Dk Kiruswa achangia Sh milioni 6 ujenzi darasa la awali – HabariLeo
ARUSHA: Juhudi za wananchi wa Kitongoji cha Lailupa, Kijiji cha Meirugoi, Kata ya Gelai-Meirugoi wilayani Longido mkoani Arusha, za kujitolea kujenga darasa la shule ya awali (chekechea) lenye thamani ya Sh milioni 12, zimemgusa Mbunge wa Jimbo hilo, Dk Steven Kiruswa, ambaye ameamua kugharamia hatua ya mwisho ya ukamilishaji wa jengo hilo kwa Sh milioni 6 kutoka kwenye fedha zake binafsi.

Wananchi hao walimweleza Mbunge huyo ambaye pia ni Naibu Waziri wa Madini, wakati akiwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo katika kata hiyo, ambapo walimsimamisha na kumueleza changamoto ya watoto wao kusoma chini ya mti bila kujali mvua au jua.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Lailupa, Ndung’anak Mepukor, alisema jitihada za akina mama, vijana pamoja na viongozi wa mila maarufu kama Laigwanani, ziliwezesha kumshawishi Mbunge huyo kufika eneo hilo na kujionea hali halisi ya mazingira ambayo watoto walikuwa wakipata elimu.

Alisema baada ya kufika eneo hilo, Kiruswa aliona wananchi walikuwa wamefanya sehemu kubwa ya kazi, lakini ujenzi ulikuwa haujakamilika kutokana na kukosekana kwa mlango mmoja, madirisha sita, mabati 60, madawati 20, mbao pamoja na hatua za upigaji plasta.
“Wananchi tulijitahidi kwa nguvu zetu wenyewe, kila kaya ilitoa mchango wa fedha, wengine waliuza mifugo na wengine walishiriki katika uchimbaji wa msingi, ujenzi na kubeba matofali ili watoto wetu wapate sehemu salama ya kusomea,” alisema Mepukor.
Alisema baada ya kuona jitihada hizo na changamoto ya watoto kusoma chini ya mti, Mbunge Kiruswa aliamua kubeba gharama za kukamilisha ujenzi huo kwa Sh milioni 6.

Akizungumza baada ya kutoa ahadi hiyo, Kiruswa aliwapongeza wananchi wa Lailupa kwa moyo wa kujitolea na kusema hatua hiyo imempa faraja kubwa kwa kuona jamii ikishiriki katika kuboresha elimu.
Alisema ameamua kuchangia kukamilika kwa darasa hilo ili kuwawezesha watoto kusoma karibu na makazi yao na kuondokana na adha ya kutembea umbali mrefu kufuata elimu.
Kiruswa alisema suala la kuhakikisha watoto wanapata elimu bora ni jukumu la kila mwananchi, huku akieleza kuwa juhudi za wananchi zinapaswa kuungwa mkono na serikali pamoja na viongozi wao.
Aidha, alisema atahakikisha shule hiyo ya awali inasajiliwa na kupata mwalimu mwenye sifa, kwani kwa sasa inategemea mwalimu wa kujitolea ambaye hana sifa rasmi za ualimu.

“Lengo langu ni kuhakikisha ifikapo Januari mwakani shule hii inakuwa imesajiliwa, inatambulika na serikali na watoto wanafundishwa na mwalimu mwenye sifa,” alisema.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Gelai-Meirugoi, Daniel Nasinda, alisema watoto wa Kitongoji cha Lailupa walikuwa wakitembea zaidi ya kilomita 10 kwenda na kurudi kutafuta elimu, hali iliyokuwa hatarishi kutokana na uwepo wa wanyama wakali katika eneo hilo.
Alisema uamuzi wa wananchi kujenga darasa hilo umeleta matumaini mapya kwa watoto na wazazi, kwani sasa watapata mazingira salama ya kujifunzia karibu na makazi yao.