Rais Samia ahimiza amani, utulivu Tamasha la Kizimkazi
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amewahimiza Watanzania, hususan vijana, kulinda amani, usalama na utulivu, akisema maendeleo ya Taifa hayawezi kustawi katika mazingira ya vurugu.
Amesema amani, usalama na utulivu ni nguzo muhimu zinazowezesha uwekezaji, utalii, biashara, ajira na utoaji wa huduma za jamii, ambazo haziwezi kustawi katika mazingira ya vurugu na uvunjifu wa amani.
“Niwaombe Watanzania wenzangu, hususan vijana, msikubali kuharibu amani ya nchi yenu, amani ndiyo kila kitu katika maisha yenu, niwaombe sana mumkatae kwa nguvu zote yeyote asiyeitakia mema Tanzania yetu, tulinde nchi yetu pamoja na Muungano wetu kwa mustakabali wa kizazi kijacho,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema hayo leo Ijumaa, Agosti 14, 2026, alipohitimisha Tamasha la Kizimkazi katika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Zanzibar.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, akiwamo Makamu wa Rais, Dk Emmanuel Nchimbi, Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi, pamoja na viongozi wa vyama vya siasa na taasisi za umma.
Akizungumzia tamasha hilo, Rais Samia amesema limeleta chachu ya maendeleo katika wilaya za Kusini mwa Zanzibar kwa kuchochea biashara na kuongeza fursa za kiuchumi zinazoboresha maisha ya wananchi.
“Ndugu zangu, shangwe siku zote ni nzuri. Zinatuleta pamoja, zinaimarisha mshikamano na umoja, zinatusaidia kutangaza utamaduni wetu na kuvutia wageni. Kazi yetu kama viongozi ni kuhakikisha fursa zinazoibuliwa kupitia shangwe hizi zinawagusa wananchi wetu na tunaziunga mkono,” amesema.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Makamu wa Rais, Dk Emmanuel Nchimbi katika Kilele cha Tamasha la Kizimkazi lililofanyika leo Agosti 14, 2026, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.
Amesisitiza kuwa, Tamasha la Kizimkazi linapaswa kuwa lango la fursa za kiuchumi na chanzo cha ustawi wa wananchi na Taifa kwa jumla.
Amesema Wilaya ya Kusini imepata mabadiliko makubwa ikilinganishwa na mwaka 2016, kutokana na kuongezeka kwa fursa za biashara na uwekezaji.
Ameongeza kuwa ujenzi wa miundombinu na utekelezaji wa miradi mbalimbali umeendelea kuvutia wananchi na wawekezaji kuwekeza katika eneo hilo.
“Rais wa Zanzibar ameweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Karibuni muwekeze. Tunaendelea kujenga uwanja wa michezo ambao utasaidia kufungua fursa mbalimbali wakati wa michuano ya AFCON itakayofanyika Juni 2027,” amesema.
Ameongeza kuwa uwanja huo utatoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza katika huduma zitakazohitajika na wachezaji pamoja na wageni watakaoshiriki mashindano hayo.
Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi amemshukuru Rais Samia kwa kuanzisha Tamasha la Kizimkazi, akisema limekuwa na mchango mkubwa katika kutangaza utalii wa Zanzibar.
“Nawapongeza wananchi wote kwa mwamko mkubwa wa kushiriki tamasha hili na kutumia fursa zilizoambatana nalo, hakika mwaka huu tamasha limefana sana. Limekuwa jukwaa muhimu la kuhamasisha shughuli za maendeleo,” amesema na kuongeza:
Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na msanii wa Uganda, Jose Chameleone wakati wa tamasha la Kizimkazi linalofanyika leo Agosti 14, 2026 viwanja vya Mwehe Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.
“Tumeshuhudia uzinduzi wa miradi mbalimbali ikiwamo ya maji, barabara, elimu, nyumba za makazi na viwanja vya michezo,” amesema.
Rais Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha miradi yote iliyozinduliwa na itakayotekelezwa baadaye inatunzwa na kuendelezwa ipasavyo.

