Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Subscribe
Close

Search

Habari

Wajenzi wanavyokiuka vibali vya ujenzi, hatari kwa watumiaji

By admin
August 17, 2026 5 Min Read
0

Dar es Salaam. Baadhi ya wamiliki wa majengo jijini Dar es Salaam wamekuwa wakibadilisha mipango ya ujenzi baada ya kupata vibali, ikiwamo kuongeza idadi ya ghorofa, hali ambayo wataalamu wanaonya inaweza kuathiri usalama wa majengo na watumiaji.



Kumbukumbu mbaya ni Novemba 16, 2024, ambapo jengo liliporomoka Mtaa wa Mchikichi na Congo, Kariakoo, Dar es Salaam, na kusababisha vifo vya watu 20, huku zaidi ya 50 wakiokolewa.

Tukio kama hilo lilitokea Machi 29, 2013, Mtaa wa Indira Gandhi, Posta jijini Dar es Salaam, ambapo jengo la ghorofa 16 liliporomoka, ambalo liliombewa kibali cha ghorofa 10. Kuporomoka huko kulisababisha vifo vya watu zaidi ya 15 na kujeruhi wengine.

Aliyekuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Ilala, Kheri Kessy, alisema mwaka 2007 walitoa kibali cha ujenzi wa ghorofa 10 kwa jengo hilo la Posta, ambazo zilikuwa zinafuatiliwa na mkaguzi hadi zilipofikia mwisho, hivyo uongezekaji wa ghorofa sita hawakuutambua.

Novemba 2025, Ofisa wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, aliyeomba jina lake lisitajwe, aliliambia Mwananchi mamlaka hiyo hutoa vibali kwa kuzingatia ramani na michoro inayowasilishwa na mwombaji.

Hata hivyo, alisema baadhi ya wamiliki hubadilisha mipango wanapoanza ujenzi na kuongeza ghorofa tofauti na walizoomba na kupewa kibali.

Alitoa mfano wa jengo moja eneo la Kariakoo, ambalo mmiliki wake aliomba kibali cha kujenga ghorofa tano, lakini wakati wa ujenzi akaongeza hadi ghorofa 10.

“Tumewahi kumpiga faini mmiliki mmoja wa jengo Kariakoo baada ya kubaini aliomba kibali cha ghorofa tano, lakini akajenga ghorofa 10,” alisema ofisa huyo alipozungumza na Mwananchi ilipokuwa ikiandaa habari maalumu kuhusu matumizi ya majengo ya Kariakoo yasiyokamilika.

Hoja hiyo inaakisi kauli ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC), Albert Chalamila, ya Agosti 6, 2026, kueleza kubaini ukiukaji wa masharti ya ujenzi wakati wa ukaguzi.

Chalamila alisema kuna majengo ambayo vibali vyake vilitolewa kwa idadi ndogo ya ghorofa, lakini yalipofikiwa katika maeneo ya ujenzi yalikuwa yamejengwa zaidi ya idadi iliyoidhinishwa.

Katika mfano alioutoa, alisema jengo moja lilipewa kibali cha ghorofa sita, lakini lilikuwa limejengwa hadi ghorofa 13.

Kutokana na hali hiyo, aliamuru mmiliki na mjenzi wakamatwe, huku uchunguzi wa kitaalamu ukiendelea kubaini kama msingi wa jengo hilo ulikuwa umeandaliwa kuhimili ghorofa hizo.

Itakumbukwa, baada ya jengo la Kariakoo kuporomoka na kuua watu 20, Rais Samia Suluhu Hassan, alipotembelea eneo la tukio saa chache baada ya kuwasili nchini akitokea Brazil, alisema Serikali haitasita kubomoa majengo yote ya Kariakoo iwapo tume iliyoundwa kuchunguza usalama wake itashauri ifanyike hivyo.

Sambamba na hilo, mkuu huyo wa nchi aliwasihi watendaji wa Serikali kuwajibika kwa nafasi zao, hasa katika mchakato wa utoaji vibali vya ujenzi, akitaka visimamiwe.

Rais aliagiza iundwe tume kuchunguza majengo yote, na tayari waziri mkuu wa wakati huo, Kassim Majaliwa, ameunda ikiwa na wajumbe 19, akibainisha matokeo yatakayopatikana yatawekwa wazi kwa wananchi.

Pamoja na kuwekwa wazi, alieleza iwapo tume hiyo itashauri majengo yote sokoni hapo yavunjwe, hatasita kufanya hivyo. Pia, Rais Samia alisema anatambua uwepo wa ripoti za tume mbalimbali, ikiwemo ya mwaka 2013, akisema uchunguzi unaofanywa utazingatia pia mapendekezo ya tume hiyo.

Mpaka sasa, ripoti ya tume hiyo ya wajumbe 19 haifahamiki kama ilishamaliza kazi na, kama imemaliza, ilibaini kitu gani.

Kifungu cha 33 cha Sheria ya Mipango Miji ya mwaka 2007 kinahusu hitaji la kupata kibali cha ujenzi kutoka mamlaka husika, huku Kifungu cha 36 kikihusu kumbukumbu za maombi na vibali vya ujenzi.

Kanuni za mwaka 2018 zinaweka utaratibu wa udhibiti na ukaguzi wa majengo, hivyo mwenye kibali cha kujenga idadi ya ghorofa husika hawezi kuongeza ghorofa nyingine tofauti na mpango ulioidhinishwa bila kufuata utaratibu wa kufanya mabadiliko na kupata idhini inayotakiwa.

Aidha, Kanuni ya 34 inaweka masharti kuhusu ukaguzi wa jengo lililokamilika na utoaji wa cheti cha matumizi, hatua ambayo inaweza kubaini tofauti kati ya ramani iliyoidhinishwa na jengo lililojengwa.

Wakili Fatma Kibakala anasema kibali hutolewa kwa kuzingatia nyaraka na michoro iliyowasilishwa, hivyo mwenye jengo anapaswa kujenga kulingana na kilichoidhinishwa.

“Ukipata kibali kwa msingi wa ramani fulani, wajibu wako ni kujenga kwa kuzingatia kile kilichoidhinishwa. Kama unataka kubadilisha, unatakiwa kuwasilisha mabadiliko kwa mamlaka husika na kupata idhini inayotakiwa,” anasema Fatma.

Anasema faini pekee haiwezi kuondoa wajibu wa kuhakikisha jengo ni salama.

“Adhabu ya ukiukaji wa masharti ya kibali ni suala moja, lakini usalama wa jengo ni suala jingine. Mmiliki anapaswa kuhakikisha mabadiliko yote yanafuata taratibu na jengo lina uwezo wa kutumika kwa usalama,” anasema.

Mtaalamu wa ujenzi, Dorcas Msabila, anasema kuongeza ghorofa si sawa na kuongeza vyumba ndani ya nyumba kwa sababu kila sakafu mpya huongeza mzigo unaobebwa na msingi, nguzo na mihimili.

Anasema wakati wa usanifu wa jengo, mhandisi hufanya hesabu kulingana na mzigo ambao mfumo wa jengo unatarajiwa kubeba.

“Ukiwa umebuni jengo kwa idadi fulani ya ghorofa, hesabu za kihandisi zinazingatia mzigo wa jengo hilo. Ukiongeza ghorofa bila kufanya tathmini na usanifu mpya, huwezi kusema moja kwa moja kwamba jengo lina uwezo wa kubeba mzigo huo,” anasema Msabila.

Msabila anasema kabla ya kuongeza sakafu, mhandisi anapaswa kuchunguza uwezo wa msingi, nguzo, mihimili na ubora wa vifaa vilivyotumika.

Anasema tathmini inaweza kuonesha kama jengo linaweza kubeba mzigo mpya au linahitaji uimarishaji wa kimuundo kabla ya kuendelea kutumika.

Mtaalamu wa ramani, Herison Amani, naamani ndiyo msingi wa kuhakikisha jengo linajengwa kwa kuzingatia mpango uliothibitishwa.

“Ukiwa umeidhinishiwa ghorofa nne, halafu ukaongeza nyingine bila kurekebisha ramani na kupata idhini, unakuwa umeondoka kwenye mpango uliokuwa umeidhinishwa,” anasema Amani.

Anasema mabadiliko hayo yanapaswa kuonyeshwa kwenye michoro mipya na kuchunguzwa na wataalamu wa usanifu na uhandisi kabla ya ujenzi kuendelea, kwani ubadilishwaji wa idadi ya ghorofa si mabadiliko madogo; ni lazima mfumo mzima wa jengo uangaliwe upya.

Mkandarasi wa majengo Kariakoo, Emmanuel Kambi, anasema hali hiyo inachangiwa na mmiliki baada ya kuona mfuko wake unaweza kuongeza idadi ya majengo tofauti na ramani ya awali.

“Tunajua ni kosa kuongeza kitu chochote wakati wa ujenzi tofauti na maelekezo ya ramani, lakini tunafanya kazi kwa matakwa ya mmiliki, kwani kazi yetu ni kutekeleza kile anachohitaji mteja kwa wakati huo,” anasema Kambi.

Anasema kingine kinachochangia ni kutokuwepo kwa ukaguzi wa mara kwa mara, kwani yapo majengo yanakaguliwa mtu akishamaliza hatua fulani, kisha wanakuja kuweka alama za kusimamisha au kubomoa.

Serikali imeonya wamiliki na waendelezaji wa majengo wanaojenga kinyume na michoro na vibali vilivyoidhinishwa, ikisema hatua hiyo ni ukiukaji wa sheria na inaweza kuhatarisha usalama wa majengo.

Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Dk Festo Dugange, anasema kabla ya kuanza ujenzi, mjenzi anatakiwa kufuata taratibu, ikiwamo kupata michoro ya jengo, kuidhinishwa na mamlaka husika na kupata kibali cha ujenzi.

Anasema kibali huzingatia mambo mbalimbali, ikiwamo aina ya jengo, eneo linapojengwa, ukubwa wake, idadi ya ghorofa, aina ya udongo na, kwa baadhi ya miradi, tathmini ya athari za mazingira.

Dk Dugange anasema mjenzi anapaswa kujenga kulingana na kibali alichopewa na hawezi kuomba ghorofa mbili, kisha kuongeza ghorofa nyingine bila kupata idhini ya mamlaka husika.

“Ukiomba kibali cha ghorofa mbili, huwezi kujenga ghorofa tatu. Hilo ni kosa kisheria,” anasema.

Anasema Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masharti ya vibali vya ujenzi, huku wataalamu wa Serikali wakifanya ukaguzi katika maeneo mbalimbali kuhakikisha ujenzi unazingatia sheria, ubora na viwango vinavyotakiwa.

Anasema ikibainika jengo linajengwa kinyume na kibali, hatua huchukuliwa, ikiwamo kusimamisha ujenzi na kuchukua hatua za kisheria kulingana na aina ya ukiukwaji.

Pia, anasisitiza umuhimu wa serikali za mitaa kushiriki katika ufuatiliaji wa ujenzi unaoendelea katika maeneo yao.

Anasema viongozi na watendaji wa serikali za mitaa wana wajibu wa kufuatilia shughuli za ujenzi na kutoa taarifa pale wanapoona ukiukwaji wa taratibu.

Anasema ufuatiliaji hufanyika hatua kwa hatua ili kuhakikisha kile kilichoombwa na kuidhinishwa ndicho kinachojengwa. 

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Jamhuri yafunga ushahidi kesi ya Lissu

Next

Miaka 10 ya kusubiri mradi, wananchi wabebeshwa zigo la gharama – 1

No Comment! Be the first one.

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • MAGAZETINI LEO IJUMAA AGOSTI 14/2026:TRA KUVUKA MALENGO KWAMGUSA BALOZI OMARI,MADAKTARI BINGWA WAPIGA KAMBI HOSPITAL YA TOSAMAGANGA IRINGA…
  • SUA YASISITIZA MAWASILIANO YA KISAYANSI KUFIKISHA MATOKEO YA UTAFITI KWA JAMII
  • MAHAFALI YA DARASA LA SABA 2026 ST DOMINIC SAVIO IRINGA PICHA ZOTE HIZI HAPA
  • ASKOFU MIHALI AWATAKA WAZAZI KUENDANA NA DIRA 2050 KWA KUWEKEZA KATIKA ELIMU
  • Ziara ya Rais Tshisekedi kufungua ukurasa mpya wa biashara, amani

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme