Jux na Priscy Waweka Wazi Sura ya Mtoto Wao Kwa Mara ya Kwanza

Global Publishers
August 25, 2026
48 views
0 Comments

Mwanamuziki wa Bongo Flava, Juma Jux, na mke wake Priscilla Ojo, maarufu kama Priscy, wamezua gumzo mitandaoni baada ya kuamua kuonyesha sura ya mtoto wao kwa mara ya kwanza tangu kuzaliwa.

Kwa miezi kadhaa, wawili hao walikuwa wamechagua kutoweka wazi sura ya mtoto wao, jambo lililowaacha mashabiki na wafuasi wao wakisubiri kwa hamu kumuona.

Hata hivyo, Jux na Priscy sasa wamevunja ukimya huo baada ya kushirikisha picha rasmi ya mtoto wao iliyopigwa kwa mtindo wa kitaalamu na kuvutia hisia za watu wengi kwenye mitandao ya kijamii.

Uamuzi huo umeongeza gumzo miongoni mwa mashabiki, huku wengi wakieleza furaha yao baada ya hatimaye kupata nafasi ya kumuona mtoto huyo ambaye amekuwa akifichwa kwa muda.

Mbali na sura yake, mavazi na muonekano wa mtoto huyo pia yamezua mjadala, huku baadhi ya mashabiki wakigusia maisha ya kifahari yanayoonekana katika familia ya Jux na Priscy.

Priscy, ambaye anatokea nchini Nigeria, amejijengea jina katika mitindo, biashara na ushawishi kupitia mitandao ya kijamii. Yeye ni binti wa mwigizaji maarufu wa Nollywood, Iyabo Ojo.

Licha ya kukulia katika familia yenye umaarufu, Priscy amefanikiwa kujenga chapa yake binafsi katika ulimwengu wa mitindo na burudani, huku uhusiano wake na Jux ukiendelea kuvuta hisia za mashabiki Tanzania na Nigeria.

Netanyahu Aingia Mtegoni, Uturuki Yataka Interpol Imkamate

Global Publishers
August 25, 2026
18 views
0 Comments

Uturuki imetangaza hatua ya kutaka Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, akamatwe kimataifa kufuatia uchunguzi kuhusu shambulio dhidi ya wanaharakati waliokuwa wakipeleka misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.

Waziri wa Sheria wa Uturuki, Akin Gurlek, amesema hati za kukamatwa zimetolewa dhidi ya Netanyahu pamoja na mshukiwa mwingine, kwa tuhuma zinazohusisha mauaji ya kimbari, uhalifu dhidi ya ubinadamu na mateso.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kesi hiyo inawahusisha jumla ya watu 35 na inahusiana na tukio la Israel kuingilia boti za Global Sea Flotilla katika maji ya kimataifa wakati zikiwa njiani kuelekea Gaza kwa ajili ya kupeleka misaada ya kibinadamu.

Uturuki imekuwa mkosoaji mkubwa wa operesheni za kijeshi za Israel nchini Gaza, huku serikali yake ikiendelea kuitaka jumuiya ya kimataifa kuchukua hatua dhidi ya kile inachodai kuwa ni ukiukaji wa sheria za kimataifa.

Hatua hiyo ya Uturuki inatarajiwa kuongeza mvutano wa kisheria na kidiplomasia kati ya nchi hiyo na Israel, huku suala la kukamatwa kwa Netanyahu likiwa sasa likielekezwa kwenye taratibu za kimataifa kupitia Interpol.

Hata hivyo, Israel imeendelea kukataa tuhuma za kufanya ukiukaji wa sheria za kimataifa na haki za binadamu, jambo linalofanya hatua hiyo ya Uturuki kuwa suala linaloweza kuendelea kujadiliwa katika ngazi za kimataifa.

Stori na Ilankize Godfrey | GPL – TUDACO