Jose Chameleone alivyoibua shangwe akitumbuiza kilele tamasha la Kizimkazi
Unguja. Msaanii wa kimataifa kutoka Uganda, Jose Chameleone ameibua shangwe wakati akitumbuiza katika kilele cha tamasha la Kizimkazi.
Katika tamasha hilo linalofanyika leo Agosti 14, 2026 viwanja vya Mwehe Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, msanii huyo amepata fursa kutumbuiza nyimbo zake mbili, Jamila na Mama Mia.
Katika kibao chake cha Jamila, alishuka kutoka katika jukwaa la burudani na kusogelea meza kuu walipokaa viongozi wakuu wa kitaifa kutoka ndani na nje ya Tanzania.
Baada ya kufika katika jukwaa hilo, Rais Samia Suluhu Hassan alishuka kutoka kwenye kiti chake alipokuwa amekaa na kuongea na msanii huyo kisha kucheza naye wimbo huo wa mbona umeniacha.
Baada ya hapo aliondoka huku akiibua shwangwe kubwa kwa wananchi na viongozi waliofurika katika viwanja hivyo kwa ajili ya kusherehekea sherehe hizo.
Katika tamasha hilo pia wasanii wengine wa ndani na nje ya Tanzania wamepata fursa ya kutumbuiza.
Miongoni mwa wasanii hao ni Mrisho Mpoto, Sholo Mwamba, kikundi cha ngoma kutoka Dodoma cha Mahenza na ngoma ya asili ya Kizimkazi ya Shomoo.
