Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Close

Search

  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Subscribe
Habari

Masaji si tiba ya kila maumivu, wataalamu waonya

By admin
August 17, 2026 3 Min Read
0

Dar es Salaam. Wataalamu wa afya wameonya wananchi dhidi ya kukimbilia huduma za masaji wanapopata maumivu ya mgongo, shingo, miguu au misuli bila kwanza kufahamu chanzo cha tatizo, wakisema kufanya hivyo kunaweza kutoa nafuu ya muda huku ugonjwa ukiendelea kukua.



Wamesema baadhi ya maumivu yanayodhaniwa kuwa ya uchovu au mkazo wa misuli yanaweza kuhitaji tathmini ya kitaalamu ili kubaini chanzo na kupewa matibabu au mazoezi yanayolenga kurejesha uwezo wa mwili.

Daktari bingwa wa magonjwa ya ndani wa Hospitali ya Medinova, Selestine Mpiri, anasema dhana inayowachanganya wananchi ni kuamini kuwa fiziotherapia na masaji ni huduma moja.

“Massage mara nyingi inalenga kutoa unafuu wa muda mfupi. Misuli ikikaza ukafanyiwa masaji utajisikia vizuri, lakini hiyo inaweza kuwa ni ya muda mfupi. Fiziotherapia inalenga kutafuta mzizi wa tatizo na kuhakikisha unafanyiwa mazoezi au utaratibu unaoweza kusaidia tatizo liondoke na lisirudi tena,” anasema.

Anasema tatizo si masaji yenyewe, bali kuitumia kama tiba ya kila aina ya maumivu bila kufanyiwa tathmini ya kitaalamu.

Kwa mfano, anasema baadhi ya wagonjwa waliowahi kufika hospitalini wakiwa na dalili zinazofanana na kiharusi, walibainika baada ya uchunguzi kuwa hawakuwa na kiharusi wala tatizo la ubongo na walisaidiwa kwa fiziotherapia.

“Nilikuwa na wagonjwa watatu vijana ambao walikuja wakiwa wamepooza upande mmoja wa uso. Baada ya kuwafanyia uchunguzi, tulibaini hawakuwa na kiharusi wala tatizo la ubongo. Walipewa fiziotherapia na wakapona,” anasema.

Kwa mujibu wa Dk Mpiri, fiziotherapia haiwahusu watu waliopata ajali au kufanyiwa upasuaji pekee, bali inaweza kusaidia changamoto mbalimbali zinazohusu misuli, mifupa, mishipa ya fahamu, mfumo wa upumuaji na utendaji wa mwili.

“Fiziotherapia ni kubwa zaidi ya tunavyofikiria. Kuna magonjwa ya upumuaji, kizunguzungu na matatizo ya misuli ya nyonga ambayo yanaweza kusaidiwa kwa tiba hii,” anasema.

Anasema udhaifu wa misuli ya nyonga unaweza kuhusishwa na changamoto za kudhibiti mkojo na kwamba, kwa baadhi ya watu, mazoezi maalumu yanaweza kusaidia kuimarisha misuli hiyo.

Hatari ya masaji ya nguvu

Wataalamu pia wanaonya matumizi ya nguvu kubwa wakati wa masaji, hasa kwa watu wenye maumivu ya mgongo ambayo chanzo chake hakijajulikana.

Baadhi ya watoa huduma hutumia uzito wa mwili, ikiwamo kukanyaga mgongo, kwa madai ya kumsaidia mteja kujisikia mwepesi.

Hata hivyo, wataalamu wanasema shinikizo kubwa linaweza kuwa hatari kwa mtu mwenye tatizo la mifupa, pingili za mgongo, mishipa ya fahamu au jeraha ambalo halijagundulika.

Dk Mpiri anawataka watu wenye maumivu ya muda mrefu au yanayorudia kutafuta ushauri wa kitaalamu badala ya kutegemea masaji kila wanapohisi maumivu.

Anasema hata uchovu wa mwili unaweza kusababishwa na mambo mbalimbali, yakiwamo kazi nzito, kukaa au kusimama kwa muda mrefu, kukosa usingizi na mkazo wa misuli.

Hata hivyo, anasema uchovu unaodumu au unaoambatana na dalili nyingine unaweza kuhitaji uchunguzi wa kitabibu.

Akizungumza na Mwananchi mwishoni mwa juma, mtaalamu mwingine wa fiziotherapia wa Medinova, Witney Lema, anasema huduma hiyo inahusika na tiba ya utengamao na mazoezi tiba bila kutumia dawa, huku ikilenga matatizo ya misuli na mifupa pamoja na magonjwa ya mfumo wa fahamu kwa watu wazima na watoto.

“Wengi wetu tunaonekana kusumbuliwa na matatizo ya misuli na mifupa. Tunaumwa migongo, shingo, miguu na tunapata ajali. Baada ya ajali au kuvunjika mifupa, baadhi hushindwa kutembea vizuri tena. Fiziotherapia imekuja kusaidia katika changamoto hizi,” anasema.

Anasema tiba hiyo hutumia mbinu mbalimbali, ikiwamo tiba kwa mikono na vifaa vya kielektroniki, kulingana na hali ya mgonjwa.

Dk Mpiri anawataka wananchi pia kutotumia mazoezi wanayoyaona kwenye Youtube kama mbadala wa tathmini ya mtaalamu.

“Tunatakiwa tujue kwamba mazoezi, ili yafae zaidi, yanatakiwa yawe individualized (yalengwe kwako). Mtaalamu wa fiziotherapia pia atakurekebisha unapofanya mazoezi vibaya,” anasema.

Anasema mazoezi yanapaswa kuzingatia umri, ukubwa wa mwili na hali ya kiafya ya mtu, hivyo mazoezi ya mtu mwenye miaka 20 hayawezi kutumika kwa mtu wa miaka 60 bila tathmini.

Dk Imran Asif Bajwa anasema fiziotherapia huanza kwa tathmini ya mgonjwa na wakati mwingine huhitaji ushirikiano wa wataalamu mbalimbali kulingana na tatizo litakalobainika.

“Kupona kwa mgonjwa hakutegemei daktari mmoja au wawili, bali timu kubwa. Mgonjwa anaweza kuja kwa mtaalamu, lakini wakati wa assessment (tathmini) tunaweza kubaini anahitaji kumuona daktari wa mifupa. Tutafanya kazi kwa pamoja,” anasema.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Kwa nini GB 128 za simu yako zinawahi kujaa? Fanya hivi…

Next

DCEA yateketeza ekari 603 za bangi Morogoro

No Comment! Be the first one.

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • Bado kiza kimetanda mtoto wa siku moja aliyeibwa Dareda
  • Dola ya Marekani yadhoofika, wawekezaji wakisubiri uamuzi wa Fed
  • Wafugaji walalamikia operesheni za usiku, Serikali yajibu
  • Tanzania, DR Congo kuimarisha ushirikiano, kuondoa vikwazo
  • Watano wafariki dunia akiwamo mtoto mchanga, wanane wajeruhiwa Lushoto

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
  • Michezo
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme