SERIKALI YATOA MIEZI SITA KUSAJILI MIUNDOMBINU MUHIMU YA TEHAMA
Na Matukio DaimaMedia
Serikali imewataka wamiliki na waendeshaji wa miundombinu muhimu ya TEHAMA katika sekta mbalimbali nchini kuhakikisha wanasajili miundombinu hiyo ndani ya kipindi cha miezi sita, huku ikionya kuwa watakaokiuka matakwa ya sheria watakabiliwa na faini au kifungo.
Akizungumza na waandishi wa habari, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha miundombinu muhimu ya TEHAMA inalindwa dhidi ya mashambulizi ya kimtandao, majanga na matukio mengine yanayoweza kuvuruga huduma muhimu.
Amesema miundombinu hiyo inahusisha mali, vifaa, mifumo ya kompyuta, mitandao na mifumo mingine ya kidijitali ambayo endapo itashambuliwa au kuharibika inaweza kusababisha madhara kwa usalama, uchumi na ustawi wa jamii.
“Lengo ni kuhakikisha mifumo hii inakuwa salama, inapatikana na inafanya kazi kwa uhakika hata wakati wa kutokea mashambulizi ya mtandao, majanga au dharura,”amesema Waziri Kairuki.
Amesema Serikali imeweka vigezo vya kisayansi na kitaalamu vya kubaini miundombinu inayoweza kutambuliwa kuwa muhimu kwa Taifa, huku sekta mbalimbali zikipewa elimu kuhusu utekelezaji wa matakwa hayo.
Ameeleza kuwa katika kubaini miundombinu hiyo, Serikali imezingatia pia utegemezi uliopo kati ya sekta moja na nyingine, kwa kuwa hitilafu au shambulio katika mfumo mmoja linaweza kuathiri huduma zinazotolewa na sekta nyingine.
“Tunapoangalia mfumo muhimu, tunajiuliza endapo utashambuliwa madhara yatakuwa yapi, unaweza kuendelea kutoa huduma kwa muda gani na sekta nyingine zitaathirika kwa kiwango gani,” amesema Waziri Kairuki
Kwa mujibu wa maelezo hayo, tathmini hiyo itasaidia kubaini uwezo wa kila mfumo kuhimili mashambulizi na kuendelea kutoa huduma kwa muda fulani, pamoja na kuweka mikakati ya kurejesha huduma kwa haraka endapo kutatokea hitilafu.
Aidha, amesema Sekta zinazohusika katika hatua hiyo ni pamoja na mawasiliano, fedha na benki, maji, afya, viwanda, madini, usafirishaji, chakula na kilimo, ujenzi, usafiri wa maji, uvuvi, mafuta, elimu, ardhi na nishati.
Serikali imesema zoezi la tathmini na usajili linapaswa kukamilika ndani ya miezi sita, ambapo mwisho wa utekelezaji huo ni Septemba 15, 2026.
Hata hivyo, amesema wamiliki na waendeshaji wa miundombinu muhimu wanatakiwa kutumia mfumo maalumu wa usajili wa CII na kuwasilisha taarifa zinazohitajika kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.
Aidha, Wizara imeandaa mwongozo wa ulinzi na usimamizi wa miundombinu muhimu ya TEHAMA pamoja na mwongozo wa ukaguzi wa CII, kwa lengo la kuwasaidia wadau kutekeleza matakwa ya usajili, ulinzi na usimamizi wa mifumo hiyo.
Serikali pia imeandaa mpango wa elimu kwa umma na wadau mbalimbali kuhusu usajili na ulinzi wa miundombinu hiyo.
Amesema Tanzania imeangalia pia uzoefu wa nchi nyingine, ikiwemo Singapore na Ufaransa, katika kuweka mifumo ya ulinzi na usimamizi wa miundombinu muhimu ya TEHAMA, huku ikitengeneza mfumo unaozingatia mazingira ya Tanzania.
Aidha, amesisitiza kuwa vitisho vya kimtandao vinaendelea kubadilika kutokana na maendeleo ya teknolojia, hivyo ni muhimu Serikali na sekta binafsi kuendelea kuboresha mifumo ya ulinzi.
Sambamba na hilo, Serikali imeonya kuwa mtu au taasisi itakayeshindwa kutekeleza matakwa ya sheria kuhusu miundombinu muhimu ya TEHAMA atachukuliwa hatua za kisheria, ikiwa ni pamoja na kutozwa faini isiyopungua sh milioni moja au mara tatu ya thamani ya hasara iliyosababishwa, au kifungo kisichopungua miaka mitano, au adhabu zote mbili kwa pamoja.
Serikali imesema adhabu hiyo inalenga kuhakikisha wamiliki na waendeshaji wa miundombinu hiyo wanazingatia matakwa ya usalama na kulinda mifumo ambayo ni muhimu kwa uchumi, usalama wa Taifa na huduma muhimu kwa wananchi.
Wamiliki na waendeshaji wa miundombinu hiyo wametakiwa kushirikiana na wataalamu wa Wizara katika mchakato wa usajili, kutoa taarifa zinazohitajika na kuhakikisha wanatekeleza matakwa yote ya usalama yaliyowekwa.
Serikali imesema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda huduma muhimu, uchumi na usalama wa Taifa, pamoja na kuhakikisha huduma zinaendelea kupatikana kwa wananchi hata wakati wa mashambulizi ya kimtandao au dharura nyingine.


