ACT yalaani Gazeti la MwanaHALISI kusitishiwa leseni
Dar es Salaam. Chama cha ACT- Wazalendo kimepinga uamuzi wa Serikali wa kusitisha kwa miezi sita leseni ya Gazeti la MwanaHALISI kikisema hatua hiyo inakiuka uhuru wa habari na haki ya umma kupata taarifa.
Katika taarifa yake ya Jumatano, Agosti 19, 2026, ACT Wazalendo kimekosoa uamuzi huo na kuitaka Serikali kuondoa kusitishwa kwa leseni hiyo.
“ACT Wazalendo tunalaani kwa nguvu zote uamuzi wa Serikali kusitisha kwa miezi sita leseni ya uchapishaji na usambazaji wa Gazeti la MwanaHALISI kuanzia Agosti 19, 2026,” imeeleza taarifa hiyo iliyosaniwa na waziri kivuli wa habari, mawasiliano na teknolojia ya habari wa chama hicho, Shangwe Shao.
Chama hicho kimeeleza kinautambua wajibu wa vyombo vya habari kuzingatia weledi, lakini kimesisitiza kuwa makosa ya kitaaluma yanapaswa kushughulikiwa kwa namna inayolinda uhuru wa habari, haki ya kusikilizwa na masilahi ya umma.
“Serikali imejipa mamlaka ya kumchunguza, kumsikiliza na kumuadhibu mtoa huduma wa habari,” imeeleza ACT- Wazalendo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Serikali kupitia Idara ya Habari Maelezo, leseni ya MwanaHALISI imesitishwa kwa miezi sita kuanzia Agosti 19, 2026, baada ya kukiuka sharti la tatu la leseni linalovitaka vyombo vya habari kuzingatia Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, na Kanuni zake za mwaka 2017.
Maelezo imeeleza kosa lilihusisha toleo namba 571 la Agosti 6 hadi 12, 2026, lililokuwa na habari yenye kichwa “Nchimbi agoma kujiuzulu” katika kurasa za kwanza, pili na tatu.
Idara hiyo imedai habari hiyo haikuzingatia usahihi, mizania na uthibitishaji kabla ya kuchapishwa.
Maelezo pia imesema katika ukurasa wa pili wa gazeti hilo lilichapisha picha ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, lakini maelezo chini ya picha yalimtaja kuwa Makamu wa Rais, Dk Emmanuel Nchimbi.
Idara imetaja hilo kuwa dosari ya mwandishi na wahariri.
*Kuhusu mizania*
Maelezo imesema habari hiyo ilijikita katika madai ya kujiuzulu kwa Nchimbi bila kuonyesha kuwa yeye alihojiwa au kutoa kauli kuhusu suala hilo.
Aidha, imesema madai yaliyodaiwa kutolewa na Makonda hayakuambatana na uthibitisho wa moja kwa moja kutoka kwake.
Idara pia imesema mwandishi hakufanya jitihada za kuwahoji viongozi wa CCM au wajumbe wa kikao kilichodaiwa kujadili suala hilo, akiwamo Katibu Mkuu, Katibu wa Itikadi na Uenezi au Ofisa Habari, ili kuthibitisha taarifa zilizotokana na vyanzo fiche.
Uamuzi huo, kwa mujibu wa Maelezo, umezingatia pia mwenendo wa gazeti hilo kurudia makosa baada ya kuonywa.
ACT Wazalendo, hata hivyo, imesema hatua hiyo inapaswa kupingwa kwa kulinda nafasi ya vyombo vya habari katika demokrasia.
“Uhuru wa habari na haki ya kupata, kutoa na kupokea taarifa ni nguzo za Katiba, demokrasia na uwajibikaji wa Serikali. Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 na sheria nyingine zinazompa mamlaka makubwa Mkurugenzi wa Habari juu ya vyombo vya habari zinapaswa kufutwa, na kuondoa vifungu vinavyokandamiza uhuru wa habari,” ACT Wazalendo imeeleza.
