Skip to content
-
Subscribe to our newsletter & never miss our best posts. Subscribe Now!
  • https://www.facebook.com/
  • https://twitter.com/
  • https://t.me/
  • https://www.instagram.com/
  • https://youtube.com/
Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

Habarimpya

Habari Mpya Kilasiku

  • Home
  • Sample Page
  • Home
  • Sample Page
Subscribe
Close

Search

Habari

Wadau wataka mipango ya tabianchi izingatie jinsia

By admin
August 17, 2026 3 Min Read
0

Dar es Salaam. Wakati dunia ikiendelea kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi, wadau wameonya kuwa vita hiyo haitakuwa na tija iwapo haitazingatia masuala ya kijinsia, hususan haki za afya ya uzazi na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Onyo hilo linakuja wakati tathmini ya mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika wilaya ya Kinondoni kuanzia mwaka 2013/14 hadi 2024/25 ikionyesha kuwa juhudi nyingi zimejikita zaidi kwenye miundombinu kama usafishaji wa mifereji na utunzaji wa mazingira, huku mahitaji maalumu ya wanawake, watoto na watu wenye ulemavu yakiachwa pembezoni.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Shirika la My Legacy, Fortunata Temu, amesema makundi hayo yameendelea kubeba mzigo mkubwa wa athari za tabianchi, ikiwemo ukosefu wa maji safi, ongezeko la magonjwa na vitendo vya ukatili vinavyochochewa na mazingira magumu ya kiuchumi na kijamii.


Amesema kupitia mradi wa “Kesho Njema”, shirika hilo lilifanya tathmini katika kata za wilaya ya Kinondoni na kubaini kuwa mipango mingi ya tabianchi haijajumuisha mtazamo wa kijinsia ipasavyo.

“Wengi huwa wanaangalia athari za mabadiliko ya tabianchi kwenye upande wa mazingira tu. Ukweli ni kwamba zipo athari nyingine ambazo zinawakumba moja kwa moja wanawake, watoto hata watu wenye ulemavu, lakini mipango iliyopo haingalii kwa jicho hilo.

“Tulibaini kuwa ushirikiano kati ya idara za mazingira, afya na jinsia bado ni mdogo. Pia, takwimu zilizogawanywa kijinsia hazitoshelezi, na ushiriki wa wanawake, vijana na makundi yaliyotengwa katika uamuzi wa tabianchi ni hafifu,” amesema Fortunata.

Ameongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi ni ajenda mtambuka inayohitaji kuangaliwa kwa upana wake, akisisitiza umuhimu wa kuingiza viashiria vya haki za afya ya uzazi na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia katika mikakati ya tabianchi kuanzia ngazi za mitaa.

Fortunata amesema ni muhimu pia kuimarisha uratibu wa kisekta na kutenga bajeti zinazozingatia jinsia ili kuhakikisha hakuna kundi linaloachwa nyuma katika harakati za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu wa shirika hilo, Amina Ally, amesema mbali na tathmini, mradi huo uliotekelezwa kwa mwaka mmoja kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, umewezesha utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kukabiliana na athari za tabianchi kwa vitendo.

Mkurugenzi wa shirika la My Legacy Fortunata Temu (kushoto) akizungumza kuhusu athari za mabadiliko ya tabia nchini. Kulia ni mratibu wa programu Amina Ally.

Amesema miti 2,000 ya kivuli na matunda imepandwa katika shule 24 za Wilaya ya Kinondoni ili kupunguza joto na kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Wanafunzi pia wamepatiwa mafunzo ya upandaji na utunzaji wa miti, pamoja na matumizi ya mifumo rahisi ya umwagiliaji kwa kutumia chupa za plastiki zilizotumika, hatua inayosaidia kupunguza taka ngumu.

“Jumla ya wanafunzi 775 kutoka shule 25 wamefikiwa kupitia vilabu vya WASH kwa vipindi maalumu vya elimu ya tabianchi. Tumetumia mbinu shirikishi kama maigizo, hadithi na sanaa kuwajengea uelewa kuhusu matumizi sahihi ya nishati, uhifadhi wa mazingira na uhusiano wa tabianchi na masuala ya kijinsia,” amesema Amina.

Aidha, shirika hilo liliandaa mdahalo wa kijamii uliopewa jina la ‘Mgahawa wa Maarifa’ uliowakutanisha viongozi wa mitaa, wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujadili changamoto na suluhisho za tabianchi katika maeneo yao.

Akichangia katika mdahalo huo, mkazi wa Kawe, Richard Mtanga, amesema kuwa haitawezekana kuwa na mkakati madhubuti wa tabianchi bila kushughulikia kwa uzito masuala ya kijinsia.

“Hakuna mkakati madhubuti wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi iwapo hautashughulikia ukatili wa kijinsia na kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi na haki zake. Ulinzi na utu lazima viwe sehemu ya hatua za kukabiliana na tabianchi,” amesema.

Author

admin

Follow Me
Other Articles
Previous

Afrika kugeukia teknolojia ya AI kuimarisha usalama wa mitihani

Next

Wakurugenzi wa Halmashauri wabebeshwa zigo la mazingira

No Comment! Be the first one.

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • UBORA WA SHULE ZA ST DOMINIC SAVIO ,WAPONGEZWA NA WAZAZI
  • FEASSA 2026 KUFANYIKA MOROGORO, WANAFUNZI 6,800 KUSHIRIKI MASHINDANO
  • Vijana wa Mwanjelwa walivyogeuza kucha, rangi kuwa dili
  • MAGAZETINI LEO JUMATANO AGOSTI 12/2026:TANZANIA NA MAREKANI KUENDELEA KUSHIRIKIANA,RC KHERI APONGEZA UWEKEZAJI HOTELI YA GOLDEN GLOW ..
  • GIZ YAAHIDI KUTOA EURO MILIONI 39.8 KWA AJILI YA KUIMARISHA BIASHARA YA KIKANDA.

Recent Comments

  1. A WordPress Commenter on Hello world!

Archives

  • August 2026

Categories

  • Habari
  • Magazeti
Copyright 2026 — Habarimpya. All rights reserved. Blogsy WordPress Theme