Category: Uncategorized

  • Mahakama kuamua Kesi ya Lissu Ijumaa

    Mahakama kuamua Kesi ya Lissu Ijumaa

    Dar es Salaam. Hatima ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, katika kesi ya uhaini inayomkabili imeingia katika hatua muhimu, baada ya Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam kupanga Ijumaa, Agosti 21, 2026, kutoa uamuzi mdogo wa kubaini kama ana kesi ya kujibu au la.

    Uamuzi huo unakuja baada ya upande wa Jamhuri kufunga ushahidi wake jana Jumatatu, Agosti 17, baada ya kuwaita mashahidi 17 kati ya 30 walioorodheshwa.

    Lissu, anafikisha siku 495 akiwa kizuizini hadi leo Agosti 17, 2026, alikamatwa Aprili 9, 2025 katika Wilaya ya Mbinga, Mkoa wa Ruvuma, kwenye mkutano wa hadhara wa Chadema.

    Kesi hiyo inatokana na shtaka moja la uhaini chini ya Kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, likihusishwa na maneno aliyodaiwa kuyatamka Aprili 3, 2025 kuhusu kuzuia Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

    Leo Agosti 17, 2026 Jamhuri imeeleza haitaita mashahidi   wote 30 waliokuwa kwenye orodha ikifafanua kuwa baada ya kupitia ushahidi uliowasilishwa na kuangalia wa mashahidi waliobaki, umeona uliopo unatosheleza. Hivyo uamuzi wa Agosti 21, 2026 utakaoweka mwelekeo wa hatua inayofuata.

    Iwapo mahakama itaona Jamhuri imefeli kujenga kesi, Lissu hatalazimika kuingia katika hatua ya kujitetea na anaweza kuachiwa kwa mujibu wa uamuzi wa mahakama. Lakini iwapo majaji wataona kuna ushahidi unaomtaka ajibu mashtaka, kesi itaingia katika hatua ya utetezi na Lissu atalazimika kujibu ushahidi uliowasilishwa dhidi yake.

    Kesi hiyo inasikilizwa na jopo la majaji watatu, Dunstan Ndunguru, James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.

    Safari ya Lissu mahakamani

    Katika kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja akiwa mahabusu, Lissu amekutana na vikwazo kadhaa vya kisheria, huku baadhi ya mapingamizi yake yakikubaliwa na mengine yakitupiliwa mbali.

    Miongoni mwa hatua kubwa ilikuwa Septemba 22, 2025, Mahakama Kuu ilipotupilia mbali mapingamizi yake kuhusu uhalali wa hati ya mashtaka.

    Mahakama ilisema hati hiyo ilikuwa inakidhi matakwa ya kisheria, huku suala la nia ya kutenda uhaini likielezwa kuwa ni jambo la ushahidi litakaloamuliwa wakati wa usikilizwaji wa kesi.

    Oktoba 2025, Lissu aliwasilisha mapingamizi manne kupinga kupokelewa kwa vielelezo vya video na vifaa vya kuhifadhia taarifa vilivyowasilishwa na upande wa Jamhuri.

    Baadaye, katika hatua nyingine ya kesi, aliwasilisha mapingamizi matano kuhusu masuala yanayohusiana na shahidi wa siri na kizimba kilichotengenezwa mahakamani kwa ajili ya mashahidi hao.

    Februari 11, 2026, Mahakama Kuu ilitupilia mbali mapingamizi manne kati ya matano, lakini ikakubali moja lililohusu kizimba cha shahidi wa siri.

    Mahakama iliamuru kifanyiwe marekebisho ili majaji waweze kumuona shahidi wakati akitoa ushahidi.

    Kwa maana hiyo, katika hatua hizo mbili zinazojulikana wazi, Lissu aliwasilisha jumla ya mapingamizi tisa, ingawa si yote yalikuwa na mada moja.

    Kati ya mapingamizi hayo, mahakama ilikubali mawili huku moja likihusu kielelezo cha video na jingine kuhusu kizimba cha shahidi wa siri, wakati mengine yalitupwa.

    Katika hoja zake Lissu ameieleza mahakama hiyo kuwa Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki iliweka msingi wa uthibitishaji wa kosa la uhani ili mshtakiwa awe na kesi ya kujibu kupitia kesi za Grey Likungu Mataka na wenzake dhidi ya Jamhuri na  Hatibu Gandhi na wenzake dhidi ya Jamhuri.

    Amesema kuwa mahakama hiyo iliweka masharti matatu ambayo ni mshtakiwa awe na utiifu kwa Jamhuri ya Muungano, nia ya kutenda kosa la uhaini, uthibitisho wa nia hiyo kwa maandishi au kwa matendo ya wazi.

    Pia, amedai kuwa mahakama hiyo ilisema maneno matupu hayatengenezi kosa la uhaini isipokuwa kama yataendana na kosa la uhaini, hata hivyo msimamo huo unatumika pale ambapo mshtakiwa wa uhaini ni mmoja.

    Kuhusu utiifu amesema kuwa halina mjadala kwani ni  raia wa Tanzania.

    Ameeleza kuwa kosa linalotajwa katika kifungu anachoshtakiwa ni kuitishia Serikali, Bunge au Mahakama na lazima nia hiyo idhihirishwe kwa kuchapisha maandishi au kwa kuonesha matendo ya wazi ni kosa la uhaini.

    Amesema kuwa kwa kurejea hati ya mashtaka maneno aliyoyatamka ya kuzuia uchaguzi si miongoni mwa makosa  kwa mujibu wa kifungu hicho cha  Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2025 au sheria yoyote nchini.

    Amesisitiza kuwa katika maneno hayo hakuna mahali alikotamka Serikali, Bunge wala mahakama, rais, waziri mkuu au mkuu wa mkoa lakini mashahidi hawakuthibitisha akisisitiza kuwa uchaguzi husimamiwa na Tume ya Uchaguzi na si Serikali.

    Kuhusu kuchapisha au kuonesha  matendo ya wazi, amedai kuwa Jamhuri haikuweza kuthibitisha kuwa ni yeye aliyechapisha maneno hayo kwenye mtandao wa Youtube wa  Jambo TV na   hata hiyo video hawakuiwasilisha mahakamani.

    Badala yake amesema kuwa shahidi wa 17 ambaye ndiye alikuwepo katika mkutano wake alieleza kuwa yeye, shahidi huyo na wenzake watano ndio waliorekodi na kuchapisha video hiyo.

    “Kwa hiyo kudhihirisha nia ya uhaini kama ilivyowekwa kwenye  kesi ya Grey na Gandhi haupo na hakuna ushahidi wa nia ya kutenda kosa lolote kwa mujibu wa sheria za Tanzania zinazojulikana”, amesema Lissu.

    Amesisitiza kuwa ameshtakiwa kwa kosa lisilokuwepo kisheria kwa mujibu wa Sheria za Uchaguzi na kwamba amekaa gerezani kwa siku 496 kwa kitendo ambacho si kosa la uhaini wala kosa kwa mujibu wa sheria yoyote nchini bali kwa mashtaka ya uonevu na ya kijinga.

    Hivyo, ameiomba mahakama iamuru alipwe fidia kwa uonevu huo wa kukaa gerezani kwa muda wote huo kwa mujibu wa kifungu cha 367 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).

    Jamhuri katika hoja zake kupitia Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga, ameieleza mahakama kuwa kwa kuzingatia ushahidi uliowasilishwa wamethibitisha viini vyote vya kosa la uhaini na kwamba kwa mshtakiwa anapaswa kujitetea.

    “Sisi Jamhuri tunaona mshtakiwa ana kesi ya kujibu katika mashtaka alivyoshtakiwa nayo chini ya kifungu  cha 39(2) (d) cha Penal code.

    Akichambua hati ya mashtaka, Katuga alidai kuwa kiini cha kwanza cha nia ya kutenda kosa mshtakiwa huyo ni kwamba yeye ni raia wa Tanzania,  anawajibu wa kutii sheria kwa mujibu wa katika ya Muungano wa Tanzania, kiini hicho kina thibitisha kuwa mshtakiwa anakiri kuwa yeye ni Mtanzania

    Kiini cha pili, cha nia ya uhaini amesema kuwa maneno aliyoyasema  mshtakiwa ya kukinukisha na kuvuruga uchaguzi yalilenga kuchochea umma  kwa nia ya kuitishia Serikali.

    Alidai kiini hicho kimedhibitisha na shahidi wa kwanza, wa 16 na wa tatu, ambapo kwa pamoja walisema maneno ya mshtakiwa ya kwamba watavuruga uchaguzi, yalitishia Serikali kwani ndio ina jukumu la kulinda sheria.

    Amesisitiza kuwa kuitishia Serikali lazima mpaka iwe imetishika bali hata kuonesha nia hiyo ni kosa la uhaini chini ya kifungu hicho.

    “Tunaomba mahakama ione ushahidi ulitolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka, mshtakiwa anao wajibu wa kujitetea, hivyo anatakiwa aletwe mahakamani kwa ajili ya kujitetea,” amesema  Katuga

    Kuhusu ombi la mshtakiwa kulipwa fidia, amesema kuwa hoja hiyo hawataijibu kwa sasa mpaka ambapo Mahakama itamkuta na kesi ya kujibu.

    Baada ya kusikiliza hoja za pande zote Jaji Ndunguru amesema kwa kuwa mashahidi ni wengi na hoja ni nyingi wanahitaji kupata muda wa kupitia ushahidi na hoja hizo na Mahakama itatoa uamuzi wake Agosti 21, 2026.

  • Nishati mbadala yatajwa kuwa suluhu ya uharibifu wa mazingira

    Nishati mbadala yatajwa kuwa suluhu ya uharibifu wa mazingira

    Tabora. Matumizi ya nishati mbadala yameendelea kutajwa kuwa suluhu ya kudumu ya kukabiliana na uharibifu wa mazingira na changamoto za kiafya zinazotokana na matumizi ya nishati isiyo rafiki kwa mazingira, huku wadau wakihimizwa kuwekeza na kuhamasisha matumizi yake kwa wananchi.

    Katika muktadha huo, washiriki wa kozi ya 14 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania (NDC) wapo mkoani Tabora kwa ziara ya siku sita ya mafunzo kwa vitendo, yenye lengo la kulinganisha nadharia waliyojifunza darasani na utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali katika mazingira halisi.

    Ziara hiyo ni sehemu ya tathmini ya utekelezaji wa sera za kitaifa katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii, ambapo washiriki wametembelea kiwanda cha kutengeneza majiko banifu, mashine za kuzalisha mkaa mbadala pamoja na uzalishaji wa mkaa huo.

    Akizungumza leo Januari 13, 2026 wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania, Brigedia Jenerali Charles Ndiege amesema matumizi ya nishati mbadala yanapaswa kuendelea kuhamasishwa kutokana na mchango wake katika kulinda mazingira na kuboresha afya za watumiaji.

    Amesema kupitia ziara hiyo, wanatazama kwa kina namna sera za kitaifa zinavyotekelezwa katika ngazi ya mikoa, ikiwemo sera za afya, mazingira, usalama, elimu, kijamii na kisiasa, akisisitiza kuwa miradi ya mkaa mbadala ni miongoni mwa suluhu za kupunguza uharibifu wa mazingira.

    “Tukiwa na miradi kama hii maeneo mengi na bei ikawa rafiki, itawawezesha wananchi na taasisi kutumia mkaa mbadala, kuhifadhi misitu yetu na kuboresha afya za watu kwa kupunguza hewa chafu,” amesema Ndiege.

    Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tabora ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kaliua, Gerald Mongela amesema mkoa huo upo salama na washiriki wa kozi hiyo wataendelea kuwa salama katika kipindi chote cha ziara yao.

    Aidha, Kanali Samwel Oloko kutoka nchini Kenya, ambaye ni mshiriki wa kozi hiyo, amesema mafunzo ya vitendo wanayoyapata ni fursa muhimu kwao kuyatumia katika mataifa yao.

    “Sasa takataka nyingi zina thamani kwa kuwa zinaweza kutumika kuzalisha nishati na kulinda mazingira,” amesema Oloko.

    Naye mshiriki wa kozi hiyo kutoka Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Godfrey Fumbuka amesema usalama wa mazingira ni msingi wa ulinzi wa Taifa.

    Muonekano wa mkaa mbadala ukiwa  unawaka kwenye jiko tayari lwa ajili kupikia.

    “Mazingira yakiharibika, watu hawawezi kuishi kwa amani, na hatimaye usalama wa taifa huathirika. Ni muhimu kutumia nishati mbadala kulinda mazingira,” amesema.

    Kwa upande wake, mkurugenzi wa kiwanda cha kuzalisha mkaa mbadala, Leonard Kushoka ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwaunga mkono wawekezaji wa ndani, huku akiomba kupanuliwa kwa masoko ya bidhaa hiyo.

    “Bado soko la mkaa mbadala halijapanuka vya kutosha, ilihali ni bidhaa rafiki kwa mazingira na inastahili kupata masoko makubwa zaidi,” amesema Kushoka.

  • MUHAS yaanzisha tiba ya kibingwa ya kinywa, meno kwa watoto

    MUHAS yaanzisha tiba ya kibingwa ya kinywa, meno kwa watoto

    Dar es Salaam. Watoto wenye matatizo ya meno nchini wameanza kupata huduma kutoka kwa madaktari bingwa baada ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kuanzisha kituo maalumu cha huduma za afya ya kinywa na meno kwa watoto.

    Kituo hicho, kilicho chini ya Shule Kuu ya Afya ya Kinywa na Meno, ni cha kwanza nchini kutoa huduma maalumu kwa watoto na tayari kimeanza kutoa huduma kwa majaribio tangu Mei mwaka huu.

    Makamu Mkuu wa MUHAS, Profesa Appolinary Kamuhabwa, akizungumza leo Jumatatu, Agosti 17, 2026, jijini Dar es Salaam, amesema watoto 27 wamepatiwa matibabu tangu huduma hiyo ilipoanza.

    Amesema miongoni mwa matatizo yanayowakabili watoto ni kuoza kwa meno, meno kupishana, saratani na changamoto nyingine za afya ya kinywa ambazo sasa zitaweza kushughulikiwa na madaktari bingwa.

    Profesa Kamuhabwa amesema kuanzishwa kwa kituo hicho ni sehemu ya ushirikiano kati ya Tanzania na Uturuki kupitia Shirika la Ushirikiano na Uratibu la Uturuki (TİKA) na Chuo Kikuu cha Ankara.

    “Tuna kitengo cha upasuaji ambapo mtoto huletwa, hufanyiwa uchunguzi na, inapobidi, hupatiwa matibabu chini ya dawa za usingizi. Huduma hii ni muhimu kwa sababu wapo watoto wenye mahitaji maalumu, wakiwamo wenye mtindio wa ubongo, ambao awali ilikuwa vigumu kuwahudumia,” amesema.

    Amesema utaratibu huo pia unawasaidia watoto wanaoogopa sindano, kwa kuwa wanaweza kupewa dawa za usingizi wakati wa matibabu badala ya kutegemea njia za kawaida za ganzi.

    Katika ushirikiano huo, amesema madaktari bingwa wa kinywa na meno, wataalamu wa usingizi, wauguzi na wataalamu wa maabara wamepata mafunzo katika Chuo Kikuu cha Ankara.

    Takwimu za Wizara ya Afya za mwaka 2025 zinaonesha asilimia 76.5 ya Watanzania wenye umri wa miaka 15 na zaidi wamewahi kuathiriwa na kuoza kwa meno, huku asilimia 31.1 ya watoto wakiwa na tatizo la kuoza meno ya utotoni.

    Aidha, asilimia 68 ya watu wazima nchini wanakabiliwa na magonjwa ya fizi, huku tatizo hilo likiwakabili asilimia 57 ya watoto.

    Takwimu hizo pia zinaonesha kuwa takriban asilimia 31 ya watoto wana changamoto ya mpangilio usio sahihi wa meno.

    Mafunzo ya huduma za dharura

    Profesa Kamuhabwa amesema ushirikiano kati ya Tanzania na Uturuki hauishii katika huduma za meno kwa watoto, bali pia unahusisha kuimarisha huduma za dharura.

    Amesema MUHAS imepokea gari maalumu kwa ajili ya mafunzo ya huduma za dharura na imeanza mpango wa kuwajengea uwezo watu ambao si madaktari ili waweze kutoa huduma za awali wakati wa dharura.

    Amesema mpango huo ni sehemu ya maandalizi ya kuimarisha huduma za afya kuelekea Michuano ya Mataifa ya Afrika (Afcon) 2027, ambayo Tanzania itakuwa mwenyeji mwenza pamoja na Kenya na Uganda.

    “Wakati wa dharura, mtu anaweza kupoteza maisha kutokana na kuhudumiwa vibaya. Wakati mwingine watu humshika mgonjwa au kumbania hewa bila kujua namna sahihi ya kumsaidia. Ndiyo maana katika ushirikiano huu tumekubaliana kuongeza uwezo wa wataalamu katika huduma za dharura,” amesema.

    Amesema maandalizi ya mashindano makubwa yanahitaji wataalamu wa kutosha, pamoja na watu wenye ujuzi wa kutoa huduma za awali za dharura.

    Kwa upande wake, Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Dk Bekir Gezer, amesema kuanzishwa kwa huduma hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano wa nchi hizo katika sekta ya afya.

    Naye Mkurugenzi Mkazi wa TİKA, Halim Omer, amesema ushirikiano na MUHAS utajikita katika kujenga uwezo wa wataalamu, kufanya tafiti, usomaji wa picha za kitabibu kwa kutumia akili bandia na kusaidia upatikanaji wa vifaa vya matibabu.

    Kwa mujibu wa MUHAS, ushirikiano huo pia umehusisha uboreshaji wa miundombinu ya Shule ya Meno na mafunzo ya wataalamu katika Chuo Kikuu cha Ankara.

  • Wakurugenzi wa Halmashauri wabebeshwa zigo la mazingira

    Wakurugenzi wa Halmashauri wabebeshwa zigo la mazingira

    Dodoma. Wakurugenzi wa halmashauri nchini Tanzania wameagizwa kusimamia na kuwa mfano wa kupunguza matumizi ya plastiki katika ofisi zao ili kulinda mazingira.

    Agizo hilo limetolewa leo Januari 17, 2026 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Profesa Peter Msofe wakati akizindua mradi wa urejeshaji wa mazingira na uoto wa asili.

    Mradi huo wa miaka mitano unasimamia na World Wildlife Fund (WWF) na kutekelezwa katika Wilaya za Mpwapwa na Chamwino (Dodoma) na Korogwe na Kilindi (Tanga).

    Profesa Msofe amesema ni aibu wakurugenzi kuwa waangalizi kwenye uharibifu wa mazingira na hawatakiwi kuwa wapanga kazi badala yake wawe wasimamizi wa kazi hizo wakianzia wao kuonyesha mfano.

    “Katika hili sitaki mkafanye, bali naagiza lazima litekelezwe tena iwe nchini nzima, na mshirikishe walio chini yenu na jamii inayowazunguka, lazima mtambue kwenye mazingira tuna hali mbaya na hivyo hatuwezi kucheka,” amesema Profesa Msofe.

    Kuhusu mradi huo amesema ni lazima uwe wa kiushindani katika mpango wa urejeshaji wa uoto wa asili ambapo Tanzania imejenga kufikia hekta milioni 5.2 wakati bara la Afrika ni hekta milioni 100 na kwa upande wa Dunia zinatakiwa kufikia hekta milioni 350 ifikapo 2050.

    Ofisa kutoka WWF Almas Kashindye ametaja lengo katika mradi huo ni kuboresha maisha ya wananchi na kulinda bayonuwai.

    Kashindye amesema mradi huo unagharimu Sh5.4 bilioni huku walengwa zaidi wakiwa watu wa vijijini katika wilaya zilizoonekana kuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira.

    Msimamizi wa mradi huo uliopewa jina la IKI Forest Landscape, Raymond Kallenga amesema mbali na Tanzania mpango huo unatekelezwa kwa nchi za Uganda, Madagasca, Brazil, Peru na Colombia na mfadhiri ni Ujerumani.

    Killenga anasema mkakati waliouweka ni ufuatiliaji zaidi katika kila hatua ili kuhakikisha wanapata matokeo kama ilivyo.

  • Wadau wataka mipango ya tabianchi izingatie jinsia

    Wadau wataka mipango ya tabianchi izingatie jinsia

    Dar es Salaam. Wakati dunia ikiendelea kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi, wadau wameonya kuwa vita hiyo haitakuwa na tija iwapo haitazingatia masuala ya kijinsia, hususan haki za afya ya uzazi na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

    Onyo hilo linakuja wakati tathmini ya mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika wilaya ya Kinondoni kuanzia mwaka 2013/14 hadi 2024/25 ikionyesha kuwa juhudi nyingi zimejikita zaidi kwenye miundombinu kama usafishaji wa mifereji na utunzaji wa mazingira, huku mahitaji maalumu ya wanawake, watoto na watu wenye ulemavu yakiachwa pembezoni.

    Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Shirika la My Legacy, Fortunata Temu, amesema makundi hayo yameendelea kubeba mzigo mkubwa wa athari za tabianchi, ikiwemo ukosefu wa maji safi, ongezeko la magonjwa na vitendo vya ukatili vinavyochochewa na mazingira magumu ya kiuchumi na kijamii.

    Amesema kupitia mradi wa “Kesho Njema”, shirika hilo lilifanya tathmini katika kata za wilaya ya Kinondoni na kubaini kuwa mipango mingi ya tabianchi haijajumuisha mtazamo wa kijinsia ipasavyo.

    “Wengi huwa wanaangalia athari za mabadiliko ya tabianchi kwenye upande wa mazingira tu. Ukweli ni kwamba zipo athari nyingine ambazo zinawakumba moja kwa moja wanawake, watoto hata watu wenye ulemavu, lakini mipango iliyopo haingalii kwa jicho hilo.

    “Tulibaini kuwa ushirikiano kati ya idara za mazingira, afya na jinsia bado ni mdogo. Pia, takwimu zilizogawanywa kijinsia hazitoshelezi, na ushiriki wa wanawake, vijana na makundi yaliyotengwa katika uamuzi wa tabianchi ni hafifu,” amesema Fortunata.

    Ameongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi ni ajenda mtambuka inayohitaji kuangaliwa kwa upana wake, akisisitiza umuhimu wa kuingiza viashiria vya haki za afya ya uzazi na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia katika mikakati ya tabianchi kuanzia ngazi za mitaa.

    Fortunata amesema ni muhimu pia kuimarisha uratibu wa kisekta na kutenga bajeti zinazozingatia jinsia ili kuhakikisha hakuna kundi linaloachwa nyuma katika harakati za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

    Kwa upande wake, Mratibu wa Programu wa shirika hilo, Amina Ally, amesema mbali na tathmini, mradi huo uliotekelezwa kwa mwaka mmoja kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, umewezesha utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kukabiliana na athari za tabianchi kwa vitendo.

    Mkurugenzi wa shirika la My Legacy Fortunata Temu (kushoto) akizungumza kuhusu athari za mabadiliko ya tabia nchini. Kulia ni mratibu wa programu Amina Ally.

    Amesema miti 2,000 ya kivuli na matunda imepandwa katika shule 24 za Wilaya ya Kinondoni ili kupunguza joto na kuboresha mazingira ya kujifunzia.

    Wanafunzi pia wamepatiwa mafunzo ya upandaji na utunzaji wa miti, pamoja na matumizi ya mifumo rahisi ya umwagiliaji kwa kutumia chupa za plastiki zilizotumika, hatua inayosaidia kupunguza taka ngumu.

    “Jumla ya wanafunzi 775 kutoka shule 25 wamefikiwa kupitia vilabu vya WASH kwa vipindi maalumu vya elimu ya tabianchi. Tumetumia mbinu shirikishi kama maigizo, hadithi na sanaa kuwajengea uelewa kuhusu matumizi sahihi ya nishati, uhifadhi wa mazingira na uhusiano wa tabianchi na masuala ya kijinsia,” amesema Amina.

    Aidha, shirika hilo liliandaa mdahalo wa kijamii uliopewa jina la ‘Mgahawa wa Maarifa’ uliowakutanisha viongozi wa mitaa, wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujadili changamoto na suluhisho za tabianchi katika maeneo yao.

    Akichangia katika mdahalo huo, mkazi wa Kawe, Richard Mtanga, amesema kuwa haitawezekana kuwa na mkakati madhubuti wa tabianchi bila kushughulikia kwa uzito masuala ya kijinsia.

    “Hakuna mkakati madhubuti wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi iwapo hautashughulikia ukatili wa kijinsia na kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi na haki zake. Ulinzi na utu lazima viwe sehemu ya hatua za kukabiliana na tabianchi,” amesema.

  • Afrika kugeukia teknolojia ya AI kuimarisha usalama wa mitihani

    Afrika kugeukia teknolojia ya AI kuimarisha usalama wa mitihani

    Arusha. Mabaraza ya mitihani barani Afrika yameshauriwa kutumia mifumo ya kidijitali, uchanganuzi wa data na akili unde (AI) kubaini na kudhibiti udanganyifu wa mitihani unaozidi kuwa wa kisasa, ili kuboresha ubora wa elimu na kuzalisha wanafunzi wenye ushindani katika soko la ajira.

    Wito huo umetolewa leo Jumatatu, Agosti 17, 2026, katika mkutano wa 42 wa mwaka wa Jumuiya ya Tathmini ya Elimu Afrika (AEAA), unaofanyika Arusha kwa siku nne na kuwakutanisha zaidi ya wajumbe 350 kutoka nchi 28 za Afrika na mabara mengine.

    Mkutano huo ulioandaliwa chini ya uenyeji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), umewakutanisha maofisa wa wizara za elimu, mabaraza ya mitihani, wataalamu wa tathmini na wadau wa elimu kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mifumo ya tathmini barani Afrika kutokana na kasi ya maendeleo ya teknolojia, hususan matumizi ya AI.

    Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Profesa Carolyne Nombo amesema njia za jadi za kulinda usalama wa mitihani hazitoshi tena kukabiliana na changamoto zinazotokana na matumizi ya simu janja, mitandao ya kijamii na AI.

    Amesema udanganyifu wa mitihani umebadilika kutoka mbinu za kawaida na sasa unaweza kufanyika kupitia vifaa na majukwaa ya kidijitali yanayowezesha taarifa kusambazwa kwa haraka.

    “Usalama wa mitihani haupaswi kuishia katika kuzuia mwanafunzi kuingia na nyenzo zisizoruhusiwa kwenye chumba cha mtihani, bali unapaswa kuanzia hatua ya uandaaji wa maswali hadi utoaji wa matokeo,” amesema.

    Amesema hatua hizo zinapaswa kujumuisha uandaaji na uchapishaji wa maswali, usafirishaji na uhifadhi wake, uendeshaji wa mitihani, usahihishaji, uchakataji wa taarifa na utoaji wa matokeo.

    “Kadiri teknolojia inavyoendelea, udanganyifu katika mitihani nao unazidi kuwa wa kisasa, huku simu janja, mitandao ya kijamii na AI zikitajwa miongoni mwa changamoto zinazohitaji mifumo mipya ya usalama,” amesema.

    Hata hivyo, Profesa Nombo amesema teknolojia hizo hazipaswi kuonekana kama tishio pekee, bali zitumike pia kutafuta suluhisho la changamoto hizo.

    “Niwahimize mabaraza ya mitihani barani Afrika kuwekeza katika mifumo imara ya usalama wa kidijitali, uchanganuzi wa data na zana zinazotumia AI ambazo zinaweza kusaidia kubaini viashiria vya udanganyifu na dosari katika mchakato wa mitihani,” amesema.

    Kwa upande wake, Rais wa AEAA, Dk Eshetu Kebede Gichoro, amesema pamoja na uwekezaji katika mifumo ya kiteknolojia, nchi za Afrika zinapaswa kuweka sera na miongozo ya wazi ya matumizi ya AI katika tathmini ya elimu.

    Amesema miongozo hiyo inapaswa kuzingatia maadili, uwazi, usalama wa data, usawa na haki kwa wanafunzi.

    Kwa mujibu wa Dk Gichoro, AI inatoa fursa kubwa za kuboresha mifumo ya tathmini, ikiwamo mitihani inayoweza kubadilika kulingana na uwezo wa mwanafunzi, uchanganuzi wa utabiri na uundaji wa njia binafsi za ujifunzaji.

    Hata hivyo, amesema teknolojia hiyo pia inazua maswali kuhusu usawa, maadili na umiliki wa data, hasa kwa nchi zinazotumia mifumo ya kiteknolojia inayotengenezwa nje ya Afrika.

    Amesema bara hilo linapaswa kujenga mifumo yake ya tathmini inayounganisha teknolojia na mahitaji yake, badala ya kutegemea mifumo ya nje ambayo huenda isiakisi uhalisia wa Afrika.

    “Endapo Afrika haitajenga mifumo yake huru ya tathmini inayounganisha teknolojia, tunahatarisha kuwa watumiaji wa mifumo iliyoagizwa kutoka nje ambayo huenda isiakisi uhalisia wala kutumikia matarajio yetu,” amesema.

    Katibu Mtendaji wa NECTA, Profesa Said Ally Mohamed amesema mkutano huo unalenga kutafakari namna mifumo ya tathmini inavyoweza kubadilishwa ili kukabiliana na kuongezeka kwa matumizi ya AI na teknolojia duniani.

    Amesema pia mkutano huo unatoa fursa kwa wataalamu kutoka nchi mbalimbali kubadilishana tafiti, uzoefu na ubunifu kuhusu matumizi ya teknolojia katika kuboresha tathmini ya elimu.

    “Pamoja na usalama wa mitihani, pia utaangazia namna data inayozalishwa kupitia tathmini inavyoweza kutumika katika kuboresha elimu,” amesema.

    Ameongeza kuwa mkutano huo utaangazia pia umuhimu wa kuhakikisha matumizi ya teknolojia hayawaachi nyuma wanafunzi kutoka maeneo yenye changamoto za kiuchumi, vijijini na makundi mengine yaliyo katika mazingira magumu.

  • CookFund yachochea mapinduzi ya nishati safi, wanafunzi 62,000 wanufaika

    CookFund yachochea mapinduzi ya nishati safi, wanafunzi 62,000 wanufaika

    Dar es Salaam. Zaidi ya wanafunzi 62,000 nchini wamenufaika na matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na usakinishaji wa majiko ya kisasa katika shule na taasisi za umma zaidi ya 45, huku idadi ya majiko ikizidi 170.

    Hatua hiyo imechukuliwa kupitia programu ya CookFund, inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na kutekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF).

    Hayo yamesemwa leo Alhamisi, Machi 26, 2026, katika hafla ya makabidhiano ya msaada huo iliyofanyika katika Shule ya Msingi Bunge, jijini Dar es Salaam, ikionesha hatua muhimu katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, pamoja na kukabiliana na changamoto ya ukataji miti.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kipaumbele cha kimkakati cha Taifa katika kulinda mazingira, kuboresha afya ya jamii, na kuongeza ufanisi wa kiuchumi.

    Amesema kwa kuzipatia shule na taasisi za umma teknolojia za kisasa za kupikia, Serikali inalenga kupunguza hewa chafuzi, kulinda rasilimali za misitu, na kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.

    “Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa kuzingatia Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024 hadi 2034,” amesema Naibu Waziri Makamba.

    Jitihada za kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini zinaongozwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali, zikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu – Tamisemi, Wizara ya Maliasili na Utalii, na Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira.

    Mpango huo unalenga taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 kwa wakati mmoja, hususan shule, ili kuondokana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa mazingira, kama kuni na mkaa.

    Akizungumza kwa niaba ya Umoja wa Ulaya, Mkuu wa Ushirikiano nchini Tanzania, Marc Stalmans, amesema mpango huo ni sehemu ya juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kusaidia mpito kuelekea matumizi ya nishati safi.

    “Tunasaidia watu kuhamia kwenye mbinu endelevu zinazolinda mazingira huku zikichochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira, na kuboresha upatikanaji wa nishati katika sekta mbalimbali,” amesema.

    Kwa upande wake, Mshauri Mkuu wa Masuala ya Kiufundi wa UNCDF, Peter Malika, amesema programu hiyo imewekeza Dola milioni 10.1 za Marekani katika biashara ndogo na za kati 102, pamoja na kusaidia taasisi 45 katika wilaya 14 za mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, na Mwanza.

    Amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia yana mchango mkubwa katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, huku yakiboresha usalama, afya, na ufanisi katika shughuli za upishi shuleni.

    Kwa mujibu wa wataalamu, matumizi ya kuni na mkaa huchangia uzalishaji wa chembechembe hatarishi zinazosababisha magonjwa ya mfumo wa upumuaji, ikiwemo pumu na saratani ya mapafu.

    Kupitia CookFund, teknolojia mbalimbali za nishati safi zimeanza kutumika, zikiwemo majiko ya umeme, majiko ya bayoethanoli, majiko banifu, pamoja na matumizi ya gesi na mkaa mbadala.

  • Kizimkazi yaaga kero ya maji, Rais Samia atoa neno

    Kizimkazi yaaga kero ya maji, Rais Samia atoa neno

    Unguja. Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kero ya maji iliyodumu kwa muda mrefu Kizimkazi na maeneo mengine ya Kusini Unguja, imefikia mwisho, baada ya kuzindua miradi miwili ya maji huku akiwataka wananchi kuitunza miundombinu hiyo.

    Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Agosti 13, 2026, alipozungumza na wananchi wa Kizimkazi Kibuteni, Mkoa wa Kusini Unguja baada ya kuzindua miradi hiyo ikiwa ni sehemu ya shughuli za Tamasha la Kizimkazi.

    Miradi hiyo inahusisha chanzo cha maji chenye uwezo wa kuzalisha lita milioni 2.4 kwa siku na tanki lenye ujazo wa lita milioni moja.

    Rais Samia amesema Kizimkazi na Kusini kwa jumla zinakabiliwa na changamoto kubwa ya maji kwa muda mrefu, lakini utekelezaji wa miradi hiyo umeiwezesha Serikali kumaliza tatizo hilo.

    “Leo tatizo la maji tumelihitimisha. Ndugu zangu wa Kusini, Kibuteni na Kizimkazi, tujipongeze sana,” amesema.

    Amesema chanzo cha maji Kizimkazi kilijengwa mwaka 1974 kikiwa na tanki lenye ujazo wa lita 150,000, lakini baadaye kilishindwa kukidhi mahitaji kutokana na ukuaji wa eneo hilo na uwekezaji ulioongezeka.

    Amesema Serikali haikuangalia mahitaji ya sasa pekee, ambayo ni takribani lita 500,000, bali imezingatia mahitaji ya baadaye kutokana na ongezeko la watu, miji na uwekezaji.

    Rais Samia amewataka wananchi kuwa walinzi wa miundombinu hiyo, akisema Serikali imetumia fedha na utaalamu mkubwa kuitekeleza.

    “Tumetengenezewa, tutunze tusiharibu. Tunajua tulipotoka, tulikuwa na tatizo kubwa la maji. Leo tumepata ufumbuzi wa maji, tutunze miundombinu hii na sisi tuwe walinzi kuilinda sisi wenyewe,” amesema.

    Katika ziara hiyo, Rais Samia amepanda mti, amepokea gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya Kizimkazi na kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa Chuo cha Amali unaotekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Zanzibar.

    Kuhusu Kituo cha Afya Kizimkazi, amesema kinaendelea kuboreshwa na sasa kinatarajiwa kutoa huduma zinazokaribia kiwango cha hospitali ya wilaya, ikiwamo huduma za dayalisisi kwa gharama nafuu.

    Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akizindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja Agosti 13, 2026.

    Amesema kituo hicho pia kitakuwa na chumba maalumu cha mazoezi ya viungo kitakachotumiwa na wachezaji pamoja na watoto wanaozaliwa wakiwa na changamoto mbalimbali.

    Amesema uwanja wa mpira wa Samia Academy unaojengwa katika eneo hilo unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu au Januari 2027, hivyo kituo hicho kitakuwa muhimu katika kutoa huduma za afya kwa wachezaji.

    Pia, amesema gari la wagonjwa lililotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO) litasaidia kuboresha huduma za afya katika kituo hicho.

    Rais Samia amesisitiza kuwa, wananchi wanapaswa kutunza miradi hiyo kwa kuwa ni uwekezaji unaolenga kuboresha maisha yao.

    “Hii ni maisha yetu, fursa yetu, uchumi na ustawi wa wananchi,” amesema.

    Pia, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani na kuunga mkono maendeleo yanayotekelezwa na Serikali.

    ‘Maji yamefika vijiji 10,756’

    Waziri wa Maji, Juma Aweso amesema Serikali imefanya maendeleo makubwa katika sekta ya maji na kufikisha huduma hiyo kwa asilimia 85 kwa wananchi nchini.

    Amesema kati ya vijiji 12,333 vilivyopo Tanzania, 10,756 vimefikiwa na huduma ya maji, huku vijiji 1,575 vikiwa katika hatua za kukamilisha miradi.

    Hakuna kijiji kitakachopitwa bila kupewa maji,” amesema Aweso.

    Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akizindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja Agosti 13, 2026.

    Amesema utekelezaji wa miradi ya Kizimkazi umetokana na maelekezo ya Rais Samia na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi yaliyolenga kuhakikisha tatizo la maji katika eneo hilo linamalizika.

    Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Hamida Mussa Khamis amesema wananchi wameanza kuona faida ya mradi huo na kuahidi kulinda miundombinu yake.

    Baadhi ya wananchi wameeleza furaha yao, wakisema changamoto ya maji iliyodumu kwa miaka mingi sasa inaanza kuwa historia.

    Mwachumu Haji, mkazi wa Kizimkazi, amesema hali ya upatikanaji wa maji ilikuwa mbaya, lakini sasa matumaini ya kupata huduma hiyo yameongezeka.

    Juma Kamis Juma amesema wananchi watahakikisha wanailinda miradi hiyo kwa sababu wanaufahamu uchungu wa kukosa maji.

  • Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini

    Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini

    Singida. Omary Mgana, amegonga mwamba katika jitihada zake za kudai fidia ya Sh40 milioni kutoka kwa mke wake wa zamani, Hadija Willa, akidai alimficha ujauzito wa mwanaume mwingine wakati akifunga naye ndoa mwaka 1997.

    Omary alidai Sh10 milioni alizotumia katika huduma za ujauzito na kujifungua, pamoja na Sh30 milioni alizodai kutumia kumlea na kumsomesha mtoto huyo hadi kufikia utu uzima.

    Alidai aligundua mwaka 2021, kwamba mtoto huyo ambaye wakati huo alikuwa na miaka 24, hakuwa wake. Pia, aliiomba mahakama iamuru kuondolewa kwa ubini wake katika nyaraka za mtoto huyo.

    Hata hivyo, Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Singida imetupilia mbali rufaa yake na kusimamia uamuzi wa Mahakama ya Wilaya ya Singida uliokataa madai hayo.

    Katika hukumu iliyotolewa Agosti 14, 2026 na Jaji, Ayoub Mwenda na kuwekwa kwenye tovuti ya Mahakama Agosti 17, 2026, ilieleza Omary alishindwa kuthibitisha kuwa alifichwa ujauzito huo.

    Jaji alisema madai ya kurejeshewa fedha yangekuwa na msingi kama Hadija angeuficha ujauzito wakati wa ndoa, lakini ushahidi ulionyesha Omary alikuwa akijua hali hiyo.

    “Nimepitia ushahidi uliopo na sijaona kasoro katika hitimisho la mahakama ya chini. Kama ilivyoelezwa kwa usahihi na mahakama ya chini, mdaiwa angeweza kuhukumiwa kwa kosa la kuficha ujauzito iwapo tu, katika siku ya harusi angeulizwa kama ana ujauzito au la, jambo ambalo halikutokea,” alisema.

    Kwa mujibu wa Jaji Mwenda, kumbukumbu za kesi zinaonyesha swali aliloulizwa Hadija siku ya ndoa lilikuwa kama alikuwa tayari kufunga ndoa na Omary.

    “Hakuna sheria inayomlazimisha mwanamke kusema kwa hiari kama ana mimba wakati wa kujiandaa kufunga ndoa ikiwa hajaulizwa,” alisema.

    Hivyo, Jaji alisema ushahidi ulionyesha Hadija alimweleza Omary kabla ya ndoa kwamba alikuwa na ujauzito wa mwanaume mwingine.

    Hadija katika utetezi wake alisema wakati Omary alipokuwa akimchumbia, alimweleza kuwa alikuwa na mwanaume mwingine aliyempa ujauzito, lakini Omary alisisitiza kumuoa akisema nyumba ya ndoa haizai mtoto haramu.

    Walipofunga ndoa mwaka 1997, Hadija alikuwa na ujauzito wa miezi minne hadi mitano na alijifungua Oktoba 10, 1997.

    Awali alimpa mtoto jina Mohamed Joseph, lakini Hadija alieleza kuwa Omary ndiye aliyesisitiza jina libadilishwe na baadaye mtoto akaitwa Juma Omary Juma Mgana.

    Katika madai yake, Omary alisema alimtunza mtoto huyo akiamini ni wake, akigharamia huduma za ujauzito, kujifungua, malezi na elimu.

    Alisema mwaka 2021 ndipo Hadija alipomweleza kuwa mtoto huyo si wake. Hata hivyo, katika shauri la talaka namba 14 la 2024, mahakama ilimwamuru kuendelea kumhudumia mtoto huyo kwa kutumia mapato ya kodi ya nyumba kugharamia matibabu na elimu hadi atakapofikia utu uzima.

    Omary pia alidai kuwa mwaka 2006 Hadija alibadili msimamo na kutangaza kuwa Juma hakuwa mtoto wake, jambo lililosababisha mtoto huyo kuhamishiwa kwa mjomba wake na baadaye shangazi yake.

    Juma aliyetoa ushahidi kama shahidi wa pili wa utetezi, alikanusha kupokea fedha kutoka kwa Omary kwa ajili ya elimu, akisema alisoma shule ya Serikali ambayo haikuwa na ada.

    Jaji Mwenda pia alikataa madai ya Omary kwamba alitumia Sh1.5 milioni kumlipia Hadija gharama za kujifungua, akisema hakuwasilisha ushahidi kuthibitisha fedha hizo zilitumika kwa matibabu.

    Kuhusu madai ya matumizi ya fedha za kodi, Jaji alisema katika shauri la talaka mahakama iligawa nyumba kwa asilimia 50 kwa 50, hivyo mapato yake hayakuwa ya mtoto huyo pekee.

    “Hata kama mdaiwa asingekuwa na sehemu ya asilimia 50 ya nyumba hiyo, jambo ambalo si kweli, mlalamikaji alishindwa kuwasilisha ushahidi wowote kuthibitisha mdaiwa alikuwa akikusanya kiasi cha Sh225,000 kwa mwezi kama ilivyodaiwa,” alisema.

    Jaji pia alisema Omary hakuthibitisha hasara au madhara halisi yaliyosababishwa na mwenendo wa Hadija.

    “Msongo wa mawazo pekee, bila uthibitisho, hauwezi kuwa sababu halali ya kutoa fidia ya jumla,” alisema.

    Aliongeza kuwa kwa kuwa Omary alijua ujauzito huo kabla ya ndoa, hakukuwa na udanganyifu uliosababisha hasara au madhara.

    “Kama ilivyobainishwa kwa usahihi na mahakama, mtoto huyo alilelewa kama sehemu ya familia; hivyo, madai ya kurejeshewa gharama hayana msingi wa kisheria. Rufaa hii inakataliwa na uamuzi wa Mahakama ya Wilaya unasimama,” alisema.

    Hata hivyo, kuhusu gharama za kesi, Jaji alisema kwa kuwa pande hizo bado zinashirikiana katika kulea watoto wengine, haikuwa mwafaka kumuamuru Omary kuzilipa kwa kuwa hatua hiyo isingeleta amani na maelewano katika familia ambayo imesambaratika.

  • DCEA yateketeza ekari 603 za bangi Morogoro

    DCEA yateketeza ekari 603 za bangi Morogoro

    Dar es Salaam. Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeanza operesheni maalumu ya kuharibu mashamba ya bangi mkoani Morogoro, baada ya kubaini wakulima kuhamia maeneo ya mbali ndani na nje ya Hifadhi ya Mikumi.

    Katika operesheni maalumu iliyofanyika kwa siku 14 katika vijiji vya Visengele na Lugenge wilayani Mvomero, DCEA imeteketeza ekari 603 za bangi,   kukamata magunia 49 ya bangi na watuhumiwa 13 kwa tuhuma za kujihusisha na kilimo cha dawa hizo za kulevya.

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Jumatatu Agosti 17, 2026 Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo operesheni hiyo ni mwendelezo wa kampeni maalumu ya kudhibiti dawa za kulevya zinazozalishwa nchini, hususani bangi, huku akieleza kuwa mamlaka imebaini baadhi ya wakulima wamehamia maeneo ambayo hayajawahi kufikiwa na operesheni za awali.

    Amesema pamoja na operesheni kufanyika katika maeneo hayo tangu mwaka 2023, bado wananchi wameendelea kulima bangi ndani ya Hifadhi ya Mikumi na maeneo ya nje ya hifadhi.

    “Katika operesheni tulizozifanya safari hii tumegundua kwamba wamelima mbali zaidi ya maeneo ambayo operesheni zilishafanyika awali, wakidhani mamlaka itashindwa kufika katika maeneo hayo,” amesema Lyimo.

    Lyimo amesema ukubwa wa mashamba yaliyobainika unaonyesha kuwa kilimo cha bangi bado ni changamoto katika baadhi ya maeneo ya Morogoro, hasa ndani ya hifadhi na katika vijiji vinavyozunguka maeneo ya mapori.

    “Maeneo haya yako mbali sana na vijiji na makazi ya wananchi, lakini mamlaka itaweka intelijensia ya kutosha ili kuhakikisha kwamba hizi operesheni na hawa wahalifu tutaendelea kuwakamata,” amesema.