Bunge lasogezwa mbele kupisha sherehe za Maulid
Dar es Salaam. Baada ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) kutangaza kuwa Jumanne Agosti 25 Agosti, 2026 itakuwa ni Sikukuu ya Maulid, mkutano wa nne wa Bunge umesogezwa mbele na sasa utaanza Jumatano Agosti 26.
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Agosti 17,2026 na Kitengo cha Mawasiliano na Elimu kwa Umma ya ofisi ya Bunge, imeeleza mabadiliko hayo yamefanyika ili kutoa fursa kwa Waislam wote na Watanzania kwa ujumla kusherehekea sikukuu hiyo ambayo kitaifa itafanyika Jijini Dar es Salaam.
“Kwa mujibu wa hoja iliyotolewa bungeni na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mwigulu Nchemba Juni 26, 2026, mkutano wa nne wa Bunge la 13 umepangwa kuanza siku ya Jumanne Agosti , 2026.”
“ Hata hivyo, kufuatia taarifa ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) kuutangazia umma kuwa siku ya Jumanne Agosti 25 Agosti, 2026 itakuwa ni Sikukuu ya Maulid.”
“Mheshimiwa Spika kwa mamlaka yake chini ya Kanuni ya 35 (4) na (5) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, 2025 anapenda kuwataarifu Waheshimiwa wabunge na umma wote wa Tanzania, kuwa mkutano wa nne wa Bunge utaanza siku ya Jumatano Agosti 26, 2026 saa 3:00 asubuhi,”imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Katika taarifa yake aliyoitoa kwa vyombo vya habari leo Agosti 17, 2026, Katibu Mkuu wa Bakwata, Nuhu Mruma, amesema Maulid hayo yatasomwa usiku wa Agosti 24, katika Viwanja vya Mnazi Mmoja.
Wakati Baraza la Maulid litafanyika Jumanne Agosti 25, 2026 katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) na mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Rais Samia Suluhu Hassan.

