Watano wafariki dunia akiwamo mtoto mchanga, wanane wajeruhiwa Lushoto
Tanga. Watu watano akiwemo mtoto mchanga wa miezi sita, wamefariki dunia na wengine wanane kujeruhiwa baada ya gari aina ya Toyota Coaster kutumbukia bondeni katika eneo la Vuga, Wilaya ya Lushoto, Mkoa wa Tanga.
Ajali hiyo imetokea leo, Agosti 18, 2026, saa 7:30 mchana katika barabara ya Mombo–Lushoto.
Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga, gari hilo lilikuwa likitokea Tanga Mjini kuelekea Ngwashi, likiendeshwa na Ally Dione.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi, amesema watu watano wamepoteza maisha katika ajali hiyo, huku miili yao ikiwa bado haijatambuliwa.
Amesema waliokufa ni wanaume wawili wanaokadiriwa kuwa na umri wa miaka 35 hadi 45, wanawake wawili wenye umri unaokadiriwa kuwa kati ya miaka 25 na 35, pamoja na mtoto mchanga anayekadiriwa kuwa na miezi sita.
Aidha, watu wanane wamejeruhiwa na wamelazwa katika Kituo cha Afya Soni, Wilaya ya Lushoto, kwa ajili ya matibabu.
Mchunguzi amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa ajali hiyo inadaiwa kusababishwa na uzembe wa dereva, aliyeshindwa kulimudu gari, hali iliyosababisha kuacha barabara na kutumbukia bondeni.
“Miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kwa ajili ya kukamilisha uchunguzi, kutambuliwa na taratibu nyingine za kisheria,” amesema.
Amesema Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo na mazingira kamili ya ajali hiyo.
Jeshi hilo limetoa wito kwa madereva kuzingatia sheria za usalama barabarani, kuwa makini na kuhakikisha wanaendesha kwa umakini ili kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.
Aidha, limewakumbusha watumiaji wote wa barabara kuwa usalama barabarani ni jukumu la kila mmoja.

