Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Mgambo wazunguka soko la mitumba, wafanyabiashara ‘wafungiwa’ biashara

By admin
August 19, 2026 3 Min Read
Comments Off on Mgambo wazunguka soko la mitumba, wafanyabiashara ‘wafungiwa’ biashara

Musoma. Wafanyabiashara katika soko la mitumba la Mlango Mmoja, Kata ya Nyasho, Manispaa ya Musoma, wameingia katika taharuki baada ya askari wa Jeshi la Akiba la manispaa hiyo, maarufu mgambo, kuzingira soko hilo na kuwazuia kufungua vibanda vyao.

Hali hiyo imetokea leo, Jumatano, Agosti 19, 2026, baada ya wafanyabiashara hao kufika sokoni asubuhi kwa ajili ya kuendelea na biashara zao, lakini wakawakuta mgambo wametanda katika maeneo mbalimbali ya soko.

Wafanyabiashara hao wamesema walizuiwa kufungua vibanda vyao hadi watakapolipa Sh10,000 kila mmoja, kiasi kilichoelezwa kuwa ada ya maombi ya kibanda.



Baadhi yao wamesema wameshangazwa na hatua hiyo kwa kuwa walitumia fedha zao kujenga vibanda hivyo baada ya manispaa kutenga eneo hilo kwa ajili ya soko.

“Tunaambiwa tujaze fomu kwa Sh10,000, ambayo ni ada ya maombi. Mbaya zaidi, ukiomba huna uhakika wa kupewa hicho kibanda, wakati tumetumia gharama zetu kujenga vibanda. Huu ni unyanyasaji, tunaomba msaada,” amesema Jenifa Yusufu.

Amesema pia kumekuwa na ongezeko la kodi ya vibanda bila kuzingatia hali ya biashara, jambo analodai linawaweka katika wakati mgumu, hasa kwa kuwa wengi wao hutegemea mikopo.

Baadhi ya wafanyabiashara wa Soko la Mitumba la Mlango Mmoja, Manispaa ya Musoma, wakiwa nje ya soko hilo baada ya mgambo kuwazuia kufungua vibanda vyao hadi walipie Sh10,000 kwa ajili ya maombi ya upangaji. Picha na Beldina Nyakeke.

Kwa mujibu wa Jenifa, awali walilipa Sh12,000 kwa mwezi kama kodi ya kibanda, lakini Aprili mwaka huu ilipanda hadi Sh15,000 na sasa imefikia Sh24,000.

Mfanyabiashara mwingine, Yohana Simon, amesema wanaendelea kutozwa kodi na tozo, huku soko likikosa baadhi ya huduma muhimu, ikiwamo vyoo vya kutosha.

“Hapa mazingira ni sisi ndio tunapambana nayo. Hivi vibanda tumejenga kwa gharama zetu. Hatuna huduma ya ulinzi kutoka manispaa na hata choo kipo kimoja, ambacho hakikidhi mahitaji,” amesema.

Katibu wa soko hilo, David Machera, amesema wafanyabiashara walifikisha malalamiko yao kwa mkuu wa mkoa wa Mara, ambaye ameahidi kukutana nao kesho kusikiliza na kujadili changamoto hiyo.

“Leo tumekuja tunakuta mgambo wamezingira eneo lote, wakati tuna ahadi ya kukutana na Mkuu wa Mkoa kesho. Tuna mikopo tunatakiwa kurejesha, unapotuzuia kufanya biashara unategemea nini?” amehoji.

Mbunge wa Musoma Mjini (CCM), Mgore Miraji, alifika sokoni na kuwasiliana na Mkurugenzi wa Manispaa ya Musoma, akimtaka kuwaondoa mgambo ili wafanyabiashara waendelee na shughuli zao.

“Hii si sawa kabisa. Serikali kila siku inatafuta namna ya kuwawezesha watu wake kujiimarisha kiuchumi. Inakuwaje mfanyabiashara anafungiwa kibanda chake? Mkurugenzi, waondoe mgambo wako hapa ili shughuli ziendelee, kisha tutakutana tufanye kikao kama tulivyokubaliana,” amesema.

Mgore amesema malalamiko hayo aliyapokea tangu juzi na jana walikubaliana kufanya kikao pamoja na mkurugenzi, ofisa biashara na wafanyabiashara hao.

Amesema wafanyabiashara hawajapata elimu ya kutosha kuhusu malipo hayo, akieleza kuwa wanapaswa kuwa na namba ya utambulisho wa mlipa kodi ili kusajiliwa katika mfumo wa Serikali wa Tausi na kupewa control namba za malipo.

“Mnatakiwa kusajiliwa kwenye mfumo wa Tausi ili kila mmoja apewe control namba awe analipa kodi yake kama kawaida. Kwa kuwa wote ni wafanyabiashara wenye vibanda hapa, msiwe na hofu kwani hakuna atakayeondolewa,” amesema.

Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Juma Chikoka, amekiri kutokea kwa hali hiyo na kusema ameitisha kikao cha pamoja cha wafanyabiashara, viongozi wao, manispaa na mbunge kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa kudumu.

“Ni kweli hiyo hali imetokea. Tayari tumechukua hatua na hivi tunavyoongea biashara zinaendelea pale sokoni. Lengo la kikao ni kupata ufumbuzi wa kudumu juu ya suala hili,” amesema.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Polisi Maswa yatoa msaada kwa wagonjwa

Next

DIT MWANZA YAONESHA NGUVU YA TEKNOLOJIA NA UZALISHAJI WA BIDHAA TANGA

Recent Posts

  • Wasira awataka wana-CCM kuhakiki taarifa za mitandaoni
  • DIT MWANZA YAONESHA NGUVU YA TEKNOLOJIA NA UZALISHAJI WA BIDHAA TANGA
  • Mgambo wazunguka soko la mitumba, wafanyabiashara ‘wafungiwa’ biashara
  • Polisi Maswa yatoa msaada kwa wagonjwa
  • Pande mbili utekelezaji agizo la Chalamila kuhusu malori

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme