Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Mbinu za kuvunja ukimya wa wanafunzi darasani

By admin
August 18, 2026 3 Min Read
0

Dodoma. Mwalimu anaingia darasani. Anaandika swali ubaoni. Anageuka na kuwauliza wanafunzi: “Nani anaweza kujibu swali hili?”  Kimya.



Anaangalia upande wa kushoto. Kimya. Anaangalia upande wa kulia. Bado kimya. Wanafunzi wanatazamana, wengine wanaangalia chini, na wachache wanatabasamu kwa aibu. Mwalimu anaishia kusema: “Hivi kweli hakuna anayejua?”

Lakini pengine tatizo si kwamba wanafunzi hawajui. Tatizo linaweza kuwa tumewazoesha kukaa kimya.

Tukirudi nyuma kidogo katika maisha yetu ya utotoni, wengi wetu tulikulia katika mazingira ambayo mtoto alifundishwa kusikiliza zaidi kuliko kuzungumza.

Watu wazima wanapozungumza, mtoto alitakiwa kukaa kimya. Ukijaribu kuingilia mazungumzo, unaweza kusikia: “Kaa kimya! Unaongea nini wewe?” Au, “Funga mdomo, watu wazima wanaongea.”

Ujumbe huu unapojirudia mara nyingi, mtoto hujifunza jambo moja muhimu: kuongea mbele ya watu wazima kunaweza kuwa hatari.

Mtoto anakua. Anaingia shule. Anaendelea na sekondari. Anafika chuo kikuu. Lakini ile hofu ya kuzungumza mbele ya mwenye mamlaka wakati mwingine inasafiri naye.

Darasani, mwalimu anaonekana kuwa ndiye mwenye maarifa yote. Mwanafunzi anaingia akiwa na mtazamo kwamba yeye amekuja kupokea ‘madini’ kutoka kwa mwalimu. Mwalimu anajua; mwanafunzi anapaswa kusikiliza.

Matokeo yake ni darasa ambalo mwalimu anaweza kuzungumza kwa dakika 60, huku wanafunzi 60 wakiwa wasikilizaji.

Lakini elimu ya kisasa inataka zaidi ya kusikiliza. Inahitaji mwanafunzi afikiri, aulize, ajadili, apinge, aeleze na ajenge maarifa pamoja na wengine.

Hapo ndipo mbinu maarufu kwa Kiingereza ijulikanayo kwa jina la ‘Think–Pair–Share’ inapoweza kuwa muhimu.

Ni mbinu rahisi, lakini yenye nguvu. Mwalimu anauliza swali. Badala ya kumtaka mwanafunzi ajibu mara moja mbele ya darasa, anampa muda wa kwanza kufikiri mwenyewe (think), kisha  azungumze na mwanafunzi mwenzake (pair) na mwisho mawazo yanashirikishwa na darasa zima (share).

Kwa nini mbinu hii inaweza kufanya kazi vizuri katika mazingira yetu? Kwa sababu mwanafunzi anaweza kuwa na ujasiri mkubwa zaidi wa kuzungumza na mwanafunzi mwenzake kuliko kuzungumza moja kwa moja mbele ya mwalimu na darasa zima.

Fikiria mwanafunzi ameulizwa swali mbele ya wanafunzi 80. Anajua jibu, lakini anaogopa. Anafikiri, “Nikisema vibaya watanicheka.” Anaogopa mwalimu kusema hajui. Anaogopa wenzake kumwona hajui.

Lakini mwalimu akisema: “Kaa na mwenzako kwa dakika mbili, jadilini swali hili,” mazingira yanabadilika.

Mwanafunzi anamwambia mwenzake, “Mimi nimeelewa hivi…”

Mwenzake anajibu, “Mimi nimeona hivi…”

Wanalinganisha mawazo. Wanarekebishana. Wanajenga jibu.

Baada ya hapo mwalimu anaweza kusema: “Sasa niambieni, mwenzako amekuambia nini?”

Hapa kuna ujanja mkubwa wa kisaikolojia.

Mwanafunzi hatakiwi tena kusema, “Jibu langu ni hili.” Anaweza kusema, “Mwenzangu amesema…”

Hii inapunguza hofu ya kukosea. Ni rahisi zaidi kueleza wazo ambalo umesikia kutoka kwa mwenzako kuliko kusimama mbele ya watu na kutangaza kwamba “hili ndilo jibu langu.”

Hivyo hatua hii ndogo inaweza kuwa mwanzo wa kujenga ujasiri wa kitaaluma.

Baada ya muda, mwanafunzi ambaye jana aliogopa kusema neno moja mbele ya darasa, anaweza kuanza kuzungumza. Leo anazungumza na mwenzake. Kesho anashiriki katika kikundi baadaye anainua mkono. Hatimaye anaweza kusimama mbele ya darasa na kueleza wazo lake mwenyewe.

Kwa hiyo, Think–Pair–Share si tu mbinu ya kufanya wanafunzi washiriki somo. Inaweza kuwa daraja la kumtoa mwanafunzi kwenye utamaduni wa ukimya na kumuingiza katika utamaduni wa mazungumzo na ujenzi wa maarifa.

Hata hivyo, kuna jambo muhimu ambalo walimu tunapaswa kulielewa: ukimya si lazima uwe ujinga.

Mwanafunzi anayekaa kimya anaweza kuwa anajua. Anaweza kuwa na wazo zuri. Anaweza hata kuwa na jibu sahihi kabisa. Lakini anaweza kukosa ujasiri wa kulisema.

Kwa hiyo, kabla hatujasema “wanafunzi wetu hawajui”, tujiulize: Je, tumewajengea mazingira ya kuwaambia wanachojua?

Darasa halipaswi kuwa mahali ambapo mwalimu pekee ndiye mwenye haki ya kuzungumza. Mwalimu anaweza kuwa mwezeshaji wa maarifa, lakini wanafunzi pia wana uzoefu, mawazo, maswali na mitazamo inayoweza kulifanya darasa liwe hai.

Labda tunahitaji kubadilisha kidogo ujumbe tuliokulia nao. Badala ya mtoto kuambiwa kila mara: “Kaa kimya, watu wazima wanaongea.” Darasani tumwambie: “Fikiri, zungumza na mwenzako. Sikiliza. Kisha shiriki.”

Hii ni kwa sababu wakati mwingine, mwanafunzi hahitaji kushinikizwa kuzungumza mbele ya watu 60. Anahitaji tu kupewa mtu mmoja wa kwanza wa kuzungumza naye.

Hapo ndipo Think–Pair–Share inapoanzia. Na pengine, hapo ndipo safari ya kuvunja ukimya wa mwanafunzi wa Kitanzania inaweza kuanzia.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

BIDHAA ZA CHAKULA ZISIZOKIDHI MATAKWA YA VIWANGO ZATEKETEZWA .

Next

MAGAZETINI LEO JUMANNE AGOSTI 18/2026,USIPITWE NA GAZETI LA JAMHURI KWA HABARI MOTO MOTO

No Comment! Be the first one.

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • DC HAI AENDELEA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI, ATATUA MIGOGORO YA ARDHI
  • Wamiliki miundombinu muhimu ya Tehama watakiwa kuisajili
  • SHILINGI BILIONI 356 ZATUMIKA KUTEKELEZA MIRADI MOROGORO
  • Binti auawa kwa madai ya kupigwa na baba yake mdogo, kisa sherehe ya tohara
  • PROF. MKUMBO: HALMASHAURI ZIBUNI SHUGHULI MPYA ZA KIUCHUMI, SI TOZO MPYA.

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme