Hichilema ashinda tena urais Zambia
Dar es Salaam. Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema, ameshinda uchaguzi wa urais na kupata muhula wa pili wa miaka mitano, katika ushindi unaompa nafasi ya kuendeleza mpango wake wa kurekebisha uchumi uliokuwa ukikabiliwa na mzigo mkubwa wa madeni.
Tume ya Uchaguzi ya Zambia imemtangaza Hichilema kuwa mshindi baada ya kupata asilimia 61.4 ya kura, sawa na karibu kura milioni tatu.
Mpinzani wake mkuu, Brian Mundubile wa Tonse Alliance, amepata takriban asilimia 38, sawa na kura milioni 1.86.
Hichilema amewashukuru wananchi kwa kumpa tena dhamana ya kuongoza nchi hiyo na kuahidi uongozi unaojumuisha hata waliompigia kura mpinzani wake.
Ushindi huo unakuja baada ya uchaguzi iliofanyika Agosti 13,2026 ukiwa na mvutano, huku shughuli ya kuhesabu kura ikisimamishwa kwa muda kutokana na taarifa za madai ya kushambuliwa kwa baadhi ya watendaji wa uchaguzi na kuibwa kwa karatasi za kura katika baadhi ya maeneo.
Upinzani pia umekosoa ushindi huo ukihoji mwenendo wa mchakato, ingawa mamlaka za Zambia zimekana madai ya kuingilia uchaguzi.
Safari ya Hichilema, kutoka mpinzani hadi kuingilia Ikulu
Hichilema, anayejulikana kwa jina la HH, aliingia madarakani mwaka 2021 baada ya kushindwa mara kadhaa katika mbio za urais.
Alikuwa kiongozi wa muda mrefu wa Chama cha United Party for National Development (UPND) kabla ya kumshinda Rais wa wakati huo, Edgar Lungu, katika uchaguzi wa 2021.
Kabla ya siasa, Hichilema alijijengea jina katika biashara na ujasiriamali, akiongoza kampuni kubwa za ushauri wa biashara nchini Zambia na baadaye kuwa mwekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwamo kilimo na mifugo.
Alipoingia madarakani mwaka 2021, alikuta Zambia ikiwa imetoka katika mgogoro mkubwa wa madeni, ikiwamo kutolipa deni lake la taifa mwaka 2020.
Katika muhula wake wa kwanza, serikali yake iliongoza mchakato wa marekebisho ya deni la zaidi ya dola za Marekani bilioni 12 (Sh31.68 trilioni), ikaongeza ushirikiano na taasisi za fedha za kimataifa na kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini, hasa shaba.
Serikali pia ilipanua huduma za kijamii, ikiwamo elimu ya sekondari bila ada. Hata hivyo, mafanikio hayo ya kiuchumi hayajaondoa changamoto kwa wananchi wa kawaida.
Gharama za chakula na nishati, ajira na umaskini bado ni miongoni mwa masuala yaliyotawala mjadala wa uchaguzi.
Kwa hiyo, ushindi wa Hichilema unaweka mbele yake mtihani wa kuhakikisha mafanikio ya uchumi wa taifa yanaonekana pia katika maisha ya wananchi.
Muhula wake wa pili pia utaangaliwa katika eneo la demokrasia kwani Serikali yake imekabiliwa na tuhuma kutoka kwa wapinzani na mashirika ya kiraia kuhusu kubanwa kwa upinzani na uhuru wa kisiasa, madai ambayo imekuwa ikiyakanusha.
Hivyo, ushindi wa Hichilema si mwisho wa safari yake ya kisiasa bali mwanzo wa miaka mingine mitano ambayo itaamua kama ahadi za mageuzi ya uchumi zitaendelea kubaki kwenye takwimu za Serikali pekee, au kuwa mabadiliko yanayoonekana katika maisha ya Mzambia wa kawaida.

