Mkakati wa kukabili uhaba wa maji na njaa, kuongeza tija ya kilimo
Dar es Salaam. Jamii za wakulima vijijini zinatarajiwa kunufaika na maboresho ya upatikanaji wa maji salama, usafi wa mazingira na usafi wa mwili, hatua inayolenga kupunguza utapiamlo, kuongeza uzalishaji wa mazao na kuimarisha ustahimilivu wa kaya dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
Mpango huo pia utasaidia kuimarisha usalama wa chakula na lishe, uongozi wa jamii katika utunzaji wa maliasili na ufikaji wa wakulima kwenye masoko yenye tija.
Hatua hiyo inatokana na ushirikiano wa kimkakati kati ya WaterAid Tanzania (WAT) na Farm Africa, unaolenga kuunganisha huduma za maji, usafi wa mazingira na usafi wa mwili (WASH) na mipango ya kilimo endelevu na ustawi wa jamii.
Hiyo ni baada ya Taasisi hizo kusaini Hati ya Makubaliano (MoU) jijini hapa, zikikubaliana kuandaa mipango ya pamoja, kutafuta rasilimali na kutekeleza miradi katika maeneo ambayo huduma za WASH ni muhimu ili kuboresha maisha ya wananchi.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi wa WaterAid Tanzania, Anna Mzinga, alisema ushirikiano huo utaunganisha utaalamu wa shirika lake katika sekta ya WASH na uzoefu wa Farm Africa katika mbinu za kilimo endelevu.
“Maji yanahusianisha afya, utu, usalama wa chakula pamoja na maisha ya kila siku ya watu,” alisema.
Mzinga alisema hatua hiyo itasaidia kubuni suluhu endelevu kwa jamii zilizoathiriwa zaidi na ukosefu wa huduma hizo na kuzijengea uwezo wa kujitegemea.
“Katika makubaliano haya pia tutashirikiana na wadau wengine wa maendeleo katika kupunguza umaskini nchini.”
Mkurugenzi wa Farm Africa Tanzania, Dk David Ojwang, alisema usafi wa mazingira na wa mwili ni nguzo muhimu katika kuimarisha usalama wa chakula na lishe bora.
“Usafi ulioboreshwa ni msingi wa kuimarisha usalama wa chakula na lishe bora nchini,” alisema.
Alisema upatikanaji wa maji si suala la afya pekee, bali ni kiungo muhimu kwa wakulima wadogo wanaokabiliwa na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Ushirikiano huo pia unalenga kuwezesha jamii kujenga maisha yanayostahimili mabadiliko ya tabianchi ifikapo mwaka 2030.
Makubaliano hayo yanakutanisha uzoefu wa miaka 43 wa WaterAid nchini na miaka 35 ya Farm Africa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo vijijini.
Tangu mwaka 1983, WaterAid imewafikia watu milioni 1.9 kwa huduma za maji na milioni 4.3 kwa huduma za usafi.

