Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Pande mbili utekelezaji agizo la Chalamila kuhusu malori

By admin
August 19, 2026 3 Min Read
Comments Off on Pande mbili utekelezaji agizo la Chalamila kuhusu malori

Dar es Salaam. Agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila la kutaka malori yasiegeshwe kwenye hifadhi za barabara limeendelea kuzua mjadala, huku baadhi ya wananchi wakiliunga mkono na wengine wakionesha shaka kuhusu utekelezaji wake.



Baadhi ya wanaounga mkono wamesema hatua hiyo itasaidia kurejesha utaratibu wa matumizi ya barabara na kupunguza msongamano wa magari, huku wenye shaka wakisema Serikali ilipaswa kujadiliana na wadau wa malori kabla ya operesheni.

Agosti 11, 2026, Chalamila aliliagiza Jeshi la Polisi kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kuendesha operesheni ya kuwaondoa madereva wanaoegesha malori kwenye maeneo yaliyotengwa kwa matumizi mengine.

Kwa mujibu wa Chalamila, hatua hiyo inalenga kurejesha nidhamu ya matumizi ya barabara na kukabiliana na uholela unaochangia msongamano na usumbufu kwa watumiaji wengine wa miundombinu ya usafiri jijini.

Kutokana na agizo hilo, Agosti 18, 2026 Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa), Elias Lukumay alitishia kusitisha shughuli za usafirishaji endapo Serikali haitashughulikia changamoto zinazowakabili wanachama wake.

“Mnatupitisha kwenye njia ngumu kila kukicha, lakini kero ni zilezile. Tunaamini maelewano ndiyo njia bora. Yakishindikana, tuko tayari kuyaegesha malori hadi hapo tutakapokubaliana,” alisema Lukumay.

Hata hivyo, tayari Tanroads wameshaanza utekelezaji wa oparesheni hiyo.

Akizungumza na Mwananchi, Meneja wa Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam, Alinanuswe Kyamba, amesema wameshaianza operesheni hiyo na wamekamata malori kadhaa yaliyokutwa yameegeshwa katika hifadhi ya barabara.

“Ni kweli tumekamata malori kadhaa yaliyokuwa katika hifadhi za barabara. Ni vigumu kukupa takwimu hapa labda nitafute kesho asubuhi (Agosti 20) nitakuwa na idadi kamili,” amesema.

Mkazi wa Dar es Salaam, Mfaume Ramadhani amesema utekelezaji wa agizo hilo utakumbana na vikwazo iwapo Serikali haitadhibiti utoaji wa vibali vya bandari kavu katikati ya jiji.

Malori yakiwa yameegeshwa kando ya barabara ya Mandela eneo la Tabata TOT hadi Tabata Mwananchi leo, Agost 19, 2026, licha ya maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kutaka yasiwepo magari yanayoegeshwa pembezoni mwa barabara. Picha na Said Powa

“Ili kumaliza tatizo, vibali vya ICD vinapaswa kudhibitiwa na shughuli nyingi zihamishiwe nje ya mji. Hifadhi za barabara zinapaswa kubaki kwa matumizi ya watembea kwa miguu,” amesema.

Mkazi wa Temeke, Shaaban Ibrahim amesema baadhi ya bandari kavu zimejaa makasha kiasi cha kukosa maeneo ya kupokelea mizigo, jambo linalochangia malori kuegeshwa barabarani.

Amesema mazungumzo kati ya Serikali na wadau ni muhimu ili kupata suluhisho linalotekelezeka bila kuathiri shughuli za usafirishaji na biashara zinazotegemea huduma za malori.

Mkazi wa Tabata,  Muhidini Athuman amesema operesheni hiyo itasaidia kuondoa usumbufu kwa watembea kwa miguu ambao mara nyingi hulazimika kutumia sehemu za magari kutokana na njia kuzibwa na malori.

Jabiri Khatibu amesema malori yanachangia msongamano katika baadhi ya barabara za jiji, hivyo ni muhimu kutengwa maeneo maalumu ya maegesho na shughuli za usafirishaji kuhamishwa pembezoni mwa mji.

Mwananchi ilipita katika barabara mbalimbali zikiwamo za Mandela na Nyerere na kubaini baadhi ya malori yaliyokuwa yemegeshwa katika kinyume cha utaratibu yameondolewa.

Maeneo ya Sokota, Uwanja wa Taifa kuelekea bandari ambayo siku za nyuma yalikuwa sehemu ya kuhifadhi malori, hali imekuwa tofauti baada ya hifadhi ya barabara katika sehemu hizo kuonekana hazina magari.

Hata hivyo, baadhi yameendelea kuwepo hasa katika maeneo yenye bandari kavu, yakiwa yameegeshwa katika hifadhi ya barabara.

Miongoni mwa maeneo ambayo yameonekana malori yakiegeshwa ni Tabata TOT, Matumbi, Mchicha, Mabibo Msikiti, ingawa kulionekana maofisa wa Tanroads na polisi wakiyashughulikia.

Makamu Mwenyekiti wa Tatoa, Rahim Dossa amesema chama hicho kimeitwa katika kikao kazi cha wadau kujadili suala hilo.

Amesema pia viongozi wa Serikali wameanza kusikiliza hoja zao na kuahidi kuzifanyia kazi changamoto zilizowasilishwa.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Saratani ya mlango wa kizazi yaongoza kwa vifo Tanzania

Next

Polisi Maswa yatoa msaada kwa wagonjwa

Recent Posts

  • Wasira awataka wana-CCM kuhakiki taarifa za mitandaoni
  • DIT MWANZA YAONESHA NGUVU YA TEKNOLOJIA NA UZALISHAJI WA BIDHAA TANGA
  • Mgambo wazunguka soko la mitumba, wafanyabiashara ‘wafungiwa’ biashara
  • Polisi Maswa yatoa msaada kwa wagonjwa
  • Pande mbili utekelezaji agizo la Chalamila kuhusu malori

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme