Kizimkazi yaaga kero ya maji, Rais Samia atoa neno
Unguja. Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kero ya maji iliyodumu kwa muda mrefu Kizimkazi na maeneo mengine ya Kusini Unguja, imefikia mwisho, baada ya kuzindua miradi miwili ya maji huku akiwataka wananchi kuitunza miundombinu hiyo.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Agosti 13, 2026, alipozungumza na wananchi wa Kizimkazi Kibuteni, Mkoa wa Kusini Unguja baada ya kuzindua miradi hiyo ikiwa ni sehemu ya shughuli za Tamasha la Kizimkazi.
Miradi hiyo inahusisha chanzo cha maji chenye uwezo wa kuzalisha lita milioni 2.4 kwa siku na tanki lenye ujazo wa lita milioni moja.
Rais Samia amesema Kizimkazi na Kusini kwa jumla zinakabiliwa na changamoto kubwa ya maji kwa muda mrefu, lakini utekelezaji wa miradi hiyo umeiwezesha Serikali kumaliza tatizo hilo.
“Leo tatizo la maji tumelihitimisha. Ndugu zangu wa Kusini, Kibuteni na Kizimkazi, tujipongeze sana,” amesema.
Amesema chanzo cha maji Kizimkazi kilijengwa mwaka 1974 kikiwa na tanki lenye ujazo wa lita 150,000, lakini baadaye kilishindwa kukidhi mahitaji kutokana na ukuaji wa eneo hilo na uwekezaji ulioongezeka.
Amesema Serikali haikuangalia mahitaji ya sasa pekee, ambayo ni takribani lita 500,000, bali imezingatia mahitaji ya baadaye kutokana na ongezeko la watu, miji na uwekezaji.
Rais Samia amewataka wananchi kuwa walinzi wa miundombinu hiyo, akisema Serikali imetumia fedha na utaalamu mkubwa kuitekeleza.
“Tumetengenezewa, tutunze tusiharibu. Tunajua tulipotoka, tulikuwa na tatizo kubwa la maji. Leo tumepata ufumbuzi wa maji, tutunze miundombinu hii na sisi tuwe walinzi kuilinda sisi wenyewe,” amesema.
Katika ziara hiyo, Rais Samia amepanda mti, amepokea gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya Kizimkazi na kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa Chuo cha Amali unaotekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Zanzibar.
Kuhusu Kituo cha Afya Kizimkazi, amesema kinaendelea kuboreshwa na sasa kinatarajiwa kutoa huduma zinazokaribia kiwango cha hospitali ya wilaya, ikiwamo huduma za dayalisisi kwa gharama nafuu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akizindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja Agosti 13, 2026.
Amesema kituo hicho pia kitakuwa na chumba maalumu cha mazoezi ya viungo kitakachotumiwa na wachezaji pamoja na watoto wanaozaliwa wakiwa na changamoto mbalimbali.
Amesema uwanja wa mpira wa Samia Academy unaojengwa katika eneo hilo unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu au Januari 2027, hivyo kituo hicho kitakuwa muhimu katika kutoa huduma za afya kwa wachezaji.
Pia, amesema gari la wagonjwa lililotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO) litasaidia kuboresha huduma za afya katika kituo hicho.
Rais Samia amesisitiza kuwa, wananchi wanapaswa kutunza miradi hiyo kwa kuwa ni uwekezaji unaolenga kuboresha maisha yao.
“Hii ni maisha yetu, fursa yetu, uchumi na ustawi wa wananchi,” amesema.
Pia, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani na kuunga mkono maendeleo yanayotekelezwa na Serikali.
‘Maji yamefika vijiji 10,756’
Waziri wa Maji, Juma Aweso amesema Serikali imefanya maendeleo makubwa katika sekta ya maji na kufikisha huduma hiyo kwa asilimia 85 kwa wananchi nchini.
Amesema kati ya vijiji 12,333 vilivyopo Tanzania, 10,756 vimefikiwa na huduma ya maji, huku vijiji 1,575 vikiwa katika hatua za kukamilisha miradi.
“Hakuna kijiji kitakachopitwa bila kupewa maji,” amesema Aweso.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akizindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja Agosti 13, 2026.
Amesema utekelezaji wa miradi ya Kizimkazi umetokana na maelekezo ya Rais Samia na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi yaliyolenga kuhakikisha tatizo la maji katika eneo hilo linamalizika.
Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Hamida Mussa Khamis amesema wananchi wameanza kuona faida ya mradi huo na kuahidi kulinda miundombinu yake.
Baadhi ya wananchi wameeleza furaha yao, wakisema changamoto ya maji iliyodumu kwa miaka mingi sasa inaanza kuwa historia.
Mwachumu Haji, mkazi wa Kizimkazi, amesema hali ya upatikanaji wa maji ilikuwa mbaya, lakini sasa matumaini ya kupata huduma hiyo yameongezeka.
Juma Kamis Juma amesema wananchi watahakikisha wanailinda miradi hiyo kwa sababu wanaufahamu uchungu wa kukosa maji.

