Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Wimbi la magonjwa ya upumuaji linavyoathiri watoto

By admin
August 18, 2026 3 Min Read
Comments Off on Wimbi la magonjwa ya upumuaji linavyoathiri watoto

Dar es Salaam. Madaktari wamesema kati ya asilimia 50 hadi 70 ya watoto wanaofikishwa hospitalini kwa ajili ya matibabu katika kipindi hiki husumbuliwa na magonjwa ya mfumo wa upumuaji, huku hali ya baridi na vumbi ikitajwa kuchangia kuongezeka kwa matatizo hayo.



Wamesema mbali na watoto, watu wazima nao wameendelea kupata changamoto za mafua na kikohozi katika kipindi hiki.

Magonjwa ya mfumo wa upumuaji yanayoathiri pua, koo, mirija ya hewa na mapafu, yanaweza kusababishwa na virusi, bakteria, vumbi au moshi.

Takwimu za Wizara ya Afya za Julai 2025 hadi Machi 2026 zinaonesha maambukizi ya mfumo wa upumuaji yalikuwa miongoni mwa magonjwa yaliyoongoza kwa wagonjwa waliofika katika huduma za afya.

Kwa watoto walio chini ya miaka mitano, maambukizi hayo yaliathiri wagonjwa milioni 4.46, sawa na asilimia 36.8, huku kwa wenye miaka mitano na zaidi, walioathirika wakiwa milioni 3.46.

Kwa mujibu wa Wizara ya Afya, maambukizi ya mfumo wa upumuaji pia yaliongoza kwa magonjwa yaliyowasumbua wagonjwa waliolazwa, yakifuatiwa na maambukizi ya njia ya mkojo kwa asilimia 9.4 na maambukizi ya ngozi kwa asilimia 3.1.

Takwimu hizo zimetajwa katika Hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka 2026/27.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne, Agosti 18, 2026, Daktari wa Watoto, Sagumo Chotta amesema watoto walio chini ya miaka mitano wanaathirika zaidi kutokana na magonjwa ya mfumo wa upumuaji.

“Matatizo mengi ambayo wazazi wanawaleta watoto hospitalini kwa kipindi hiki ni mafua na kikohozi. Hilo ndilo tatizo kubwa kwa watoto, ingawa wapo baadhi wanaoathirika na nimonia,” amesema Dk Chotta.

Amesema watoto wako katika hatari kubwa ya kuambukizwa kutokana na kukaa katika mikusanyiko, ikiwamo shuleni na wakati wa kucheza.

“Karibu asilimia 50 hadi 70 ya watoto wanaofikishwa hospitali hivi sasa ni kutokana na matatizo hayo. Kundi hili ni rahisi kuambukizwa kwa kuwa huwa kwenye mikusanyiko, hata wanapokuwa shuleni,” amesema.

Dk Yusuph Mneka amesema mazingira yasiyo safi nyumbani pia yanaweza kuwaweka watoto katika hatari ya kupata maambukizi yanayosababishwa na bakteria, virusi na fangasi.

“Watoto chini ya miaka miwili wanaofikishwa hospitalini sasa, wengi wanaumwa mafua ambayo huwafanya kushindwa kupumua. Kila kundi linakuja na changamoto yake,” amesema.

Ili kudhibiti hali hiyo, Dk Mneka amesisitiza umuhimu wa wazazi kuhakikisha watoto wanapata chanjo, wanazingatia usafi na kuwapeleka hospitalini wanapoonesha dalili za ugonjwa.

Akizungumzia changamoto hiyo, Dk Jida Said amesema matatizo ya mfumo wa upumuaji hayaishii kwa watoto, bali hata watu wazima wanakabiliwa nayo hivi sasa.

“Virusi vya mafua na kifua vinawaathiri sana pia watu wazima na hii inatokana na hali ya hewa ilivyo sasa,” amesema.

Mtaalamu wa Hali ya Hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Ramadhani Omary amesema kipindi hiki kina ni cha baridi na vumbi, hali inayoweza kuchochea magonjwa ya mfumo wa upumuaji.

“Sasa hivi ni msimu wa vumbi na baridi. Katika kipindi cha baridi na vumbi, magonjwa ya macho na kifua hujitokeza, kwa hiyo hali hii ya hewa inachangia,” amesema.

Wakati huo huo, utafiti uliochapishwa Juni mwaka huu na watafiti wa Taasisi ya Afya ya Ifakara (IHI) umeonesha kuwa kuishi katika maeneo yanayokumbwa na mafuriko mara kwa mara kunaongeza hatari ya kupata magonjwa sugu ya mfumo wa upumuaji.

Utafiti huo uliochapishwa katika Jarida la Kisayansi la GeoHealthJuni, 2026, uliongozwa na Dk Ibrahim Msuya kwa kushirikiana na watafiti kutoka IHI na Chuo Kikuu cha Cork nchini Ireland.

Watafiti hao, wametumia taarifa za picha za satelaiti kuhusu unyevunyevu wa ardhi pamoja na takwimu za afya kutoka kaya 1,500 katika mitaa 15 yenye viwango tofauti vya kipato jijini Dar es Salaam.

Matokeo yanaonesha wakazi wa maeneo yenye mafuriko mengi walikuwa na uwezekano wa hadi mara tisa kuugua magonjwa sugu ya mfumo wa upumuaji ikilinganishwa na wanaoishi katika maeneo makavu.

Aidha, kila ongezeko la unyevunyevu wa ardhi lilihusishwa na ongezeko la takribani asilimia 18 la hatari ya kupata magonjwa hayo.

Utafiti huo pia ulibaini msongamano wa watu katika kaya na matumizi ya maeneo ya pamoja ya kutupa taka, ukihusishwa na ongezeko la hatari ya magonjwa ya mfumo wa upumuaji.

Watafiti wamependekeza mipango bora ya miji na uboreshaji wa makazi kupewa kipaumbele katika kudhibiti magonjwa hayo, sambamba na hatua nyingine za afya ikiwamo kupunguza uvutaji wa sigara.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

PATRICK VIEIRA ATEULIWA KUWA KOCHA MKUU WA SENEGAL

Next

*MKAKATI WA TAIFA WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA WAANZA KUTEKELEZWA MKINGA*

Recent Posts

  • Watano wafariki dunia akiwamo mtoto mchanga, wanane wajeruhiwa Lushoto
  • Madeleka aeleza namna alivyokamatwa Mahakama Kuu
  • Makosa matatu yasababisha daladala 203 kufungiwa VTS
  • Wadau kujadili maendeleo ya kidijitali, data ikipewa kipaumbele
  • *MKAKATI WA TAIFA WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA WAANZA KUTEKELEZWA MKINGA*

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme