Polisi yawashikilia 18 kwa madai ya kuchoma magari
Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limewakamata na kuwashikilia watuhumiwa 18 pamoja na pikipiki 23, likiwatuhumu kujihusisha na matukio ya kushambulia, kuchoma na kuharibu magari yanayopata ajali.
Polisi pia limewaonya waendesha bodaboda wenye tabia ya kujichukulia sheria mkononi baada ya ajali, likisema baadhi yao hujiona wamekosewa hata wanapokuwa wahusika au chanzo cha ajali, kisha kuchoma au kuharibu magari yaliyohusika.
Onyo hilo limetolewa baada ya ajali iliyotokea leo, Agosti 19, 2026, katika Barabara ya Kilwa, eneo la Mivinjeni, Temeke, iliyosababisha vifo vya watu wawili na kumjeruhi mmoja.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro ajali hiyo ilitokea saa 3:45 asubuhi baada ya lori aina ya DAF lililokuwa na tela kugongana na pikipiki aina ya Boxer.
Lori hilo lilikuwa likitokea eneo la Uhasibu kuelekea Bendera Tatu, wakati pikipiki hiyo ikiendeshwa na Msichoke Mohamed, maarufu Mnyige, mkazi wa Chamazi, Dar es Salaam.
Polisi imesema chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa pikipiki kuhama kutoka barabara ya huduma na kuingia katika Barabara ya Kilwa bila kuchukua tahadhari kwa watumiaji wengine wa barabara.
Wakati wa ajali, pikipiki hiyo ilikuwa imebeba abiria wawili.
Ajali hiyo ilisababisha kifo cha dereva wa pikipiki, Msichoke Mohamed, pamoja na mmoja wa abiria, George Luis Nyantora, mfanyabiashara na mkazi wa Mbagala Zakhem, Dar es Salaam.
Abiria mwingine, William Ashery, maarufu Tumbo, mjasiriamali na mkazi wa Mwanza, alijeruhiwa na kupelekwa hospitalini kwa matibabu.
Bodaboda wachoma lori baada ya ajali
Baada ya ajali hiyo, kundi la waendesha bodaboda lilikusanyika eneo la tukio na kudaiwa kuchoma moto sehemu ya mbele ya lori lililohusika katika ajali, maarufu ‘horse’.
Jeshi la Polisi limelaani tukio hilo, likisema kuchoma moto, kupiga au kuharibu magari yanayohusika katika ajali, pamoja na kupora mali zilizomo ndani yake, ni vitendo vya kihalifu na kinyume cha sheria.
Polisi imesema baadhi ya waendesha bodaboda wamekuwa na tabia ya kujiona wao ndio waliokosewa kila ajali inapotokea, hata pale ambapo uchunguzi unaweza kuonyesha kuwa wao ndio waliohusika au kusababisha ajali.
Kwa mujibu wa Polisi, badala ya kuacha mamlaka zinazohusika kufanya uchunguzi na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria, baadhi yao hukusanyika na kuamua kulipiza kisasi kwa kushambulia magari au watu wanaohusishwa na ajali.
Jeshi hilo limeonya kuwa hatua hiyo haiwezi kuvumiliwa na kwamba waendesha bodaboda watakaohusika na uharibifu wa mali au vitendo vya vurugu watachukuliwa hatua za kisheria.
Watuhumiwa 18 washikiliwa
Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam imesema imewakamata na kuwashikilia watuhumiwa 18 pamoja na pikipiki 23 zinazodaiwa kuhusishwa na matukio ya aina hiyo.
Baadhi ya pikipiki hizo, kwa mujibu wa taarifa hiyo, ziliachwa na watuhumiwa waliokimbia baada ya matukio yaliyotokea maeneo ya Mbopo, Mabwepande, Bunju B, Tegeta, Kunduchi, Kimara na Magomeni Kanisani.
Polisi imesema kukamatwa na kushikiliwa kwa watuhumiwa hao ni sehemu ya hatua zinazochukuliwa kukomesha tabia ya baadhi ya waendesha bodaboda kushambulia magari mara baada ya ajali.
Katika tukio jingine lililotajwa na Polisi, Ally Abdallah (44), fundi rejeta na dereva bodaboda, anadaiwa kuwa miongoni mwa kundi la waendesha pikipiki lililohusika katika tukio la Agosti 15, 2026.
Kwa mujibu wa Polisi, siku hiyo Abdallah akiwa na kundi la wenzake na pikipiki zao, walilishambulia gari lenye namba T 333 EMR, aina ya Harrier, rangi nyeusi, baada ya mmoja wao kuhusika katika ajali.
Gari hilo lilishambuliwa kwa jiwe kubwa lililovunja kioo cha nyuma na kusababisha uharibifu pamoja na hofu kwa mwenye gari.

