Bandari ya Tanga yapaa, wadau wataka bandari kavu
Tanga. Maboresho yaliyofanyika katika Bandari ya Tanga yameongeza ufanisi na kusababisha ongezeko la shehena, meli na abiria, hali iliyowafanya wadau kujadili uanzishwaji wa bandari kavu ili kupunguza msongamano na kuboresha huduma.
Maboresho hayo yanahusisha kuongeza kina cha bandari kutoka mita tatu hadi 13 pamoja na kupanua na kuboresha eneo lake, uwekezaji ulioongeza uwezo wa kuhudumia meli na shehena.
Leo Jumanne Agosti 18, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dk Batilda Burian amesema katika mwaka wa fedha 2025/26, bandari ililenga kuhudumia tani 1,643,363, lakini hadi Juni 2026 imehudumia takribani tani milioni 1.7.
Amesema pia ilipangiwa kuhudumia meli 364, lakini imehudumia 616, sawa na asilimia 196 ya lengo. Kwa abiria, amesema ililenga 59,990 na kufikia 110,356 hukju mapato, lengo lilikuwa Sh85 bilioni, lakini imekusanya Sh 138 bilioni.
Baadhi ya wadau waliokutana kwa ajili ya kujadili mpango wa bandari kavu katika bandari ya Tanga .Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dk Batilda Burian, kulia ni Mwakilishi wa Mkurugenzi wa TPA, Josephat Lukindo na kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salim. Picha na Mbonea Herman.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Joseph Lukindo amesema kupitia Mpango Mkakati wa Miaka Mitano, Bandari ya Tanga inalenga kufikisha uwezo wa kuhudumia tani milioni 4.5 ifikapo 2030/31, sawa na ukuaji wa asilimia 19.8 kwa mwaka.
Amesema bandari kavu itasaidia kuongeza maeneo ya kuhifadhi na kusafirisha shehena nje ya bandari, kupunguza msongamano na kuongeza kasi ya mzunguko wa magari na mizigo.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Meli Tanzania (Tasac), Mohamed Salim amesema ukuaji wa shughuli za Bandari ya Tanga umeongeza mahitaji ya maeneo ya kuhifadhia shehena nje ya bandari.
Amesema maeneo hayo yanaweza kutumika kama “port extension” yakipata ridhaa ya TPA na kuendelezwa na wawekezaji.
Salim amesema Tasac imekutana na wadau Tanga kuhakikisha changamoto za msongamano zinazoshuhudiwa Dar es Salaam hazijirudii, huku akisisitiza kuwa lengo si kuwanyima wadau fursa za biashara, bali kuweka utaratibu unaoendana na ukuaji wa bandari.

