha abiria katika ofisi za kampuni zilizokuwa nje ya Stendi ya Magufuli, sasa yameanza kuwafikisha abiria kituoni hapo.

Katika maeneo ambayo mabasi hayawezi kuingia au kuendelea na safari, abiria wanatumia magbasi madogo na daladala kuwafikisha Kituo cha Magufuli.

Kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa, mabasi yanayotoka mikoani yanatakiwa kuingia Stendi ya Magufuli na kushusha abiria, huku yale yanayoanza safari Dar es Salaam yakitakiwa kupakia abiria ndani ya kituo hicho.

Baadhi ya abiria wameeleza kuwa matumizi ya mabasi magodo yamewasaidia kufika kituoni, hasa wale wanaotoka maeneo ya mbali na Mbezi.

Gema Mshana, mkazi wa Masaki amesema eneo la Shekilango lilikuwa rahisi kwake kufika, lakini anashukuru kwa kuwa baada ya kutumia gari dogo kwenda Kituo cha Magufuli, amelipa nauli inayohusisha safari yake ya kwenda mkoani.

Emil Jonas wa Gongo la Mboto amesema kampuni zote zenye ofisi nje ya kituo zinapaswa kuweka utaratibu wa kuwapeleka abiria Magufuli badala ya kuwaambia wakutane kituoni bila msaada wa usafiri.

Hata hivyo, baadhi ya abiria wameonyesha wasiwasi kuhusu muda wa kusubiri mabasi madogo. Luhende Jandika, aliyekuwa akisafiri na familia yake yenye watu 14, amesema alifika kituoni asubuhi akitokea Lindi kuelekea Singida kwa ajili ya mazishi, lakini alilazimika kusubiri muda mrefu hadi basi kuondoka.

Amesema alifika saa tatu asubuhi na kuambiwa gari lao lingeondoka saa sita mchana, hali iliyowaongezea gharama za chakula na mahitaji mengine.

Ameomba kampuni za mabasi kupanga ratiba vizuri ili abiria wanaofikishwa kituoni kwa mabasi madogo wasikae muda mrefu kusubiri mabasi waliyoahidiwa.

Katika utekelezaji wa utaratibu huo, huduma za usafiri wa bodaboda pia zimetajwa kuwa sehemu ya kuwasaidia abiria wanaofika au kuondoka Kituo cha Magufuli.

Bodaboda wanaruhusiwa kubeba abiria pamoja na mizigo yao, hasa katika maeneo yanayohitaji usafiri wa haraka kuelekea au kutoka kituoni.

Hata hivyo, huduma hizo zinatakiwa kuendeshwa kwa kuzingatia taratibu za kituo na usalama wa abiria.

Bodaboda hawatakiwi kuingia maeneo yasiyoruhusiwa ndani ya kituo, bali kuwapokea au kuwashusha abiria katika maeneo yaliyopangwa.

Utaratibu huo unalenga kuwasaidia abiria wanaotumia usafiri wa mabasi, hasa wale wenye mizigo au wanaotoka maeneo ambayo hayana usafiri wa moja kwa moja hadi Kituo cha Magufuli.

Kwa upande mwingine, Chalamila amewataka madereva wa mabasi kukataa maagizo kutoka kwa waajiri wao ya kupakia au kushusha abiria nje ya Kituo cha Magufuli.

Amesema dereva atakayelazimishwa kufanya hivyo anapaswa kukataa kwa kuwa utekelezaji wa agizo la Serikali ni wa lazima.

“Madereva ambao watalazimishwa na mabosi wao kupakia abiria nje ya stendi wakatae, la sivyo wataishia gerezani,” amesema.

Amesema hatakuwa tayari kufanya mazungumzo na wamiliki wa mabasi kuhusu kubadili agizo hilo, akisisitiza kuwa ni msimamo wa Serikali.

Abiria katika kituo Kikuu Cha Mabasi Cha Magufuli kilichopo Mbezi Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam wakiwa wanashushwa katika magari madogo kwa ajili ya kuanzia safari katika kituo hicho.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Mawasiliano kwa Umma wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa), Mustapha Mwalongo amesema wamiliki hawajakataa kutekeleza agizo hilo.

Amesema Taboa imeandika barua kwa Mkuu wa Mkoa ikiomba kukutana naye kwa ajili ya majadiliano, kwa kuwa uamuzi huo haukushirikisha chama hicho.

Katika utekelezaji huo, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando amesema Serikali imeweka vituo vinne vya ukaguzi ili kudhibiti mabasi yanayoweza kukiuka agizo hilo.

Ametaja vituo hivyo kuwa Kiluvya, Goba Njia Nne, Shekilango na Barabara ya Sam Nujoma.

Amesema tangu Agosti 17, 2026, yeye pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya wamekuwa wakifanya ukaguzi katika maeneo mbalimbali, hasa Shekilango.

Kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Serikali pia imeagiza hifadhi za barabara ziendelee kuwa wazi na hatua zichukuliwe kwa kampuni zinazopakia abiria katika maeneo yasiyoruhusiwa.

Msando amesema Jeshi la Polisi limepewa jukumu la kukagua mabasi yanayoenda mikoani kabla hayajaanza safari, huku ukaguzi huo ukifanyika ndani ya Kituo cha Magufuli.

Abiria, wafanyabiashara wanufaika

Baadhi ya wafanyabiashara wadogo katika Kituo cha Magufuli, wakiwemo wamachinga, wabeba mizigo na wapiga debe, wameipongeza Serikali kwa kusimamia matumizi ya kituo hicho.

Wamesema awali baadhi ya mabasi yalikuwa yakipita moja kwa moja bila kupakia au kushusha abiria, hali iliyopunguza wateja na mapato yao.

Mbunge wa Kibamba na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema kituo hicho kina uwezo wa kuhudumia zaidi ya abiria 33,000 kwa siku, lakini kwa sasa kinahudumia takribani 16,000.

Amesema kuna zaidi ya kampuni 40 za mabasi na kutotumia kituo hicho kumekuwa kukiiingizia halmashauri hasara ya zaidi ya Sh2 bilioni kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Kairuki, kituo hicho pia kinatoa ajira kwa zaidi ya watu 7,000, wakiwemo mamalishe, wauza tiketi na wabeba mizigo.

Bandari ya Mtwara inavyofungua fursa kiuchumi, mizigo ikiongezeka

Maboresho ya Bandari ya Mtwara yameanza kuleta mabadiliko katika shughuli za usafirishaji na biashara huku ongezeko la shehena likifungua fursa kwa wananchi, madereva, wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali.

Mabadiliko hayo yanatokana na uwekezaji unaofanywa na Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), ukiwamo upanuzi wa magati, kuongeza mitambo ya kisasa na kuboresha miundombinu inayorahisisha meli na magari kuhudumiwa kwa wakati.

Bandari hiyo sasa inapokea shehena mbalimbali, zikiwamo magari makubwa, vifaa vya ujenzi wa miradi ya kimkakati, saruji, mafuta, makaa ya mawe, mbaazi na korosho. Baadhi ya mizigo hiyo husafirishwa kwenda nchi jirani za Malawi, Zambia, Zimbabwe, Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Msumbiji.

Mamalishe wa eneo la bandarini, Rehema Mputa, anasema maboresho ya bandari yamebadili biashara yake na kuongeza kipato.

Anasema awali alikuwa akitumia kilo moja ya ngano kutengeneza chapati kwa siku, lakini sasa anatumia kilo nne na zote zinaisha.

“Yaani mimi kipindi hicho biashara ilikuwa ngumu sana hapa, lakini mpaka leo nimemsomesha mtoto wangu amemaliza kidato cha nne kwa fedha hizihizi za mamalishe,” anasema.

Rehema anasema ongezeko la biashara limemwezesha pia kuwekeza katika kilimo cha mazao mbalimbali, ikiwamo korosho, kwa kuwa na uwezo wa kuwalipa wakulima.

Anasema anaomba maboresho ya bandari yaendelee kwa sababu kuongezeka kwa shughuli kunawapa wananchi fursa zaidi za kujipatia kipato.

Naye kiongozi wa madereva bodaboda katika eneo la matangi ya mafuta bandarini, Issa Mchika, anasema shughuli za bandari zimeongeza abiria na kipato kwa madereva.

“Kiukweli, ujio wa bandari umetusaidia sana sisi wananchi, hususan sisi madereva bodaboda,” anasema.

Mchika anasema uwepo wa depo, magari ya mizigo na magari ya mafuta umeongeza shughuli za usafiri, huku wageni wanaokuja Mtwara wakitumia hoteli, migahawa na huduma za bodaboda.

Anasema awali wananchi wengi, wakiwamo madereva na mama lishe, walitegemea zaidi msimu wa korosho, lakini ongezeko la shughuli za bandari limeleta biashara katika kipindi kirefu zaidi.

Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara, Hekima Ngezi, anasema bandari hiyo iliyoanzishwa mwaka 1950 imeboreshwa kwa kuongeza uwezo wa kuhudumia meli na shehena kubwa.

Ngezi anasema awali Bandari ya Mtwara ilikuwa ya msimu, ikitegemea zaidi karanga na baadaye korosho, lakini Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan iliona umuhimu wa kuiongezea uwezo ili ifanye kazi kwa ufanisi mwaka mzima.

Anasema gati zimeongezwa kutoka tatu hadi nne, huku gati moja likiwa na urefu wa mita 300 na kina cha maji cha mita 13, hali inayowezesha meli kubwa kutia nanga na kupakia au kushusha shehena nyingi zaidi.

“Mpaka sasa, Bandari ya Mtwara inahudumia shehena ya mafuta, korosho, makaa ya mawe, mbaazi na saruji na tunahudumia magari makubwa. Kuanzia Februari mwaka huu hadi sasa, tumehudumia meli 23 na magari 6,390,” anasema.

Anasema saruji kutoka Kiwanda cha Dangote husafirishwa kwenda Zanzibar, Comoro na Msumbiji kwa ajili ya miradi ya Gesi Asilia (LNG).

Ngezi anasema Serikali inaendelea kujenga gati jipya katika eneo la Kisiwa Mpangawe/Kisiwa Mgao, lenye urefu wa mita 300 na kina cha maji mita 15. Ujenzi wake umefikia asilimia 44 na unatarajiwa kukamilika mwakani.

“Bandari hii au gati hili ni maalum kwa ajili ya kusafirisha mizigo michafu. Kwa hiyo, mizigo yote ile ambayo ina asili ya vumbi kama saruji pamoja na makaa ya mawe na aina nyingine itaweza kupelekwa au kuhudumiwa katika gati hilo jipya,” anasema.

Anasema gati hilo litaongeza uwezo wa bandari kuhudumia shehena nyingi zaidi, akieleza eneo la Kisiwa Mgao lina uwezo wa kuhudumia tani 100,000 kwa pamoja.

Kwa mujibu wa Ngezi, zaidi ya magari 6,000 yaliyohudumiwa bandarini tangu Februari yameelekezwa katika nchi zinazozunguka Tanzania, zikiwamo Malawi, Msumbiji, Zambia, Zimbabwe, DRC, Burundi na Rwanda.

Anasema lengo la TPA ni kuendelea kuongeza uwezo wa Bandari ya Mtwara ili iweze kuhudumia wateja wengi zaidi, akisisitiza kuwa mitambo bora na ya kisasa ni muhimu katika kuongeza ufanisi wa upakiaji na upakuaji wa shehena.

Kiungo cha Ushoroba wa Kusini

Ngezi anasema Bandari ya Mtwara ipo katika Ushoroba wa Kusini unaounganisha mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma, hivyo ina nafasi muhimu katika kukuza biashara ya ndani na kuvuka mipaka.

Anasema malengo ya TPA ni kuhakikisha bandari hiyo inakuwa kiunganishi na chachu ya kukuza ushoroba huo, ambako mizigo itatoka Mtwara kupitia Lindi na Ruvuma hadi Bandari ya Mbamba Bay na baadaye kwenda Malawi.

“Kwa hiyo malengo ya mamlaka ni kuhakikisha Bandari ya Mtwara inakuwa kiunganishi na chachu ya kukuza ushoroba wa kusini ambapo mizigo yetu itatoka hapa Bandari ya Mtwara ikipitia mikoa ya Lindi na Ruvuma mpaka Bandari ya Mbamba Bay, ambapo katika bandari ile mizigo hiyo itaweza kuvuka kwenda nchi jirani ya Malawi,” anasema.

Anasema kuimarika kwa ushoroba huo kutachochea biashara katika mikoa ya kusini na kuongeza fursa kwa wananchi na wafanyabiashara.

Ngezi anasema Bandari ya Dar es Salaam ina mzigo mkubwa, hivyo TPA imeona ni muhimu baadhi ya mizigo ipitie Mtwara ili kupunguza mzigo katika bandari hiyo na kutoa huduma kwa wakati.

“Nafuu iliyopo ya kupitishia mizigo katika Bandari ya Mtwara, tunao uwezo wa kuitumikia kwa wakati na kuweza kuokoa muda ambao unatumika katika kuisafirisha mizigo kwenda Burundi, Rwanda, Zambia, Zimbabwe na Malawi,” anasema.

Anasema kutumia Mtwara kunaweza kupunguza muda wa kusafirisha mizigo kwa nchi zinazotumia njia hiyo, huku pia kukiwa na nafasi ya kuchochea shughuli za kiuchumi katika maeneo yanayopitiwa na ushoroba.

Kuhusu fursa zinazotokana na maboresho hayo, Ngezi anasema wananchi wanaozunguka bandari tayari wanaanza kunufaika kutokana na ongezeko la shehena na mahitaji ya huduma mbalimbali.

Anasema ongezeko la magari yanayoingia na kutoka bandarini limeongeza mahitaji ya madereva, hasa wale wanaosafirisha magari na mizigo kwenda nchi jirani.

“Tulipoanza kupitisha shehena ya magari, magari haya yanahitaji madereva. Madereva ambao watayatoa magari haya kwenye yadi zetu, lakini madereva watakayosafirisha magari haya kuyatoa Mtwara kuyapeleka nchi husika au kwenye mipaka ya mataifa husika hiyo ni fursa,” anasema.

Kuhusu mradi wa LNG wa Lindi, Ngezi anasema bandari imejipanga kuhudumia vifaa mbalimbali vitakavyotumika katika miradi ya gesi, kwa kutumia mitambo ya kisasa.

“Tunafahamu miradi hii ya gesi lazima itakuwa na shehena ya vifaa mbalimbali ambavyo vitatumika katika uchimbaji wa gesi, sisi tumejipanga mitambo ya kisasa, ambayo ni kitu cha kwanza kabisa, bandari haiwezi kufanya kazi bila mitambo,” anasema.

Anasema bandari ina mitambo ya kupakua na kushusha shehena ambayo inaweza kutumika katika shughuli zinazohusiana na miradi ya gesi.

Kuhusu kuzuia msongamano wa magari, Ngezi anasema bandari imejipanga kutumia Bandari Kavu (ICDs) endapo kutakuwa na ongezeko kubwa la magari au shehena.

Anasema maeneo ya bandari ambayo hayajatumika kikamilifu yanaweza kutumika kuhifadhi mizigo, huku ICD ya Mangachini ikiwa ni miongoni mwa maeneo yanayoweza kusaidia kupunguza msongamano.

Wakala wa Meli wa Joyous Shipping Service Ltd, Esthersia Mallya, anasema mazingira ya Bandari ya Mtwara yamebadilika, huku idadi ya meli ikiongezeka na huduma kutolewa kwa wakati.

“Hapa Mtwara hakuna kabisa,” anasema wakati akizungumzia changamoto ya foleni.

Anasema Serikali na uongozi wa bandari wamefanya juhudi kuboresha mazingira yanayozunguka bandari, ikiwamo barabara zinazorahisisha magari kuingia na kutoka.

“Uboreshaji ambao umefanyika pamoja na mifumo ya namna ya kuhifadhi mizigo, kiasi kwamba mzigo wako utakavyoingia ndivyo utakavyoupata,” anasema.

Mallya anasema hali hiyo ni manufaa kwa wafanyabiashara na mawakala kwa sababu meli zinapofika hupata huduma kwa wakati, hivyo mizigo kushushwa na kupakiwa bila kuchelewa.

Anashauri wafanyabiashara na mawakala ambao wamekuwa wakitegemea zaidi Bandari ya Dar es Salaam kuangalia uwezekano wa kutumia Mtwara kutokana na kutokuwapo kwa foleni kubwa.

Madereva wachangamkie fursa

Wakala wa Baruti International Limited, Abdulrahman Upete, anasema Bandari ya Mtwara imewekeza katika mitambo mbalimbali inayorahisisha utendaji wa kazi na kuzipa nafuu Bandari za Dar es Salaam na Tanga.

Anasema kampuni yao, yenye ofisi Dar es Salaam na Tanga pia inatarajia kuwa na tawi Unguja, imeweza kuwahudumia wateja wake kwa kutumia Bandari ya Mtwara.

Aidha, Upete anasema maboresho hayo yameifanya Mtwara kuwa kiungo kwa nchi zinazozunguka Tanzania, zikiwamo Msumbiji, Malawi, Congo na Zambia, huku ikianza kupokea mizigo ya magari, mashine na vifaa vya ujenzi kutoka mataifa mbalimbali.

Anashauri Serikali kuendelea kuwekeza katika mitambo na miundombinu ili kuongeza ufanisi wa bandari.

Anasema uwekezaji zaidi utaifanya Mtwara kuwa lango kuu la kusini katika kuingiza na kusafirisha mizigo kwenda maeneo mbalimbali.

Upete amewataka wadau wa usafirishaji wa magari na mitambo pamoja na wananchi kuchangamkia fursa za udereva na huduma zinazohusiana na usafirishaji.

“Magari mengi yanapita hapa, mahitaji ya madereva yameongezeka, mahitaji ya magari ya kusaidia nayo yanahitajika, kwa sababu mara nyingine yanakuja ‘matrailer’ hapa yanatakiwa magari ya kuvuta,” anasema.

Anasema baadhi ya magari yanayopita Mtwara yanaendelea na safari kwenda nje ya Tanzania, hivyo kuna umuhimu kwa madereva wa eneo hilo kupata ujuzi na uzoefu wa usafirishaji wa kimataifa.

Anasema madereva wengi waliopo Mtwara hawana uzoefu wa kuvuka mipaka, jambo linaloweza kuwa changamoto wakati wa kusafirisha magari au mitambo kwenda Malawi, Zambia, Congo na nchi nyingine.

“Kwa hiyo kuna haja ya madereva waliopo hapa Mtwara sasa kuingia vyuoni kama Veta ili kupata uzoefu na ujuzi zaidi kwa sababu unapotoka nje ya mipaka ya Tanzania kuna taratibu zake,” anasema.

Michezo kama kazi kwa vijana wa Tanzania

Kwa miaka mingi, katika jamii yetu, kijana anaposema anataka kuwa mwanamichezo, mara nyingi huulizwa: “Utasoma lini ili upate kazi ya maana?” Mtazamo huu unaonyesha namna ambavyo bado tunauona mchezo kama burudani zaidi kuliko fursa ya kiuchumi.

Lakini katika dunia ya sasa, michezo si burudani pekee; ni sekta inayoweza kuzalisha ajira, kipato, biashara na fursa za uwekezaji.

Kwa vijana wengi wa Tanzania wanaokabiliwa na changamoto ya ajira, kipaji cha michezo kinaweza kuwa mtaji muhimu wa kujiajiri na kujenga maisha bora.

Soka, riadha, mpira wa kikapu, netiboli, ndondi, kuogelea na michezo mingine ina uwezo wa kuwapa vijana fursa za ndani na nje ya nchi.

Hata hivyo, mafanikio katika michezo hayapaswi kutegemea kipaji pekee. Yanahitaji nidhamu, mafunzo, elimu, usimamizi mzuri wa fedha na mipango ya muda mrefu.

Muhimu zaidi, vijana wanapaswa kuelewa kwamba “career in sports” haimaanishi kuwa mchezaji pekee.

Sekta ya michezo inahitaji makocha, waamuzi, waandishi wa habari za michezo, wataalamu wa lishe na mazoezi, wapigapicha, wataalamu wa masoko, wasimamizi wa timu, waandaaji wa matukio, watengenezaji wa maudhui ya kidijitali na wafanyabiashara wa vifaa vya michezo.

Hivyo, hata kijana ambaye hawezi kuwa mwanamichezo wa kulipwa anaweza kujenga taaluma yenye kipato kupitia sekta hiyo.

Kwa Tanzania, hii inapaswa kutufanya tubadili namna tunavyowaandaa vijana wenye vipaji.

Shuleni na vyuoni, michezo haipaswi kutenganishwa na elimu ya ujasiriamali na usimamizi wa fedha.

Kijana mwenye kipaji anapaswa kufundishwa namna ya kutengeneza chapa yake, kutumia mitandao ya kijamii, kusimamia mikataba, kuweka akiba na kuwekeza mapato yake.

Vinginevyo, kipato kikubwa cha muda mfupi kinaweza kupotea bila kujenga maisha ya baadaye.

Serikali, taasisi za elimu na sekta binafsi pia zina nafasi kubwa. Uwekezaji katika miundombinu ya michezo, akademi, ligi za vijana, udhamini na programu za kukuza vipaji unaweza kuifanya michezo kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa vijana.

Aidha, mifumo bora ya kutambua na kuendeleza vipaji inaweza kuwasaidia vijana kutoka mazingira ya kawaida kufikia soko la kitaifa na kimataifa.

Kwa hiyo, ni wakati wa kuacha kumwambia kijana mwenye kipaji cha michezo kwamba “michezo si kazi.” Badala yake, tumwulize: “Unawezaje kubadilisha kipaji chako kuwa taaluma endelevu?”

Kipaji kinaweza kuwa mwanzo wa safari. Lakini elimu, nidhamu, ubunifu na usimamizi mzuri wa fedha ndivyo vinavyoweza kukifanya kipaji hicho kilipie bili leo na kujenga maisha bora kesho.

Zijue mbinu za kujenga utajiri wa muda mrefu

Watu wengi wanapotafuta namna ya kujenga maisha bora ya kifedha, mawazo yao huenda moja kwa moja kwenye kuanzisha biashara, kununua kiwanja, kujenga nyumba au kuweka fedha benki. Hizi zote ni njia nzuri za kutumia na kuhifadhi fedha.

Kununua hisa maana yake ni kununua sehemu ndogo ya umiliki wa kampuni. Unaponunua hisa za kampuni, hata kama ni chache, unakuwa mmoja wa wamiliki wa kampuni hiyo kwa kiwango cha hisa ulizonazo. Kampuni inapokua, kupata faida na kuongeza thamani yake, wewe kama mwanahisa unaweza kunufaika pia.

Jambo muhimu hapa ni kuelewa kwamba uwekezaji kwenye hisa si mpango wa kutajirika kwa siku moja. Ni safari inayohitaji muda, maarifa, nidhamu na uvumilivu.

Fikiria mtu mwenye uwezo wa kutenga Sh100,000 kila mwezi. Badala ya kusubiri mpaka siku moja apate Sh10 milioni ndipo aanze kuwekeza, anaweza kuanza taratibu kwa kiasi anachoweza kumudu. Anaweza kujenga utaratibu wa kuweka fedha pembeni na baada ya kufanya uchambuzi unaofaa, kuwekeza kwenye kampuni zenye misingi mizuri ya biashara.

Baada ya miaka kadhaa, uwekezaji huo unaweza kuwa mkubwa kuliko alivyotarajia mwanzoni. Hii ni kwa sababu utajiri wa muda mrefu haujengwi tu na ukubwa wa fedha uliyoanza nayo. Mara nyingi unajengwa na nidhamu ya kuendelea kuwekeza.

Mwekezaji wa hisa anaweza kupata faida kwa njia kuu mbili. Njia ya kwanza ni ongezeko la thamani ya hisa. Kwa mfano, kama mtu amenunua hisa kwa Sh1,000 na baada ya muda thamani yake ikafikia Sh1,500, thamani ya uwekezaji wake imeongezeka. Hata hivyo, bei inaweza pia kushuka, ndiyo maana uwekezaji unahitaji utafiti na uvumilivu.

Njia ya pili ni gawio au dividend. Kampuni inapopata faida, inaweza kuamua kugawa sehemu ya faida hiyo kwa wanahisa wake. Hivyo, mtu anaweza kuendelea kumiliki hisa zake huku akipokea gawio pale linapotangazwa na kulipwa.

Hapa ndipo tunapopaswa kubadili mtazamo wetu kuhusu fedha. Watu wengi tunafanya kazi kwa bidii ili kupata fedha, lakini hatua nyingine muhimu ni kujifunza namna ya kufanya fedha tulizopata nazo zifanye kazi.

Changamoto nyingine ni kwamba baadhi ya watu huingia kwenye soko la hisa wakitarajia bei ipande haraka. Wakiona bei imeshuka kwa muda mfupi, wanaingiwa na hofu na kuuza. Wengine wakisikia hisa fulani inapanda, wanakimbilia kununua bila hata kuelewa kampuni inayohusika. kununua hisa hakupaswi kufanana na kubashiri.

Uwekezaji mzuri huanza na maarifa. Ni muhimu kutoweka fedha zote kwenye kampuni moja. Kampuni yoyote inaweza kukutana na changamoto.

Jambo jingine muhimu ni muda. Mtu aliyeanza kujenga uwekezaji akiwa na miaka 25 ana nafasi tofauti na yule anayesubiri mpaka miaka 50, hata kama wote wana kiasi kinachofanana cha kuanzia. Miaka mingi inatoa nafasi kwa uwekezaji kukua na mapato yanayopatikana kuendelea kuongezwa kwenye uwekezaji.

Ndiyo maana vijana wanapaswa kufundishwa mapema kuhusu kuweka akiba na kuwekeza. Elimu ya uwekezaji isiwe jambo tunaloanza kulifikiria tunapokaribia kustaafu. Hata hivyo, uwekezaji wowote una hatari.

Hakuna uhakika kwamba bei ya hisa itapanda au kampuni italipa gawio kila mwaka. Ndiyo maana ni muhimu kujifunza, kufanya uchambuzi na inapohitajika kupata ushauri kutoka kwa wataalamu wenye leseni.

Mwisho wa siku, kujenga utajiri si lazima kuanze na mamilioni ya fedha. Kunaweza kuanza na uamuzi mdogo: kutumia chini ya unachopata, kuweka sehemu ya kipato pembeni, kuwekeza kwa maarifa na kufanya hivyo kwa muda mrefu.