Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Vyuo vikuu vinavyohitaji mfumo wa ‘Living Lab’ kwenye utafiti

By admin
August 18, 2026 7 Min Read
0

Kwa muda mrefu, Wataalamu na watafiti wamekuwa wakiwaona wananchi wa vijijini kama watu wa kufanyiwa utafiti, badala ya kuwa washirika katika kutafuta suluhisho la changamoto zao.

Mfumo huo umezalisha maarifa muhimu ya kitaaluma, lakini pia umeacha pengo kubwa kati ya kile watafiti wanachogundua katika maabara, na kile ambacho jamii zinahitaji katika maisha yao ya kila siku.

Kupuuza maarifa ya asili ya jamii, watalamu wanasema, kumesababisha gharama kwa Taifa.



Kwa mfano, hatua za kukabiliana na changamoto za mazingira zinaposhindwa kuzingatia uhusiano wa kina uliopo kati ya watu na ardhi yao, huwa zinakosa uhalisia wa kitamaduni unaohitajika ili ziwe endelevu kwa muda mrefu.

Kwa jamii za wafugaji, mfano, maarifa hayahifadhiwi kwenye vitabu, kanzidata au machapisho ya kitaaluma pekee.

Yamejikita katika uzoefu wa muda mrefu wa kutazama mvua, malisho, tabia za mifugo, vyanzo vya maji, magonjwa, uoto wa asili na mifumo ya kijamii inayoamua namna jamii inavyokabiliana na uhaba wa rasilimali.

Kwa mzee wa Kimaasai na mhifadhi wa maarifa ya asili, Ole Morind, maisha ya jamii yake yamejengwa juu ya nguzo tatu; rasilimali za asili, mifugo na jamii.

“Watafiti wanaposhindwa kuelewa namna nguzo hizi zinavyohusiana, wanakosa kutambua kuwa kupambana na umaskini bila kushughulikia mabadiliko ya tabianchi, ni kazi isiyoweza kufanikiwa,”anasema.

Hapa ndipo uzoefu wa Kituo cha Utafiti na mazingira kilichopo Arusha (Arusha Climate and Environmental Research Centre (ACERC) cha Aga Khan University (AKU) unapokuwa na  umuhimu mkubwa unaoweza kubadilisha namna kazi za kitafiti zinavyoweza kufanywa nchini.

Katika kituo hicho, mfumo tofauti umeanzishwa; ni mfumo unaotazama mazingira na watu wanaoishi ndani yake si kama watafitiwa pekee, bali kama sehemu kuu ya kuendesha ubunifu na kutafuta suluhisho la pamoja.

AKU-ACER imekuwa ikijenga mazingira ya utafiti yanayofanana na maabara hai, ambako wanafunzi, watafiti na jamii hujifunza na kutafuta suluhisho kwa changamoto halisi za mazingira.

Falsafa ya ‘Macho Mawili’

Chini ya uongozi wa Dk Emmanuel Sulle, ACERC inaendeleza mfumo unaoelezwa kama “Macho Mawili”, unaolenga kuunganisha maarifa ya kisayansi na maarifa ya asili.

“Falsafa hii inawawezesha watafiti kuuona ulimwengu kwa kutumia jicho la sayansi na jicho la maarifa ya asili kwa wakati mmoja, huku wakitambua kwamba si elimu yote inayopatikana darasani,” anasema Dk Sulle.

Ili kuufanya mfumo huo kuwa sehemu ya taasisi, kituo hicho kimechukua hatua ya kumshirikisha Ole Morind kama mhadhiri msaidizi, akisaidia kuziba pengo kati ya maarifa ya jadi na yale ya kisayansi.

Dk Sulle anaeleza kuwa wazee ni kama miti kwa sababu wamekusanya utajiri wa uzoefu ambao vitabu pekee haviwezi kuutoa.

“Kwa kuishirikisha jamii katika kubuni na kutekeleza utafiti kwa pamoja, kituo kinahakikisha maarifa yanayozalishwa yanajibu mahitaji halisi badala ya kubaki katika maswali ya kitaaluma yasiyogusa maisha ya watu,” anasema.

Mtazamo huo unapata nguvu kutokana na tafiti nyingine zilizofanyika Tanzania.

Utafiti wa mwaka 2023 uliochapishwa katika Tanzania Journal of Development Studies, uliotathmini namna jamii ya Wamasai katika Tarafa ya Ngerengere, Morogoro, inavyokabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ulibaini kuwa wafugaji wanatumia mbinu mbalimbali, ikiwamo kuhamisha mifugo kutafuta malisho, ufugaji unaochanganywa na kilimo na kupunguza idadi ya mifugo wakati wa changamoto.

Watafiti walihitimisha kuwa uwezo wa jamii kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,  unahitaji kutambua na kutumia mifumo ya maarifa ya asili na jadi ya wafugaji.

Utafiti mwingine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam uliofanyika katika Kijiji cha Parakuyo, pia ulionyesha umuhimu wa maarifa ya asili katika usimamizi wa malisho na mifugo wakati mazingira yanapobadilika.

Ushahidi huo unapinga dhana ya zamani kwamba maarifa huwa na uhalali pale tu yanapozalishwa ndani ya chuo kikuu.

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Aga Khan, Dk Tania Bubela, anasema falsafa ya kituo hicho ya kufanya kazi kwa kushirikiana na jamii, ni muhimu katika kipindi ambacho taarifa potofu zinaongezeka.

Kwa mtazamo wake, ushirikiano huo unasaidia kujenga upya imani kati ya wataalamu na wananchi kupitia uwazi katika kuweka ajenda za utafiti na kuweka malengo yanayoshirikishwa.

Kurejesha uhai wa ardhi iliyoharibika

Matokeo ya ushirikiano huo tayari yanaonekana katika mazingira ya Arusha, ambako eneo la kituo limeendelea kuwa na uoto wa kijani hata wakati maeneo yanayokizunguka yakikabiliwa na ukame.

Hali hiyo imewafanya baadhi ya wananchi kujiuliza kituo hicho kinatumia “maajabu” gani, wakati kinachofanyika ni matumizi ya mbinu rahisi zilizobuniwa kwa ushirikiano, ikiwamo kilimo kisichogeuza udongo na urejeshaji wa ardhi iliyoharibika.

Dk Sulle anasema mafanikio makubwa ni pamoja na majaribio na usambazaji wa nyasi aina ya Bana, chakula chenye virutubisho kwa mifugo kinachosaidia kukabiliana kwa wakati mmoja na uhaba wa malisho na uharibifu wa ardhi.

“Kila asubuhi, wanawake wa eneo hili hufika katika ardhi ya kituo, ambayo sasa imekuwa chanzo cha nyasi wanazozihitaji kwa haraka ili kuendeleza maisha yao na mifugo wao,” anasema Dk Sulle.

Ushirikiano huo pia umewasaidia wafugaji kama Ole Morind, ambaye alipoteza asilimia 75 ya mifugo yake kutokana na ukame ndani ya miaka miwili, kubadili na kuanza kufuga mifugo yenye uwezo mkubwa wa kustahimili mazingira magumu.

Hata hivyo, funzo hapa si kwamba maarifa ya jadi yanapaswa kuchukua nafasi ya sayansi ya kisasa.

Badala yake, uzoefu huo unaonyesha umuhimu wa mifumo hiyo miwili kufanya kazi kwa pamoja.

Utafiti wa mwaka 2024 kuhusu wafugaji Wamasai katika Wilaya ya Longido, ulibaini kuwa jamii inatambua kuwa mabadiliko ya tabianchi yanazidi kuwa magumu kutabirika, na kwamba maarifa yao ya jadi pekee yanaanza kushindwa kutoa majibu ya kutosha.

Muhimu zaidi, watafiti walilinganisha mitazamo ya jamii na takwimu za muda mrefu za mvua na joto.

Hili ni fundisho muhimu linaloonyesha kuwa maarifa ya asili hayapaswi kutukuzwa kupita kiasi wala kupuuzwa. Mabadiliko ya tabianchi yenyewe yanabadilisha mazingira ambayo vizazi vilivyopita vilitumia kujenga maarifa hayo.

Kwa hiyo, utafiti imara zaidi ni ule unaoruhusu uchunguzi wa wananchi na vipimo vya kisayansi kujaribiana, kukamilishana na kutoa picha pana zaidi ya tatizo.

Sayansi kueleweka kwa lugha ya jamii

Ushirikishwaji wa jamii unaofanywa na kituo hicho hauishii kwenye kilimo pekee, bali unaingia pia katika afya na mawasiliano.

Kwa kutambua kuwa wafugaji wengi hawajui kusoma na kuandika, ACERC imefanya kazi na viongozi wa jamii, kurahisisha taarifa tata za kisayansi kwa kuzigeuza kuwa alama na michoro inayoweza kueleweka kwa urahisi.

Mfumo huo umetumika pia katika kushughulikia magonjwa ya kitropiki yaliyopuuzwa, ambapo watafiti na wazee wa jamii, wamebuni kwa pamoja alama na misimbo inayotokana na taarifa za Kiingereza na Kiswahili na kutafsiriwa katika Kimasai. Zana hizo zinawawezesha wananchi kutambua dalili za magonjwa na kupata matibabu bila kujali kiwango chao cha elimu.

“Mtazamo huu unahakikisha matokeo ya utafiti mkubwa hayabaki kwenye majarida ya kitaaluma pekee, bali yanatafsiriwa katika lugha rahisi inayoweza kubadilisha maisha na kuwafikia watu waliotengwa na ambao mara nyingi hawana sauti,” anasema Dk Sulle.

Kwa maelezo yake, lugha si suala la mawasiliano pekee; ni suala la utafiti pia.

Anasema, ikiwa jamii haiwezi kueleza uzoefu wake kwa lugha yake, watafiti wanaweza kupoteza maana muhimu wakati wa kukusanya taarifa.

Vilevile, “matokeo yanaporejeshwa kwa jamii kwa Kiingereza cha kitaalamu pekee, wananchi wanaweza kutengwa na uelewa wa utafiti unaohusu maisha yao wenyewe.”

Mtazamo huu unazidi kutambuliwa kimataifa, likiwamo Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi (Unesco), ambalo limekuwa likisisitiza sera za tabianchi na mikakati ya kukabiliana na mabadiliko ya mazingira, inayotumia ushahidi wa kisayansi pamoja na maarifa ya jamii za wenyeji.

Jamii hizo zimejenga kwa vizazi vingi maarifa ya kina kuhusu maeneo yao kupitia uchunguzi wa mvua, joto, bioanuwai na mabadiliko ya ikolojia.

Kwa hiyo, mjadala si kuhusu kuchagua kati ya maarifa ya “kisasa” na “jadi”. Ni kuhusu kujenga msingi mpana na kamili zaidi wa ushahidi.

Mwongozo wa kujenga ustahimilivu wa taifa

Tanzania imeweka lengo la kupunguza uzalishaji wa gesi zinazochangia ongezeko la joto duniani kwa kati ya asilimia 30 na 35 ifikapo mwaka 2030, ikilinganishwa na hali ya kawaida ya shughuli za kiuchumi.

Mpango huo unatambua kilimo, mifugo, misitu, maji na sekta nyingine kama maeneo muhimu ya kujenga uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kazi inayofanywa ACERC inatoa mfano muhimu wa namna Tanzania inavyoweza kubadilisha ahadi hizo kuwa hatua ambazo jamii inaweza kuzimiliki na kuzitekeleza.

Dk Sulle anasema kituo hicho tayari kinafanya jitihada kubwa za kufyonza hewa ukaa kupitia upandaji wa miti na urejeshaji wa mazingira.

Lakini ili mipango hiyo ikue na kufikia maeneo mengi zaidi, taasisi nyingine za utafiti zinapaswa kujifunza kuoanisha mikakati yao na hali halisi ya jamii wanazozihudumia.

Dk Bubela anashauri vyuo vikuu kuwa kiungo kinachounganisha vipaji vya ndani na washirika wa kimataifa, ili kujenga msingi wa ushahidi utakaosaidia utungaji wa sera unaowajibika.

“Kwa kutowachukulia wenyeji kama ‘watu wa porini’, bali kama watu wenye akili na utamaduni uliojengeka kwa kina, kituo kinaonyesha kuwa mifumo ya maisha ya jadi inaweza kutoa somo muhimu kuhusu namna ya kuishi katika mazingira yenye changamoto kubwa,” anasema.

Mtazamo huu pia unavipa vyuo vikuu changamoto ya kutafakari upya maana ya utaalamu katika utafiti.

Mzee anayeweza kutambua mabadiliko ya malisho, tabia za mifugo, upatikanaji wa maji au mabadiliko ya misimu, huenda asiwe na shahada ya kitaaluma, lakini hilo halimaanishi kwamba maarifa yake hayana thamani.

Mtafiti na mtaalamu wa utamaduni, Dk Mrisho Jonas, anasema changamoto ni kujenga mifumo ya utafiti yenye maadili ambayo inaweza kurekodi, kupima na kulinda maarifa hayo bila kuyachukua kutoka kwa jamii au kuwafanya wananchi kuwa vyanzo vya taarifa za bure.

“Jamii inapaswa kuwa na nafasi ya kuamua maswali yanayoulizwa, maarifa yanayoweza kushirikishwa, namna yanavyotafsiriwa na jinsi manufaa yanayotokana na utafiti yanavyogawanywa,” anaeleza.

Anaongeza: “Hapo ndipo utafiti unaweza kuwa na uhalisia wa kweli wa eneo husika.”

Mafanikio ya kituo cha Arusha, yanatoa somo pana kwa mfumo wa elimu ya juu nchini Tanzania.

“Utafiti huwa na uaminifu zaidi pale unapoweza kupita katika uchambuzi mkali wa kisayansi huku ukiendelea kuhusishwa na maisha halisi ya watu ambao unalenga kuyaboresha,” anasema Dk Jonas.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

MAGAZETINI LEO JUMANNE AGOSTI 18/2026,USIPITWE NA GAZETI LA JAMHURI KWA HABARI MOTO MOTO

Next

WATOTO 774,459 WALIO CHINI YA MIAKA 10 KUPATIWA CHANJO YA POLIO MKOANI ARUSHA.

No Comment! Be the first one.

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • Kilomita sita kufuata matibabu zawasukuma Kola kujenga zahanati 
  • FIFA IMEJIHARIBIA YENYEWE KWA MPANGO WA KOMBE LA DUNIA – MKUU WA LIGI KUU YA UINGEREZA
  • SERIKALI YATOA MIEZI SITA KUSAJILI MIUNDOMBINU MUHIMU YA TEHAMA
  • MAONESHO YA YST YAIBUA HAMASA YA SAYANSI KWA WANAFUNZI LINDI
  • Ebola yazidi kutikisa DR Congo, vifo vyafikia 2,378

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme