Jaji Warioba atoa kauli sakata la Lissu

Written by

in

Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe, Jaji Joseph Warioba amesema busara za kisiasa zinatakiwa kutumika ili kumwezesha Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia (Chadema), Tundu Lissu anayekabiliwa na kesi ya uhaini kuachiwa huru.

Kauli ya Jaji Warioba imekuja baada ya siku mbili tangu wadau wa siasa na haki za binadamu, kueleza hatua nne za kiutu, ikiwemo kumuachia Lissu, katika kulirejesha Taifa pamoja baada ya matukio ya Oktoba 29, 2025.

Jaji Warioba, mwanasheria na jaji wa siku nyingi na aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzia Novemba 5, 1985 hadi Novemba 9, 1990, amesema hayo katika Mahojiano la Mwandishi wa siku nyingi, Jenerali Ulimwengu.

Amesema mamlaka aliyonayo Rais ya kutoa msamaha kwa wafungwa hayamaanishi kuingilia uhuru wa Mahakama, akieleza kuwa Rais anaweza kutumia mamlaka hayo pale anapoona kuna sababu za msingi za kuponya majeraha au kulinda masilahi mapana ya nchi.

Amesema Mahakama inapomhukumu mtu, hata kwa adhabu kubwa kama kifungo cha muda mrefu au hukumu ya kifo, uamuzi huo unabaki kuwa wa Mahakama, lakini Katiba inampa Rais mamlaka ya kusamehe au kupunguza adhabu katika mazingira yanayofaa.

“Mahakama imeamua, lakini Rais anaweza kusema huyu hapana. Ndiyo maana kila mwaka wakati wa siku ya Uhuru, hutolewa orodha ya watu ambao Rais amewasamehe. Anao uwezo huo,” amesema.

Warioba amesema mamlaka hayo yanaweza kutumika pia katika mazingira ambayo nchi inahitaji kutuliza hali, kuponya majeraha na kufungua nafasi ya mazungumzo, akisisitiza kuwa hatua hiyo si kuingilia Mahakama, bali ni kutumia mamlaka aliyopewa Rais.

“Mbowe alitiwa ndani lakini kwa sababau ya public interest (masilahi ya umma) na mambo yalivyokuwa, wakasema tumtoe ili tuweze kujadiliana, haikutoka sababu kwamba suala hili liko mahakamani hivyo hawawezi kuingilia mahakama.

Akitoa mfano mwingine, amesema: “Mwaka jana wakati vijana wengi walikamatwa na kufikishwa mahakamani kutokana na vurugu za uchaguzi, Rais aliweza kuingilia kwa kuzingatia hali ya nchi na kuamua kuwa waachiliwe.”

“Kwa nini katika hali Lissu ishindikane? Kwa sababu nchi iko katika hali fulani. Unaona ili tuponye majeraha haya, tuzungumze, ni vizuri huyu akaachwa kwa sababu ni mtu muhimu katika haya,” amesema.

Amesema Tanzania haitakuwa nchi ya kwanza kutumia mamlaka hayo, akitoa mfano wa Afrika Kusini wakati wa utawala wa makaburu, ambapo baadhi ya watu walifungwa kutokana na misimamo yao ya kisiasa.

Kauli ya Warioba inaungana na ile iliyowahi kutolewa na Julai 13, 2026 na mwanasiasa mkongwe na mwanazuoni wa uchumi, Profesa Anna Tibaijuka, aliyemshauri Rais Samia Suluhu Hassan kutumia hekima, busara na kuzingatia falsafa yake ya 4R aliyoasisi, kumwachia huru Lissu.

Rais Samia alipoingia madarakani Machi 19, 2021 alitangaza kuongoza kwa kutumia falsafa za R nne, Reconciliation, Resilience, Reforms and Rebuilding, akimaanisha maridhiano, mabadiliko, ustahimilivu na kujenga upya.

Kwa mujibu wa Tibajuka, kuendelea kwa kesi ya Lissu, na simulizi zinazoripotiwa na vyombo vya habari vya kimataifa, vinazidi kuibua hisia tofauti miongoni mwa vijana na kuathiri taswira ya Tanzania pamoja na masilahi yake katika jumuiya ya kimataifa.

Ushauri huo wa Profesa ulienda sambamba na ule uliotolewa na Baraza la Mawaziri (CMAG) wa Jumuiya ya Madola, lililoipa Serikali ya Tanzania muda wa siku 30 kutafuta suluhisho la kisiasa na kisheria kuhusu kesi inayomkabili Lissu. Taarifa hiyo ilitolewa baada ya kikao cha 73 cha dharura cha CMAG kilichofanyika Julai 10, 2026.

Katika mahojiano yake juzi yaliyofanywa na mwanahabari mkongwe Jenerali Ulimwengu na kurushwa na JU Post, Jaji Warioba amejenga hoja yake akirejea namna baadhi ya wanasiasa waliowahi kuwekwa gerezani, lakini Rais Samia akawatoa.

Jaji Warioba alieleza namna Rais Samia alivyomtoa gerezani Mwenyekiti wa zamani wa Chadema, Freeman Mbowe aliyekuwa akikabiliwa na mashitaka ya ugaidi.

“Mbowe aliwekwa ndani, kwa sababu ya masilahi ya umma na mambo yalivyokuwa, akatoka ili kujadiliana,” ameeleza Warioba.

Julai 21, 2021 Mbowe alikamatwa na Polisi jijini Mwanza kisha kusafirishwa hadi Dar es Salaam kwa tuhuma za ugaidi.

Agosti 16, 2021 Mbowe alishtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kwa makosa mbalimbali ikiwemo kufadhili vitendo vya ugaidi na alikaa ndani kwa miezi minane.

Baadhi ya viongozi wa kisiasa walimwomba Rais Samia kumwachia Mbowe, miongoni mwao alikuwa Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe wakitaka kuingilia kati sakata la Mbowe, wakisema Rais anao uwezo huo.

Novemba 13, 2025 akihutubia Bunge Rais Samia Suluhu aliviagiza vyombo vya ulinzi na usalama ikiwemo ofisi ya DPP kuchuja makosa ya vijana wanaoshtakiwa kwa makosa ya uhaini baada ya maandamano yaliyosababisha vurugu wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Rais Samia alisema kwa wale vijana waliofanya makosa kwa kufuata mkumbo waachiwe huru.

“Natambua kuna vijana wengi wamekamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhaini, hawakujua wanachokifanya,”

“Wengine walifuata mkumbo, nikiwa kama mama navielekeza vyombo vya kisheria kuangalia makosa yaliyofanywa na vijana wetu, kwa wale waliofanya mambo kwa kufuata mkumbo na hawakudhamiria kufanya uhalifu wawafutie makosa yao,” alisema Rais Samia.

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *