WANANCHI WAFURAHISHWA NA ELIMU YA PBPA KATIKA MAONESHO YA UTAMADUNI

 

Na Matukio Daima Media, MOROGORO

WANANCHI waliotembelea banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) katika Maonesho ya Utamaduni, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu majukumu ya Wakala katika kuratibu uagizaji wa mafuta kwa pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Wananchi hao wamesema maonesho hayo yamekuwa fursa muhimu kwao kupata uelewa kuhusu Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (Bulk Procurement System – BPS), namna mafuta yanavyoagizwa nchini na nafasi ya PBPA katika kuratibu mchakato huo.

Bi. Maria Ngilisho, mmoja wa waliotembelea banda hilo, alisema elimu hiyo imemsaidia kuelewa mchakato wa upatikanaji wa mafuta nchini, ambao awali hakuwa na ufahamu wa kutosha kuuhusu.

“Nimefurahi kupata elimu hii kwa sababu tumekuwa tukitumia mafuta kila siku, lakini hatukuwa tunafahamu mchakato unaofanyika hadi mafuta yanapofika nchini. Sasa nimeelewa kuwa kuna taasisi kama PBPA inayoratibu uagizaji wa mafuta kwa pamoja,” alisema Ngilisho.

Naye, Bw. Michael Maganga, alisema mawasiliano ya ana kwa ana na watumishi wa PBPA yamewapa wananchi nafasi ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi wa moja kwa moja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu mafuta.

“Elimu tunayopata hapa ni muhimu sana kwa sababu tunapata nafasi ya kuuliza maswali yanayotuhusu kama watumiaji wa mafuta na tunapata majibu kutoka kwa wataalamu. Ni vizuri PBPA kuendelea kutumia maonesho haya kuwafikia wananchi,” alisema Maganga.

Kwa mujibu wa PBPA, miongoni mwa majukumu ya Wakala ni kukusanya mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta, kuendesha zabuni za kimataifa za ununuzi wa mafuta kwa wingi, pamoja na kuratibu upokeaji na uwasilishaji wa bidhaa hizo nchini.

Ushiriki wa PBPA katika maonesho mbalimbali ni sehemu ya juhudi za Wakala za kuwaelimisha wananchi kuhusu majukumu yake na nafasi yake katika sekta ya mafuta, huku  ukitoa fursa kwa wananchi kupata ufafanuzi kuhusu mchakato wa uagizaji wa mafuta na hatua zinazochukuliwa kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa hizo unaendelea kuwa wa uhakika nchini.