Zanzibar. Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imesema itaendelea kuwa mshirika wa kimkakati katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar kwa kuwawezesha wafanyabiashara, wawekezaji na wajasiriamali kutumia fursa zinazotokana na uwekezaji, maendeleo ya miundombinu na ukuaji wa sekta ya utalii.
Benki hiyo imesema itaendelea kutoa huduma na suluhisho za kifedha zitakazowawezesha wafanyabiashara kupata mitaji, kupanua shughuli zao, kuongeza uzalishaji na kuwekeza katika fursa mpya za biashara, hususan maeneo yenye kasi ya ukuaji wa uchumi kama Kizimkazi.
Kauli hiyo ilitolewa jana Jumapili, Agosti 16, 2026, na Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, wakati wa hitimisho la Tamasha la Kizimkazi mwishoni mwa wiki. Mgeni rasmi katika hitimisho hilo alikuwa Rais Samia Suluhu Hassan.
Sabi alisema benki hiyo inaona fursa kubwa katika mabadiliko yanayoendelea Zanzibar na imejipanga kushirikiana na sekta binafsi kuzigeuza fursa hizo kuwa shughuli endelevu za kiuchumi.
“NBC itaendelea kuwa mshirika wa wafanyabiashara na wawekezaji katika kutumia fursa zinazopatikana Zanzibar, ikiwemo Kizimkazi. Tumejipanga kutoa suluhisho mbalimbali za kifedha zitakazowasaidia kupata mitaji, kukuza biashara zao na hatimaye kuchangia katika ukuaji wa uchumi,” alisema.
Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi (kulia), akizungumza na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba wakati wa hafla ya kuhitimisha Tamasha la Kizimkazi lililoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Sabi alisema uwezeshaji wa kifedha ni muhimu katika kujenga mazingira yanayowezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya uchumi, kwa kuwa ukuaji wa biashara unaweza kuongeza uzalishaji, ajira na fursa za kipato kwa wananchi.
Kauli hiyo imekuja wakati Zanzibar, hususan maeneo ya Kusini, ikiendelea kushuhudia ongezeko la shughuli za kiuchumi linalochochewa na uwekezaji katika sekta ya utalii na maendeleo ya miundombinu.
Akihitimisha tamasha hilo Agosti 14, 2026, Rais Samia Suluhu aliwahimiza wafanyabiashara na wawekezaji kutumia fursa zinazozidi kujitokeza Zanzibar.
Rais Samia alisema Wilaya ya Kusini imepiga hatua kubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita kutokana na ongezeko la uwekezaji, hasa katika sekta ya utalii.
“Wilaya ya Kusini imepata mabadiliko makubwa sana ikilinganishwa na mwaka 2016 kutokana na kuongezeka kwa fursa za biashara zilizotokana na uwekezaji, hususani kwenye maeneo ya utalii. Tamasha la Kizimkazi limekuwa chachu muhimu kuelekea mafanikio hayo. Hivyo, tunawakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji kutumia fursa hizi,” alisema.
Akizungumzia wito huo, Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa NBC, Elvis Ndunguru, alisisitiza nafasi ya sekta binafsi katika kunufaika na mnyororo wa thamani unaotokana na ukuaji wa utalii.
Alisema fursa hizo zinahusisha biashara za huduma, usafirishaji, malazi, chakula na vinywaji, bidhaa za ndani, burudani, sanaa na huduma nyingine zinazohusiana na utalii.
“Dhamira ya NBC ya kushirikiana na wafanyabiashara na wawekezaji ipo wazi na inaakisi umuhimu wa upatikanaji wa huduma na mitaji inayowawezesha wadau wa sekta binafsi kuchangamkia fursa hizo na kuzifanya kuwa shughuli za kibiashara zenye tija na endelevu,” alisema.
Ndunguru alisema ushiriki huo unaonesha dhamira ya NBC kwenda zaidi ya utoaji wa huduma za kifedha kwa kushirikiana na wadau katika masuala yenye umuhimu kwa maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kimazingira.
Katika hafla hiyo, Rais Samia aliwashukuru wadau mbalimbali walioshiriki na kuchangia kufanikisha Tamasha la Kizimkazi, akiwemo NBC kwa mchango wake.



Leave a Reply