Dar es Salaam. Ili kuhakikisha makundi yote yanashiriki na kunufaika na fursa zinazotokana na uwekezaji nchini, Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum Tanzania (Tiseza) imeingia makubaliano na Ella Foundation kutumia mifuko inayozalishwa na watu wenye ulemavu wa kusikia kama zawadi kwa wawekezaji wanaofika nchini.
Mifuko hiyo inazalishwa na watu wenye uziwi kupitia ujuzi wanaoupata katika taasisi hiyo ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha kujitegemea na kuwapatia soko la uhakika la bidhaa zao.
Mkurugenzi wa Tiseza, Hilead Teri anasema ushirikiano huo ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la mamlaka kuhakikisha fursa za uwekezaji zinawafikia Watanzania wote wakiwamo watu wenye mahitaji maalumu.
Anasema miongoni mwa bidhaa zinazozalishwa na watu hao ni mifuko yenye ubora ambayo sasa Tiseza itakuwa ikinunua na kuitumia kama zawadi rasmi kwa wawekezaji wanaokuja nchini.
“Tutakuwa washirika wao wa kununua bidhaa ambazo zimetengenezwa na watu wenye makundi maalumu. Mfano ni mifuko hii ambayo tutaendelea kuitumia na kuwapatia wawekezaji mbalimbali,” anasema.
Kwa mujibu wa Teri, hatua hiyo inalenga kutoa soko endelevu kwa bidhaa huku ikiwezesha taasisi za Serikali kutumia mahitaji yao ya kawaida kuchochea matokeo chanya katika jamii.
Anasema awali Tiseza imekuwa ikitumia bidhaa zinazozalishwa nchini, ikiwamo korosho na mvinyo kama sehemu ya zawadi kwa wawekezaji hivyo kuongeza bidhaa zinazotengenezwa na watu wenye mahitaji maalumu kutasaidia kupanua fursa hizo.
“Tumekuwa tukitumia bidhaa za Tanzania kama korosho na mvinyo kwa wawekezaji. Sasa tutaongeza bidhaa hizi ambazo zimetengenezwa na watu wenye mahitaji maalumu. Hatua hii itawasaidia kupata soko endelevu la bidhaa zao na kuongeza fursa za kiuchumi,” anasema.
Anasema ushirikiano huo pia unaonyesha namna taasisi zinavyoweza kutumia shughuli zao za kawaida kusaidia makundi maalumu, huku ukichochea ubunifu, ujuzi na maisha endelevu kwa vijana.
Teri anasema Tiseza inalenga kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu na Ella Foundation katika kuunga mkono na kutangaza ubunifu na ujuzi wa watu wenye mahitaji maalumu.
“Tutaangalia katika sera zetu kwani kuna baadhi ya kazi zinaweza kufundishwa hivyo tutawashawishi wawekezaji kuwa wanapotoa ajira wawafanye watu wenye ulemavu kuwa sehemu ya wanufaika,” anasema.
Kwa upande wake, mwanzilishi wa Ella Foundation, Esther Jaswant anasema ulemavu haupaswi kuwa kikwazo kwa mtu kupata uhuru wa kiuchumi, hivyo taasisi hiyo imeanzisha miradi ya uzalishaji wa bidhaa zenye ubora ili kuwasaidia viziwi kujitegemea.
“Moja ya miradi yetu ni kuzalisha bidhaa zenye ubora ili kusaidia viziwi kujikwamua kiuchumi. Fursa tuliyopata inatoa ujumbe kwamba Tanzania inawathamini watu wenye ulemavu, kwani mifuko yetu ina nembo inayoonyesha imetengenezwa na nani,” anasema.
Aliongeza kuwa matumizi ya bidhaa hizo na Tiseza kama zawadi kwa wawekezaji ni fursa muhimu ya kuitangaza kazi inayofanywa na viziwi, huku ikiwapatia soko na kuongeza thamani ya ujuzi wanaoupata.

























































