Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Hichilema ashinda tena urais Zambia, Mundubile aibua shaka

By admin
August 18, 2026 3 Min Read
Comments Off on Hichilema ashinda tena urais Zambia, Mundubile aibua shaka

Dar es Salaam. Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema wa Chama cha United Party for National Development (UPND), ameshinda muhula wa pili wa urais baada ya kupata kura 2,965,326, sawa na asilimia 60.5, katika uchaguzi mkuu uliofanyika Agosti 13, 2026.

Katika matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi Zambia (ECZ), Hichilema amemshinda mpinzani wake mkuu, Brian Mundubile wa National Reconciliation Party for Unity and Prosperity (NRPUP), aliyepata kura 1,856,217, sawa na asilimia 37.8.

Ushindi huo unampa Hichilema fursa ya kuendelea kuongoza Zambia kwa kipindi kingine cha miaka mitano, baada ya kuingia madarakani mwaka 2021 akimshinda aliyekuwa Rais Edgar Lungu.



Hata hivyo, uchaguzi huo umeacha maswali kadhaa kuhusu mwenendo wa mchakato, baada ya ECZ kusimamisha kwa muda uhesabuji kura kufuatia mashambulizi dhidi ya maofisa wa uchaguzi na wizi wa baadhi ya karatasi za kura. Uhesabuji uliendelea baada ya tume kusema hali ya kiusalama imedhibitiwa.

Mundubile ameeleza kutoridhishwa na mchakato huo, akitaka kumbukumbu za kura zilindwe na zihesabiwe kwa uwazi. Pia kumekuwa na taarifa za madai ya vitisho vya kiusalama dhidi yake, ingawa baadhi ya madai hayo hayajathibitishwa kwa uhuru.

Uchaguzi huo ulikuwa na wagombea zaidi ya 10, akiwamo Harry Kalaba, Fred M’membe, Kelvin Fube Bwalya na Richard Silumbe.

Uchaguzi na changamoto za demokrasia

Mchambuzi wa siasa, Absalom Kibanda, amesema malalamiko ya upinzani baada ya uchaguzi si jambo geni katika siasa za Zambia, akisema historia ya nchi hiyo imekuwa na mabadiliko ya madaraka kupitia uchaguzi.

“Zambia kumwondoa madarakani Rais ishazoeleka tangu alipoondolewa mwasisi wa Taifa hilo Kenneth Kaunda. Hichilema naye alimwondoa Rais Edgar Lungu, hivyo kushinda kwa kiongozi aliyekuwepo  madarakani na malalamiko ya upinzani yasingeepukika,” amesema.

Kibanda amesisitiza kuwa malalamiko ya uchaguzi yanapaswa kutazamwa kwa kuzingatia ushahidi na taratibu za kisheria, badala ya kuhitimisha moja kwa moja kuwa mchakato wote haukuwa halali.

Mchambuzi wa siasa za kimataifa, Conrad Masabo, amesema uchaguzi huo unaonyesha safari ya demokrasia ya Afrika ambayo, licha ya changamoto, inaendelea kujengwa.

“Demokrasia siyo mpinzani kushinda uchaguzi, bali ni mifumo ya kisheria ya uchaguzi ya nchi husika kufuatwa kikamilifu,” amesema.

Amesema hatua ya ECZ kusimamisha uhesabuji kwa muda ili kushughulikia changamoto za kiusalama inaonyesha umuhimu wa taasisi za uchaguzi kuchukua hatua pale mchakato unapokumbwa na matatizo.

Hata hivyo, amesema madai yoyote ya kuingiliwa kwa uchaguzi kutoka nchi nyingine yanapaswa kuwasilishwa pamoja na ushahidi ili yaweze kutathiminiwa.

Mtihani wa muhula wa pili kwa Hichilema

Hichilema aliingia madarakani mwaka 2021 baada ya kushiriki katika mbio za urais mara kadhaa. Kabla ya siasa, alikuwa mfanyabiashara na mwekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwamo kilimo.

Alipoingia madarakani, Zambia ilikuwa ikikabiliwa na mzigo mkubwa wa deni, baada ya kutolipa deni lake la taifa mwaka 2020. Serikali yake iliongoza mchakato wa marekebisho ya deni, ikaongeza ushirikiano na taasisi za fedha za kimataifa na kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini, hususan shaba.

Pia ilipanua huduma za kijamii, ikiwamo elimu ya sekondari bila ada.

Hata hivyo, gharama za maisha, ajira, umaskini na changamoto za nishati bado ni miongoni mwa masuala yanayowakabili wananchi.

Kwa hiyo, ushindi wa Hichilema unamweka mbele ya mtihani mwingine mkubwa: kuhakikisha mafanikio ya kiuchumi yanaonekana katika maisha ya Mzambia wa kawaida.

Muhula wake wa pili pia utapimwa katika eneo la demokrasia na uhuru wa kisiasa, ambako Serikali yake imewahi kukabiliwa na ukosoaji kutoka kwa wapinzani na mashirika ya kiraia kuhusu mazingira ya kisiasa, madai ambayo Serikali imekuwa ikiyakanusha.

Kwa Hichilema, ushindi huu si mwisho wa safari ya kisiasa, bali mwanzo wa muhula mwingine ambao utapima uwezo wake wa kuunganisha utulivu wa uchumi, maendeleo na demokrasia.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Bado kiza kimetanda mtoto wa siku moja aliyeibwa Dareda

Next

TBS YALENGA VIFAA BORA NA MATUMIZI SALAMA YA UMEME KUPITIA MEPS

Recent Posts

  • Kibwagizo cha wimbo wa ‘kilio cha mtu mzima’ kilivyotumika kesi ya ardhi
  • Mwili wa mtoto wa miaka saba wakutwa shimoni Tabora
  • WRRB, MIKOA NA HALMASHAURI KUIMARISHA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA
  • Tatoa yatishia kupaki malori | Mwananchi
  • TBS YALENGA VIFAA BORA NA MATUMIZI SALAMA YA UMEME KUPITIA MEPS

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme